Kitabu cha Kwanza cha Samweli 13:1-23

  • Sauli achagua jeshi (1-4)

  • Sauli atenda kwa kimbelembele (5-9)

  • Samweli amkaripia Sauli (10-14)

  • Waisraeli hawakuwa na silaha (15-23)

13  Sauli alikuwa na umri wa miaka . . .* alipowekwa kuwa mfalme,+ na kwa miaka miwili alitawala Israeli.  Sauli alichagua wanaume 3,000 katika Israeli; 2,000 kati yao walikuwa pamoja na Sauli kule Mikmashi na katika eneo lenye milima la Betheli, na 1,000 walikuwa pamoja na Yonathani+ katika jiji la Gibea+ la Benjamini. Aliwaruhusu waliobaki waende zao, kila mmoja kwenye hema lake.  Kisha Yonathani akaishambulia kambi ya kijeshi ya Wafilisti+ iliyokuwa Geba,+ na Wafilisti wakasikia habari hizo. Basi Sauli akaagiza pembe* ipigwe+ nchini kote, akisema: “Waebrania na wasikie!”  Waisraeli wote wakasikia habari hizi: “Sauli ameishambulia kambi ya kijeshi ya Wafilisti, na sasa Waisraeli wananuka mbele ya Wafilisti.” Basi watu wakakusanywa ili wamfuate Sauli huko Gilgali.+  Wafilisti pia wakakusanyika pamoja ili wapigane na Waisraeli, nao walikuwa na magari 30,000 ya vita na wapanda farasi 6,000 na wanajeshi wengi kama chembe za mchanga kwenye ufuo wa bahari;+ nao wakapanda na kupiga kambi kule Mikmashi upande wa mashariki wa Beth-aveni.+  Na wanaume wa Israeli wakaona kwamba walikuwa hatarini, kwa sababu watu walikuwa chini ya mkazo mkali; basi watu wakajificha ndani ya mapango,+ mashimo, miamba, mahandaki, na hifadhi za maji.  Hata baadhi ya Waebrania walivuka Yordani na kuingia nchi ya Gadi na Gileadi.+ Lakini Sauli alikuwa bado Gilgali, na watu wote waliomfuata walikuwa wakitetemeka.  Aliendelea kungoja kwa siku saba mpaka wakati uliowekwa na Samweli ulipofika, lakini Samweli hakuja Gilgali, na watu walikuwa wakitawanyika kutoka kwake.  Mwishowe Sauli akasema: “Nileteeni dhabihu ya kuteketezwa na dhabihu za ushirika.” Basi akaitoa dhabihu ya kuteketezwa.+ 10  Lakini mara tu alipomaliza kutoa dhabihu ya kuteketezwa, Samweli akafika. Kwa hiyo Sauli akaenda kumpokea na kumbariki. 11  Kisha Samweli akamuuliza: “Umefanya nini?” Sauli akamjibu: “Niliona kwamba watu wanatawanyika kutoka kwangu,+ nawe hukuja kwa wakati uliowekwa, na Wafilisti walikuwa wakikusanyika huko Mikmashi.+ 12  Kwa hiyo nikajiambia, ‘Sasa Wafilisti watashuka kunishambulia Gilgali, nami sijatafuta kibali cha* Yehova.’ Kwa hiyo nikahisi kwamba nina wajibu wa kutoa dhabihu ya kuteketezwa.” 13  Ndipo Samweli akamwambia Sauli: “Umetenda kipumbavu. Hukutii amri ambayo Yehova Mungu wako alikupa.+ Kama ungetii, Yehova angeimarisha ufalme wako juu ya Waisraeli milele. 14  Lakini sasa ufalme wako hautadumu.+ Yehova atamtafuta mtu anayeupendeza moyo wake,+ na Yehova atamweka kuwa kiongozi juu ya watu wake,+ kwa sababu hukutii mambo uliyoamriwa na Yehova.”+ 15  Kisha Samweli akainuka na kupanda kwenda zake kutoka Gilgali mpaka jiji la Gibea la Benjamini, naye Sauli akawahesabu watu; wale waliobaki naye walikuwa wanaume wapatao 600.+ 16  Sauli na Yonathani mwana wake pamoja na watu waliobaki pamoja nao walikuwa wakikaa katika jiji la Geba+ la Benjamini, nao Wafilisti walikuwa wamepiga kambi kule Mikmashi.+ 17  Na makundi ya wavamizi yalikuwa yakitoka katika kambi ya Wafilisti katika vikosi vitatu. Kikosi kimoja kilikuwa kikielekea kwenye barabara inayoenda Ofra, katika nchi ya Shuali; 18  kikosi kingine kilikuwa kikielekea kwenye barabara ya Beth-horoni;+ na kikosi cha tatu kilikuwa kikifuata barabara inayoelekea kwenye mpaka ulio ng’ambo ya bonde la Seboimu, kuelekea nyikani. 19  Basi hakukuwa na fundi yeyote wa chuma katika nchi yote ya Israeli, kwa sababu Wafilisti walikuwa wamesema: “Ili Waebrania wasitengeneze upanga wala mkuki.” 20  Na Waisraeli wote walilazimika kushuka kwenda kwa Wafilisti ili majembe yao ya plau, sururu, mashoka, au miundu yao inolewe. 21  Bei ya kunoa ilikuwa pimu moja* kwa majembe ya plau, kwa sururu, kwa vifaa vyenye meno matatu, kwa mashoka, na pia kwa ajili ya kurekebisha mchokoo wa ng’ombe. 22  Na siku ya vita, hakuna yeyote kati ya watu waliokuwa pamoja na Sauli na Yonathani aliyekuwa na upanga wala mkuki mkononi mwake;+ Sauli na Yonathani mwanawe ndio tu waliokuwa na silaha. 23  Basi kikosi cha wanajeshi* Wafilisti kilikuwa kimeenda kwenye kivuko kilicho kwenye njia inayoenda Mikmashi.+

Maelezo ya Chini

Hati ya Kiebrania haionyeshi idadi ya miaka yake.
Au “tarumbeta.”
Au “sijautuliza uso wa.”
Kipimo cha zamani ambacho ni karibu theluthi mbili za shekeli.
Tnn., “kituo cha ulinzi cha.”