Kitabu cha Kwanza cha Samweli 16:1-23

  • Samweli amtia mafuta Daudi kuwa mfalme anayefuata (1-13)

    • “Yehova huona ndani ya moyo” (7)

  • Sauli anyang’anywa roho ya Mungu (14-17)

  • Daudi awa mpiga kinubi wa Sauli (18-23)

16  Mwishowe Yehova akamuuliza Samweli: “Kwa kuwa nimemkataa Sauli asitawale akiwa mfalme wa Israeli,+ utaendelea kumwombolezea mpaka lini?+ Jaza pembe yako mafuta,+ uende. Nitakutuma kwa Yese+ Mbethlehemu, kwa sababu nimejichagulia mfalme kutoka miongoni mwa wanawe.”+  Lakini Samweli akasema: “Nitaendaje? Sauli akisikia habari hii, ataniua.”+ Yehova akamwambia: “Nenda na ng’ombe mchanga, useme, ‘Nimekuja kumtolea Yehova dhabihu.’  Mwalike Yese kwenye dhabihu; kisha nitakujulisha utakalofanya. Utamtia mafuta kwa ajili yangu yule nitakayekuonyesha.”+  Samweli alifanya mambo aliyoambiwa na Yehova. Alipofika Bethlehemu,+ wazee wa jiji walitetemeka walipokutana naye, wakamuuliza: “Je, umekuja kwa amani?”  Akajibu: “Nimekuja kwa amani. Nimekuja kumtolea Yehova dhabihu. Jitakaseni, mje pamoja nami kwenye dhabihu.” Kisha akamtakasa Yese na wanawe, halafu akawaalika kwenye dhabihu.  Walipokuwa wakiingia, Samweli alimwona Eliabu+ na kusema: “Hakika mtiwa-mafuta wa Yehova amesimama hapa mbele zake.”  Lakini Yehova akamwambia Samweli: “Usitazame sura yake wala urefu wake,+ kwa maana nimemkataa. Kwa kuwa Mungu haoni kama mwanadamu anavyoona, kwa maana mwanadamu huona kinachoonekana kwa macho, lakini Yehova huona ndani ya moyo.”+  Kisha Yese akamwita Abinadabu,+ akampitisha mbele ya Samweli, lakini Samweli akasema: “Huyu pia Yehova hajamchagua.”  Kisha Yese akampitisha Shamma,+ lakini Samweli akasema: “Hata huyu Yehova hajamchagua.” 10  Basi Yese akawapitisha wanawe saba mbele ya Samweli, lakini Samweli akamwambia Yese: “Yehova hajamchagua yeyote kati ya hawa.” 11  Mwishowe Samweli akamuuliza Yese: “Je, hawa ndio wana wako wote?” Akajibu: “Aliye mdogo zaidi+ ameachwa mpaka sasa; anawalisha kondoo.”+ Kisha Samweli akamwambia Yese: “Mtume mtu akamwite, kwa sababu hatutaketi kula chakula mpaka atakapokuja hapa.” 12  Basi akamtuma mtu amwite, Yese akamleta ndani. Kijana huyo alikuwa mwekundu, mwenye macho yanayovutia, na mwenye sura nzuri.+ Ndipo Yehova akasema: “Simama, mtie mafuta, kwa maana huyu ndiye!”+ 13  Basi Samweli akachukua ile pembe ya mafuta+ na kumtia mafuta mbele ya ndugu zake. Na roho ya Yehova ikaanza kumtia nguvu Daudi kuanzia siku hiyo na kuendelea.+ Baadaye Samweli akainuka na kwenda zake Rama.+ 14  Sasa roho ya Yehova ilikuwa imemwacha Sauli,+ na roho mbaya kutoka kwa Yehova ilikuwa ikimtesa.+ 15  Watumishi wa Sauli wakamwambia: “Unaona kwamba roho mbaya kutoka kwa Mungu inakutesa. 16  Tafadhali, bwana wetu, waamuru watumishi wako walio mbele yako wamtafute mtu mwenye ustadi wa kupiga kinubi.+ Wakati wowote roho mbaya kutoka kwa Mungu inapokujia, atapiga kinubi, nawe utahisi vizuri.” 17  Basi Sauli akawaambia watumishi wake: “Tafadhali, nitafutieni mtu anayepiga kinubi vizuri, mumlete kwangu.” 18  Mtumishi mmoja akasema: “Tazama! Nimeona mwana fulani wa Yese Mbethlehemu anavyopiga kinubi kwa ustadi, ni mtu jasiri na shujaa hodari.+ Ana ustadi wa kuongea, ana sura nzuri,+ na Yehova yuko pamoja naye.”+ 19  Ndipo Sauli akawatuma wajumbe kwa Yese na kumwambia: “Mtume mwana wako Daudi aje kwangu, yule anayechunga kondoo.”+ 20  Basi Yese akapakia mikate, kiriba cha ngozi chenye divai, na mwanambuzi juu ya punda, akamtuma Daudi mwana wake kwa Sauli akiwa na vitu hivyo. 21  Kwa hiyo Daudi akafika kwa Sauli na kuanza kumtumikia.+ Sauli akampenda sana, naye Daudi akawa akimbebea silaha zake. 22  Sauli akamtumia Yese ujumbe huu: “Tafadhali, mruhusu Daudi aendelee kunitumikia, kwa sababu amepata kibali machoni pangu.” 23  Wakati wowote roho mbaya kutoka kwa Mungu ilipomjia Sauli, Daudi alichukua kinubi na kukipiga, kisha Sauli alipata kitulizo na kuhisi vizuri, na roho hiyo mbaya ilimwacha.+

Maelezo ya Chini