Kitabu cha Kwanza cha Samweli 14:1-52

  • Yonathani aenda kupigana kule Mikmashi (1-14)

  • Mungu awashinda maadui wa Waisraeli (15-23)

  • Sauli afanya kiapo bila kufikiria (24-46)

    • Watu wala nyama pamoja na damu (32-34)

  • Vita vya Sauli; familia yake (47-52)

14  Siku moja Yonathani+ mwana wa Sauli alimwambia hivi mtumishi aliyembebea silaha: “Njoo tuvuke, twende kwenye kituo cha ulinzi cha Wafilisti upande wa pili.” Lakini hakumwambia baba yake jambo hilo.  Sauli alikuwa akikaa karibu na jiji la Gibea+ chini ya mkomamanga kule Migroni, na wanaume wapatao 600 walikuwa pamoja naye.+  (Na Ahiya mwana wa Ahitubu,+ ndugu ya Ikabodi,+ mwana wa Finehasi,+ mwana wa Eli,+ kuhani wa Yehova kule Shilo,+ alikuwa amebeba efodi.)+ Na watu hawakujua kwamba Yonathani alikuwa ameondoka.  Basi kati ya njia ambazo Yonathani alijaribu kutumia kuvuka ili afike kwenye kituo cha ulinzi cha Wafilisti, kulikuwa na mwamba ulio na umbo la jino upande huu na mwamba mwingine ulio na umbo la jino upande wa pili; mwamba mmoja uliitwa Bosesi, na mwamba wa pili uliitwa Sene.  Mwamba mmoja ulikuwa nguzo upande wa kaskazini ng’ambo ya Mikmashi, na wa pili ulikuwa upande wa kusini ng’ambo ya Geba.+  Basi Yonathani akamwambia mtumishi wake aliyembebea silaha: “Njoo tuvuke na kwenda kwenye kituo cha ulinzi cha wanaume hawa wasiotahiriwa.+ Labda Yehova atatusaidia, kwa maana hakuna kitu chochote kinachoweza kumzuia Yehova kuokoa kwa kutumia watu wengi au wachache.”+  Ndipo mtumishi wake aliyembebea silaha akamwambia: “Fanya jambo lolote ambalo moyo wako unakuchochea kufanya. Nenda popote unapotaka, nami nitakufuata popote ambapo moyo wako unakuchochea kwenda.”  Ndipo Yonathani akasema: “Tutavuka kwa wanaume wale ili watuone.  Wakituambia, ‘Simameni papo hapo mpaka tuje mlipo!’ basi tutasimama papo hapo, hatutapanda kwenda walipo. 10  Lakini wakisema, ‘Njooni hapa juu tupambane!’ tutapanda, kwa sababu Yehova atawatia mikononi mwetu. Hiyo ndiyo itakayokuwa ishara yetu.”+ 11  Basi wote wawili wakajitokeza mbele ya kituo cha ulinzi cha Wafilisti. Wafilisti wakasema: “Tazameni! Waebrania wanatoka katika mashimo walimokuwa wamejificha.”+ 12  Kwa hiyo wanaume waliokuwa kwenye kituo hicho cha ulinzi wakamwambia Yonathani na mtumishi wake aliyembebea silaha: “Njooni hapa juu tulipo, nasi tutawafunza somo!”+ Mara moja Yonathani akamwambia hivi mtumishi aliyembebea silaha: “Nifuate, kwa kuwa Yehova atawatia mikononi mwa Waisraeli.”+ 13  Basi Yonathani akapanda kwa mikono na miguu yake, na mtumishi wake aliyembebea silaha alikuwa nyuma yake; na Yonathani akaanza kuwashambulia na kuwaangusha Wafilisti, na mtumishi wake aliyembebea silaha alikuwa akiwaua nyuma ya Yonathani. 14  Katika shambulizi la kwanza la Yonathani na mtumishi aliyembebea silaha, waliwaua wanaume wapatao 20 katika shamba lenye ukubwa wa karibu nusu eka linaloweza kulimwa kwa plau.* 15  Ndipo hofu ikaenea katika kambi iliyo shambani na miongoni mwa watu wote waliokuwa katika kituo cha ulinzi, na hata makundi ya wavamizi+ yakashikwa na hofu. Dunia ikaanza kutetemeka, kukawa na hofu kubwa kutoka kwa Mungu. 16  Walinzi wa Sauli waliokuwa katika jiji la Gibea+ la Benjamini wakaona kwamba machafuko yalikuwa yakienea kila upande.+ 17  Sauli akawaambia watu waliokuwa pamoja naye: “Tafadhali, wahesabuni watu, mwone ni nani aliyetuacha.” Walipohesabu, wakagundua kwamba Yonathani na mtumishi wake aliyembebea silaha hawakuwepo. 18  Basi Sauli akamwambia Ahiya:+ “Lilete karibu Sanduku la Mungu wa kweli!” (Kwa maana wakati huo* Sanduku la Mungu wa kweli lilikuwa pamoja na Waisraeli.) 19  Sauli alipokuwa akiongea na kuhani, machafuko yaliyokuwa katika kambi ya Wafilisti yalizidi kuongezeka. Ndipo Sauli akamwambia hivi kuhani: “Acha unachofanya.”* 20  Kwa hiyo Sauli na watu wote waliokuwa pamoja naye wakakusanyika na kwenda vitani, na huko wakapata kwamba Wafilisti walikuwa wameshambuliana wenyewe kwa wenyewe kwa mapanga yao, na machafuko yalikuwa makubwa sana. 21  Pia, Waebrania ambao awali waliwaunga mkono Wafilisti na walioingia pamoja nao kambini walienda kujiunga na Waisraeli chini ya usimamizi wa Sauli na Yonathani. 22  Wanaume wote wa Israeli waliokuwa wamejificha+ katika eneo lenye milima la Efraimu wakasikia kwamba Wafilisti wamekimbia, nao pia wakaingia vitani na kuwafuatia. 23  Basi Yehova akawaokoa Waisraeli siku hiyo,+ na vita vikaenea mpaka Beth-aveni.+ 24  Lakini wanaume wa Israeli walikuwa chini ya mkazo mkali siku hiyo, kwa kuwa Sauli alikuwa amewaapisha hivi: “Alaaniwe mtu yeyote atakayekula chakula chochote* kabla ya jioni na kabla sijalipiza kisasi dhidi ya maadui wangu!” Kwa hiyo hakuna yeyote miongoni mwao aliyekula chakula chochote.+ 25  Basi watu wote wakafika* msituni, na kulikuwa na asali ardhini. 26  Watu walipoingia msituni, waliona asali ikidondoka, lakini hakuna yeyote aliyethubutu kunyoosha mkono wake ili kuila, kwa sababu waliogopa kile kiapo. 27  Lakini Yonathani hakumsikia baba yake akiwaapisha watu,+ kwa hiyo akanyoosha ncha ya fimbo iliyokuwa mkononi mwake na kuichovya ndani ya sega la asali. Alipourudisha mkono wake kinywani na kuila, macho yake yakang’aa. 28  Ndipo mtu mmoja akasema: “Baba yako aliwaapisha watu vikali akisema, ‘Na alaaniwe mtu atakayekula chakula leo!’+ Ndio sababu watu wamechoka sana.” 29  Hata hivyo, Yonathani akasema: “Baba yangu ameleta shida kubwa nchini. Angalieni jinsi macho yangu yalivyong’aa nilipoonja asali hii kidogo. 30  Hali ingekuwa bora zaidi ikiwa watu wangekula kwa uhuru+ leo baadhi ya nyara walizopata kutoka kwa maadui wao! Kwa maana Wafilisti wengi hata zaidi wangeuawa.” 31  Siku hiyo, waliendelea kuwaua Wafilisti kuanzia Mikmashi mpaka Aiyaloni,+ na watu wakachoka sana. 32  Basi watu wakaanza kukimbilia nyara kwa pupa, wakachukua kondoo na ng’ombe na ndama na kuwachinjia ardhini, nao wakala nyama pamoja na damu.+ 33  Basi Sauli akaambiwa hivi: “Tazama! Watu wanamtendea Yehova dhambi kwa kula nyama pamoja na damu.”+ Ndipo akasema: “Mmetenda kwa ukosefu wa imani. Bingirisheni jiwe kubwa juu yangu mara moja.” 34  Kisha Sauli akasema: “Nendeni kotekote miongoni mwa watu mkawaambie, ‘Ni lazima kila mmoja wenu aje na ng’ombe dume wake na kondoo wake mwachinjie hapa na kuwala. Msimtendee Yehova dhambi kwa kula nyama pamoja na damu.’”+ Basi kila mmoja wao akaja na ng’ombe dume wake usiku huo na kumchinjia mahali hapo. 35  Na Sauli akamjengea Yehova madhabahu.+ Hiyo ndiyo iliyokuwa madhabahu ya kwanza aliyomjengea Yehova. 36  Baadaye Sauli akasema: “Acheni tushuke tuwafuatie Wafilisti usiku na kuwapora mpaka asubuhi wakati wa mapambazuko. Hatutamwacha hai mtu yeyote.” Basi wakasema: “Fanya jambo lolote unaloona ni jema.” Kisha kuhani akasema: “Na tumkaribie Mungu wa kweli mahali hapa.”+ 37  Naye Sauli akamuuliza Mungu: “Je, nishuke nikawafuatie Wafilisti?+ Je, utawatia mikononi mwa Waisraeli?” Lakini Mungu hakumjibu siku hiyo. 38  Basi Sauli akasema: “Njooni hapa, enyi wakuu wote wa watu, mtafute ni dhambi gani iliyotendwa leo. 39  Kwa hakika kama anavyoishi Yehova, aliyewaokoa Waisraeli, hata kama ni mwanangu Yonathani, ni lazima afe.” Lakini hakuna mtu yeyote aliyemjibu. 40  Kisha akawaambia Waisraeli wote: “Mtakuwa upande mmoja, na mimi na mwanangu Yonathani tutakuwa upande wa pili.” Ndipo watu wakamwambia Sauli: “Fanya jambo lolote unaloona ni jema.” 41  Kisha Sauli akamwambia Yehova: “Ee Mungu wa Israeli, jibu kwa Thumimu!”+ Ndipo Yonathani na Sauli wakachaguliwa, nao watu wakawa huru. 42  Basi Sauli akasema: “Pigeni kura+ kuamua kati yangu na mwanangu Yonathani.” Kisha Yonathani akachaguliwa. 43  Halafu Sauli akamuuliza Yonathani: “Niambie, umefanya nini?” Yonathani akamwambia: “Nilionja tu asali kidogo kwa ncha ya fimbo iliyo mikononi mwangu.+ Nipo hapa! Niko tayari kufa!” 44  Basi Sauli akasema: “Mungu na akuadhibu, tena vikali, ikiwa hutakufa, Yonathani.”+ 45  Lakini watu wakamwambia Sauli: “Je, Yonathani afe, ambaye ameleta ushindi*+ huu mkubwa katika Israeli? Ni jambo lisiloweza kuwaziwa kamwe! Kwa hakika kama anavyoishi Yehova, hakuna unywele hata mmoja wa kichwa chake unaopaswa kuanguka ardhini, kwa maana alitenda pamoja na Mungu leo.”+ Hivyo watu wakamwokoa* Yonathani, naye hakufa. 46  Basi Sauli akaacha kuwafuatia Wafilisti, nao Wafilisti wakarudi katika eneo lao. 47  Sauli akauimarisha ufalme wake juu ya Waisraeli, akapigana na maadui wake wote waliomzunguka, alipigana na Wamoabu,+ Waamoni,+ Waedomu,+ wafalme wa Soba,+ na Wafilisti;+ na mahali popote alipoenda aliwashinda. 48  Alipigana kwa ushujaa na kuwashinda Waamaleki+ na kuwaokoa Waisraeli kutoka mikononi mwa waporaji. 49  Wana wa Sauli walikuwa Yonathani, Ishvi, na Malki-shua.+ Na alikuwa na mabinti wawili; mkubwa aliitwa Merabu,+ na mdogo aliitwa Mikali.+ 50  Mke wa Sauli aliitwa Ahinoamu binti ya Ahimaazi. Mkuu wa jeshi lake aliitwa Abneri+ mwana wa Neri, ndugu ya baba ya Sauli. 51  Kishi+ alikuwa baba ya Sauli, na Neri+ baba ya Abneri alikuwa mwana wa Abieli. 52  Kulikuwa na vita vikali dhidi ya Wafilisti siku zote za Sauli.+ Sauli alipomwona mwanamume yeyote mwenye nguvu au jasiri alimwandikisha katika utumishi wake.+

Maelezo ya Chini

Yaani, eneo linaloweza kulimwa kwa plau na ng’ombe dume wawili katika siku moja.
Tnn., “siku hiyo.”
Tnn., “Rudisha mkono wako.”
Tnn., “mkate wowote.”
Tnn., “nchi yote ikafika.”
Tnn., “wakamkomboa.”
Au “wokovu.”