Kitabu cha Kwanza cha Samweli 17:1-58

  • Daudi amshinda Goliathi (1-58)

    • Goliathi awatukana Waisraeli (8-10)

    • Daudi akubali kupigana na Goliathi (32-37)

    • Daudi apigana kwa jina la Yehova (45-47)

17  Sasa Wafilisti+ wakakusanya majeshi yao* kwa ajili ya vita. Walikusanyika huko Soko,+ jiji la Yuda, wakapiga kambi kati ya Soko na Azeka,+ kule Efes-damimu.+  Sauli na wanaume wa Israeli wakakusanyika na kupiga kambi katika Bonde la* Ela,+ nao wakajipanga kivita ili kupigana na Wafilisti.  Wafilisti walikuwa upande mmoja wa mlima, na Waisraeli walikuwa upande ule mwingine, na bonde lilikuwa katikati yao.  Kisha shujaa mmoja akatoka katika kambi za Wafilisti; aliitwa Goliathi,+ kutoka Gathi,+ alikuwa na urefu wa mikono sita na shubiri moja.*  Alikuwa na kofia ya shaba kichwani, naye alivaa koti la vita lenye magamba yanayolaliana. Koti hilo la vita la shaba+ lilikuwa na uzito wa shekeli 5,000.*  Alikuwa na mabamba ya shaba yaliyokinga miguu yake na fumo+ la shaba lililoning’inia katikati ya mabega yake.  Mpini wa mbao wa mkuki wake ulikuwa kama mti wa wafumaji wa nguo,+ na kichwa cha chuma cha mkuki wake kilikuwa na uzito wa shekeli 600;* na mtu aliyembebea ngao alitembea mbele yake.  Basi akasimama na kuviita vikosi vya Israeli+ akisema: “Kwa nini mmekuja kujipanga kivita? Je, mimi si Mfilisti nanyi je, si watumishi wa Sauli? Jichagulieni mwanamume, aje kupigana nami.  Akiweza kupigana nami na kuniua, tutakuwa watumishi wenu. Lakini nikimshinda na kumuua, mtakuwa watumishi wetu, nanyi mtatutumikia.” 10  Kisha Mfilisti huyo akasema: “Ninavitukana* vikosi vya Israeli+ leo. Nipeni mwanamume, nipigane naye!” 11  Sauli na Waisraeli wote waliposikia maneno hayo ya Mfilisti huyo, wakashikwa na hofu na kuogopa sana. 12  Basi Daudi alikuwa mwana wa Yese,+ Mwefrathi+ kutoka mji wa Bethlehemu+ wa Yuda, ambaye alikuwa na wana wanane+ na ambaye katika siku za Sauli alikuwa tayari amezeeka. 13  Wana watatu wakubwa wa Yese walikuwa wameenda na Sauli vitani.+ Majina ya wana hao watatu walioenda vitani ni Eliabu+ mzaliwa wake wa kwanza, Abinadabu+ mwana wake wa pili, na Shamma mwana wake wa tatu.+ 14  Daudi ndiye aliyekuwa mdogo zaidi,+ na wale watatu wakubwa walikuwa wameenda pamoja na Sauli. 15  Daudi alikuwa akienda na kurudi kutoka kwa Sauli ili kuchunga kondoo+ wa baba yake huko Bethlehemu. 16  Wakati huo, yule Mfilisti alikuwa akija na kuwadhihaki kila asubuhi na kila jioni kwa siku 40. 17  Ndipo Yese akamwambia Daudi mwana wake: “Tafadhali, chukua hii efa* ya nafaka iliyokaangwa na mikate hii kumi, uwapelekee haraka ndugu zako kambini. 18  Nawe umpelekee mkuu wa elfu mafungu haya kumi ya jibini;* pia, angalia ndugu zako wanaendeleaje na uniletee kitu fulani kutoka kwao.” 19  Walikuwa pamoja na Sauli na wanaume wengine wote wa Israeli katika Bonde la* Ela,+ wakipigana na Wafilisti.+ 20  Kwa hiyo Daudi akaamka asubuhi na mapema na kuwaacha kondoo mikononi mwa mtu mwingine; kisha akapakia vitu hivyo na kwenda kama Yese alivyokuwa amemwamuru. Alipofika kambini, jeshi lilikuwa likienda kwenye uwanja wa vita huku likipiga kelele za vita. 21  Waisraeli na Wafilisti wakajipanga kivita wakikabiliana uso kwa uso. 22  Mara moja Daudi akaiacha mizigo yake mikononi mwa mtu aliyetunza mizigo, akakimbia kwenda kwenye uwanja wa vita. Alipofika, akaanza kuulizia habari za ndugu zake.+ 23  Alipokuwa akizungumza nao, akaja yule Mfilisti shujaa aliyeitwa Goliathi,+ kutoka Gathi. Alitoka katika vikosi vya Wafilisti, akasema maneno yaleyale aliyozoea kusema,+ na Daudi akamsikia. 24  Wanaume wote wa Israeli walipomwona mwanamume huyo, wakaogopa sana na kumkimbia.+ 25  Wanaume wa Israeli walikuwa wakisema: “Je, mnamwona mwanamume yule anayekuja? Anakuja kuwatukana* Waisraeli.+ Mfalme atampa utajiri mwingi mtu atakayemuua mwanamume huyo, atampa pia binti yake mwenyewe,+ naye ataiondolea wajibu nyumba ya baba yake katika Israeli.” 26  Daudi akaanza kuwauliza wanaume waliokuwa wamesimama karibu naye: “Mtu atakayemuua yule Mfilisti na kuwaondolea Waisraeli aibu atafanyiwa nini? Kwani huyu Mfilisti asiyetahiriwa ni nani hata avitukane* vikosi vya Mungu aliye hai?”+ 27  Basi watu hao wakamwambia maneno yaleyale yaliyokuwa yamesemwa: “Hivi ndivyo atakavyofanyiwa mwanamume atakayemuua.” 28  Eliabu ndugu yake mkubwa+ alipomsikia Daudi akizungumza na wanaume hao, akamkasirikia Daudi na kumwambia: “Kwa nini umeshuka huku? Na wale kondoo wachache nyikani umemwachia nani?+ Najua vizuri kimbelembele chako na nia mbaya ya moyo wako; umeshuka tu ili kutazama vita.” 29  Daudi akamwambia: “Sasa nimefanya nini? Nilikuwa nikiuliza swali tu!” 30  Ndipo Daudi akamwacha, akamgeukia mtu mwingine na kumuuliza swali lilelile,+ na watu wakamjibu vilevile kama mwanzoni.+ 31  Watu wakasikia maneno aliyosema Daudi, wakamwambia Sauli. Basi Sauli akaagiza aitwe. 32  Daudi akamwambia Sauli: “Mtu yeyote asife moyo* kwa sababu yake. Mimi mtumishi wako nitaenda kupigana na huyo Mfilisti.”+ 33  Lakini Sauli akamwambia Daudi: “Huwezi kwenda kupigana na huyo Mfilisti, kwa sababu wewe ni mvulana tu,+ naye amekuwa mwanajeshi* tangu alipokuwa kijana.” 34  Ndipo Daudi akamwambia Sauli: “Mimi mtumishi wako nimekuwa nikichunga kondoo wa baba yangu, na simba+ akaja, na pia dubu, na kila mmoja wao akamchukua kondoo kutoka kundini. 35  Nilimfuata, nikamuua na kumwokoa kondoo kutoka kinywani mwake. Aliporuka ili kunishambulia, nilimkamata manyoya yake,* nikampiga, na kumuua. 36  Mimi mtumishi wako nilimuua simba na dubu pia, na huyu Mfilisti asiyetahiriwa atakuwa kama mmoja wao, kwa sababu amevitukana* vikosi vya Mungu aliye hai.”+ 37  Kisha Daudi akasema: “Yehova, aliyeniokoa kutoka katika makucha ya simba na ya dubu, ndiye atakayeniokoa kutoka mikononi mwa Mfilisti huyo.”+ Ndipo Sauli akamwambia Daudi: “Nenda, na Yehova awe pamoja nawe.” 38  Basi Sauli akamvisha Daudi mavazi yake. Akamvisha kofia ya shaba kichwani, halafu akamvisha koti la vita. 39  Kisha Daudi akajifunga upanga wake juu ya mavazi yake, akajaribu kutembea lakini akashindwa kwa sababu hakuwa ameyazoea. Basi Daudi akamwambia Sauli: “Siwezi kwenda nikiwa nimevaa vitu hivi, kwa maana sijavizoea.” Kwa hiyo Daudi akavivua. 40  Kisha akachukua fimbo yake mkononi, akajichagulia mawe matano laini kutoka katika bonde la kijito, akayaweka kwenye kifuko ndani ya mfuko wake wa mchungaji, na kombeo+ lilikuwa mkononi mwake. Naye akaanza kumkaribia huyo Mfilisti. 41  Mfilisti huyo akaanza kumkaribia Daudi zaidi na zaidi, na mtu aliyembebea ngao alikuwa mbele yake. 42  Mfilisti huyo alipotazama na kumwona Daudi, akaanza kumdhihaki kwa dharau kwa sababu alikuwa tu mvulana mwekundu mwenye sura nzuri.+ 43  Basi Mfilisti huyo akamuuliza Daudi: “Je, mimi ni mbwa+ hivi kwamba unijie na vijiti?” Ndipo huyo Mfilisti akamlaani Daudi kwa miungu yake. 44  Akamwambia Daudi: “Nikaribie tu, nyama yako nitawapa ndege wa angani na wanyama wa mwituni.” 45  Daudi akamjibu hivi huyo Mfilisti: “Unakuja kupigana nami kwa upanga, mkuki, na fumo,+ lakini mimi naja kupigana nawe kwa jina la Yehova wa majeshi,+ Mungu wa vikosi vya Israeli, ambaye umemtukana.*+ 46  Siku hii ya leo Yehova atakutia wewe mikononi mwangu,+ nami nitakuua na kukata kichwa chako; na siku ya leo nitawapa ndege wa angani na wanyama mwitu wa dunia maiti za kambi ya Wafilisti; na watu wote duniani watajua kwamba kuna Mungu katika Israeli.+ 47  Na watu wote waliokusanyika hapa watajua* kwamba Yehova haokoi kwa upanga wala kwa mkuki,+ kwa sababu vita ni vya Yehova,+ naye atawatia ninyi nyote mikononi mwetu.”+ 48  Basi Mfilisti huyo akasimama, akazidi kukaribia ili akutane na Daudi, lakini Daudi akakimbia haraka kuelekea kwenye uwanja wa vita kukutana na Mfilisti huyo. 49  Daudi akautia mkono wake ndani ya mfuko wake, akachukua jiwe kutoka humo, na kulirusha kwa kombeo. Akampiga Mfilisti huyo kwenye paji la uso, na jiwe hilo likapenya katika paji la uso wake, akaanguka chini kifudifudi.+ 50  Basi Daudi akamshinda Mfilisti huyo kwa kombeo na jiwe; alimpiga Mfilisti huyo na kumuua, ingawa Daudi hakuwa na upanga mkononi mwake.+ 51  Daudi akaendelea kukimbia na kusimama juu yake. Kisha akaushika upanga wa Mfilisti+ huyo na kuuchomoa kutoka katika ala yake, akahakikisha kwamba amekufa kwa kumkata kichwa kwa upanga huo. Wafilisti walipoona kwamba shujaa wao amekufa, wakakimbia.+ 52  Kisha wanaume wa Israeli na Yuda wakainuka na kuanza kupiga kelele na kuwafuatia Wafilisti kuanzia bondeni+ mpaka kwenye malango ya Ekroni,+ na maiti za Wafilisti waliouawa zilienea barabarani kuanzia Shaaraimu,+ mpaka Gathi na Ekroni. 53  Waisraeli waliporudi baada ya kuwafuatia vikali Wafilisti, walipora kambi zao. 54  Halafu Daudi akachukua kichwa cha yule Mfilisti na kukileta Yerusalemu, lakini akaziweka silaha za Mfilisti huyo ndani ya hema lake mwenyewe.+ 55  Sauli alipomwona Daudi akienda kupigana na Mfilisti huyo, alimuuliza hivi Abneri+ mkuu wa jeshi: “Abneri, mvulana huyu ni mwana wa nani?”+ Abneri akajibu: “Kwa hakika kama unavyoishi,* Ee mfalme, mimi sijui!” 56  Mfalme akasema: “Tafuta mvulana huyu ni mwana wa nani.” 57  Basi mara tu Daudi aliporudi baada ya kumuua huyo Mfilisti, Abneri akamchukua na kumpeleka mbele ya Sauli akiwa na kichwa cha huyo Mfilisti+ mkononi mwake. 58  Ndipo Sauli akamuuliza: “Mvulana, wewe ni mwana wa nani?” Daudi akamjibu: “Mimi ni mwana wa mtumishi wako Yese+ Mbethlehemu.”+

Maelezo ya Chini

Tnn., “kambi zao.”
Tnn., “Nchi Tambarare ya Chini ya.”
Alikuwa na urefu wa mita 2.9 hivi (futi 9 na inchi 5.75). Angalia Nyongeza B14.
Karibu kilogramu 57. Angalia Nyongeza B14.
Karibu kilogramu 6.84. Angalia Nyongeza B14.
Au “Nataka kushindana na.”
Efa ilikuwa sawa na lita 22 au kilogramu 13 hivi. Angalia Nyongeza B14.
Tnn., “maziwa.”
Au “Nchi Tambarare ya Chini ya.”
Au “kushindana na.”
Au “ashindane na.”
Au “asiogope.”
Au “mwanamume wa vita.”
Au “utaya wake.” Tnn., “ndevu zake.”
Au “ameshindana na.”
Au “umeshindana naye.”
Tnn., “Na kutaniko hili lote litajua.”
Au “Kama nafsi yako inavyoishi.”