Kitabu cha Kwanza cha Samweli 15:1-35

  • Sauli akosa kutii kwa kumwacha hai Agagi (1-9)

  • Samweli amkaripia Sauli (10-23)

    • “Kutii ni bora kuliko dhabihu” (22)

  • Sauli akataliwa asiendelee kuwa mfalme (24-29)

  • Samweli amuua Agagi (30-35)

15  Kisha Samweli akamwambia Sauli: “Yehova alinituma nikutie mafuta uwe mfalme juu ya watu wake Waisraeli,+ sasa sikiliza anavyosema Yehova.+  Yehova wa majeshi anasema hivi: ‘Nitawaadhibu Waamaleki kwa sababu waliwapinga Waisraeli walipokuwa njiani wakipanda kutoka Misri.+  Sasa, nenda uwashambulie Waamaleki+ na kuwaangamiza+ wao pamoja na vitu vyao vyote. Usiwaache hai;* unapaswa kuwaua,+ wanaume na wanawake, watoto wadogo na wale wanaonyonya, ng’ombe dume na kondoo, ngamia na pia punda.’”+  Sauli akawakusanya watu na kuwahesabu huko Telaimu: Kulikuwa na wanajeshi 200,000 wanaotembea kwa miguu na wanaume 10,000 wa Yuda.+  Sauli akaenda mpaka kwenye jiji la Amaleki, akavizia kando ya bonde.  Ndipo Sauli akawaambia hivi Wakeni:+ “Nendeni, ondokeni kati ya Waamaleki ili nisiwafagilie mbali pamoja nao.+ Kwa maana mliwatendea watu wote wa Israeli+ kwa upendo mshikamanifu walipotoka Misri.” Basi Wakeni wakaondoka kati ya Waamaleki.  Kisha Sauli akawaangamiza Waamaleki+ kuanzia Havila+ mpaka Shuri,+ jiji lililo karibu na Misri.  Akamkamata Agagi+ mfalme wa Amaleki akiwa hai, lakini watu wengine wote akawaangamiza kwa upanga.+  Hata hivyo, Sauli na watu wake walimwacha hai* Agagi na kondoo walio bora, ng’ombe, wanyama waliononeshwa, kondoo dume, na vitu vyote vizuri.+ Hawakutaka kuviangamiza. Lakini waliangamiza vitu vyote visivyo na thamani na visivyofaa. 10  Basi neno la Yehova likamjia Samweli: 11  “Ninasikitika* kwamba nimemweka Sauli kuwa mfalme, kwa sababu ameacha kunifuata naye hajatekeleza maneno yangu.”+ Samweli akakasirika sana, akaendelea kumlilia Yehova usiku kucha.+ 12  Samweli alipoamka asubuhi na mapema ili akutane na Sauli, aliambiwa hivi: “Sauli alienda Karmeli,+ na huko akajisimamishia mnara wa ukumbusho.+ Kisha akageuka na kushuka mpaka Gilgali.” 13  Mwishowe Samweli alipomfikia Sauli, Sauli akamwambia: “Yehova na akubariki. Nimetekeleza neno la Yehova.” 14  Lakini Samweli akamwambia: “Basi mbona nasikia milio ya kondoo na ng’ombe?”+ 15  Sauli akamjibu: “Waliletwa kutoka kwa Waamaleki, kwa sababu watu waliwaacha hai* kondoo bora na ng’ombe bora ili wawatoe dhabihu kwa Yehova Mungu wako; lakini vitu vilivyobaki tuliviangamiza.” 16  Ndipo Samweli akamwambia Sauli: “Nyamaza! Acha nikwambie jambo ambalo Yehova aliniambia jana usiku.”+ Basi akamwambia: “Sema!” 17  Samweli akamwambia: “Je, hukujiona kuwa mtu asiyefaa+ ulipowekwa kuwa kiongozi wa makabila ya Israeli na Yehova alipokutia mafuta kuwa mfalme wa Israeli?+ 18  Baadaye Yehova alikupa kazi na kukuambia, ‘Nenda, uwaangamize Waamaleki hao watenda dhambi.+ Pigana nao mpaka uwaangamize kabisa.’+ 19  Basi kwa nini hukuitii sauti ya Yehova? Badala yake, ulikimbilia nyara kwa pupa+ na kufanya maovu machoni pa Yehova!” 20  Hata hivyo, Sauli akamwambia Samweli: “Lakini nimeitii sauti ya Yehova! Nimefanya kazi ambayo Yehova alinituma nifanye, nikamleta Agagi mfalme wa Waamaleki na kuwaangamiza Waamaleki.+ 21  Lakini watu walichukua kondoo na ng’ombe kutoka kwenye nyara, vitu bora kati ya vitu vilivyopaswa kuangamizwa, ili wavitoe dhabihu kwa Yehova Mungu wako huko Gilgali.”+ 22  Ndipo Samweli akasema: “Je, Yehova hupendezwa zaidi na dhabihu za kuteketezwa na dhabihu nyinginezo+ kuliko kuitii sauti ya Yehova? Tazama! Kutii ni bora kuliko dhabihu,+ na kusikiliza kuliko mafuta+ ya kondoo dume; 23  kwa maana uasi+ ni sawa na dhambi ya uaguzi,*+ na kutenda kwa kimbelembele ni sawa na kutumia nguvu za uchawi na ibada ya sanamu.* Kwa kuwa umelikataa neno la Yehova,+ yeye pia amekukataa usiwe mfalme.”+ 24  Ndipo Sauli akamwambia Samweli: “Nimetenda dhambi, kwa kuwa nimeasi agizo la Yehova na maneno yako, kwa sababu niliwaogopa watu na kusikiliza maneno yao. 25  Sasa, tafadhali, nisamehe dhambi yangu, nawe urudi pamoja nami ili nimwinamie Yehova.”+ 26  Lakini Samweli akamwambia Sauli: “Sitarudi pamoja nawe, kwa kuwa umelikataa neno la Yehova, naye Yehova amekukataa usiendelee kuwa mfalme wa Israeli.”+ 27  Samweli alipokuwa akigeuka aende zake, Sauli akaushika upindo wa joho lake lisilo na mikono, lakini likararuka. 28  Ndipo Samweli akamwambia: “Yehova ameurarua ufalme wa Israeli kutoka kwako leo, naye atampa mwenzako aliye bora kuliko wewe.+ 29  Isitoshe, Mtukufu wa Israeli+ hatasema uwongo+ wala kubadili nia yake,* kwa maana Yeye si mwanadamu abadili nia yake.”*+ 30  Sauli akasema: “Nimetenda dhambi. Lakini tafadhali niheshimu mbele ya wazee wa watu wangu na mbele ya Waisraeli. Rudi pamoja nami, nami nitamwinamia Yehova Mungu wako.”+ 31  Basi Samweli akarudi pamoja na Sauli, na Sauli akamwinamia Yehova. 32  Kisha Samweli akasema: “Mleteni hapa Agagi mfalme wa Waamaleki.” Ndipo Agagi akaja kwake akisitasita,* kwa sababu Agagi alisema moyoni mwake: “Kwa hakika hatari ya kifo imepita.”* 33  Hata hivyo, Samweli akasema: “Kama upanga wako ulivyofanya wanawake wafiwe na watoto, ndivyo mama yako atakavyofiwa zaidi miongoni mwa wanawake.” Papo hapo Samweli akamkatakata Agagi vipandevipande mbele za Yehova huko Gilgali.+ 34  Kisha Samweli akaenda zake Rama, naye Sauli akapanda kwenda nyumbani kwake katika jiji la Gibea la Sauli. 35  Samweli hakumwona Sauli tena mpaka siku alipokufa, kwa maana Samweli alikuwa akimwombolezea Sauli.+ Yehova akaghairi kwamba alikuwa amemweka Sauli kuwa mfalme wa Israeli.+

Maelezo ya Chini

Au “Usiwahurumie.”
Au “walimhurumia.”
Au “Ninahuzunika.”
Au “waliwahurumia.”
Tnn., “sanamu za terafimu,” yaani, miungu ya familia; sanamu.
Au “ubashiri.”
Au “aghairi.”
Au “hataghairi.”
Au labda, “kwa ujasiri.”
Tnn., “uchungu wa kifo umepita.”