Kitabu cha Kwanza cha Samweli 18:1-30

  • Urafiki wa Daudi na Yonathani (1-4)

  • Sauli ashikwa na wivu kwa sababu ya ushindi wa Daudi (5-9)

  • Sauli ajaribu kumuua Daudi (10-19)

  • Daudi amwoa Mikali binti ya Sauli (20-30)

18  Baada tu ya Daudi kumaliza kuzungumza na Sauli, Yonathani+ na Daudi wakashikamana na kuwa marafiki wa karibu sana,* na Yonathani akaanza kumpenda kama alivyojipenda mwenyewe.*+  Kuanzia siku hiyo, Sauli akamchukua Daudi, naye hakumruhusu arudi nyumbani kwa baba yake.+  Na Yonathani na Daudi wakafanya agano,+ kwa sababu alimpenda kama alivyojipenda mwenyewe.*+  Yonathani akavua joho lake lisilo na mikono na kumpa Daudi, pamoja na silaha zake, upanga wake, upinde wake, na mshipi wake.  Daudi akaanza kwenda vitani, naye alifanikiwa*+ popote alipotumwa na Sauli. Basi Sauli akamweka asimamie wanajeshi vitani,+ na jambo hilo likawafurahisha watu wote na pia watumishi wa Sauli.  Daudi na watu wengine walipokuwa wakirudi baada ya kuwaua Wafilisti, wanawake walikuwa wakitoka katika majiji yote ya Israeli wakiimba+ na kucheza dansi ili kumpokea Mfalme Sauli kwa matari,+ kwa vigelegele, na udi.  Wanawake hao waliokuwa wakisherehekea walikuwa wakiimba hivi: “Sauli ameua maelfu yake,Na Daudi makumi yake ya maelfu.”+  Sauli akakasirika sana,+ na wimbo huo haukumpendeza kwa kuwa alisema: “Wamempa Daudi makumi ya maelfu, lakini mimi wamenipa maelfu. Lililobaki tu ni kumpa ufalme!”+  Kuanzia siku hiyo na kuendelea, Sauli alikuwa akimtilia shaka Daudi. 10  Siku iliyofuata, roho mbaya kutoka kwa Mungu ikamvamia Sauli,+ naye akaanza kutenda kwa njia ya ajabu* nyumbani, huku Daudi akipiga muziki kwa kinubi+ kama alivyofanya nyakati nyingine. Sauli alikuwa na mkuki mkononi,+ 11  basi akaurusha mkuki huo+ akisema hivi moyoni: ‘Nitampigilia Daudi ukutani!’ Lakini Daudi alimkwepa mara mbili. 12  Ndipo Sauli akamwogopa Daudi kwa sababu Yehova alikuwa pamoja naye+ lakini alikuwa amemwacha yeye.*+ 13  Kwa hiyo Sauli akamwondoa nyumbani mwake na kumweka kuwa mkuu wa elfu, basi Daudi alikuwa akiliongoza jeshi vitani.*+ 14  Daudi akaendelea kufanikiwa*+ katika mambo yote aliyofanya, na Yehova alikuwa pamoja naye.+ 15  Sauli alipoona kwamba Daudi anafanikiwa sana, akaanza kumwogopa. 16  Lakini watu wote wa Israeli na Yuda walimpenda Daudi, kwa sababu alikuwa akiwaongoza vitani. 17  Baadaye Sauli akamwambia Daudi: “Ndiye huyu Merabu binti yangu mkubwa.+ Nitakupa awe mke wako.+ Lakini unapaswa kuendelea kunitumikia kwa ujasiri na kupigana vita vya Yehova.”+ Kwa maana Sauli alisema hivi moyoni: ‘Mkono wangu usimuue. Acha mikono ya Wafilisti imuue.’+ 18  Ndipo Daudi akamwambia Sauli: “Mimi ni nani na watu wangu wa ukoo ni nani, au familia ya baba yangu katika Israeli, hata mfalme awe baba mkwe wangu?”+ 19  Hata hivyo, wakati ulipofika wa kumpa Daudi Merabu, binti ya Sauli, tayari Adrieli+ Mmeholathi alikuwa amepewa binti huyo awe mke wake. 20  Sasa Mikali+ binti ya Sauli alimpenda Daudi, Sauli akajulishwa jambo hilo, nalo likampendeza. 21  Kwa hiyo Sauli akasema: “Nitampa Daudi binti huyo ili awe mtego kwake, na ili mikono ya Wafilisti imuue.”+ Kisha Sauli akamwambia hivi Daudi mara ya pili: “Utafanya mapatano ya ndoa pamoja nami* leo.” 22  Pia, Sauli akawaamuru hivi watumishi wake: “Zungumzeni na Daudi kwa siri na kumwambia, ‘Tazama! Mfalme anakupenda, na watumishi wake wote wanakupenda sana. Basi sasa fanya mapatano ya ndoa na mfalme.’” 23  Watumishi wa Sauli walipomwambia Daudi mambo hayo, Daudi akasema: “Je, mnafikiri ni jambo rahisi kwa mtu maskini na asiyeheshimiwa sana kama mimi kufanya mapatano ya ndoa na mfalme?”+ 24  Kisha watumishi wa Sauli wakamletea habari hii: “Haya ndiyo maneno aliyosema Daudi.” 25  Kwa hiyo Sauli akasema: “Hivi ndivyo mnavyopaswa kumwambia Daudi: ‘Mfalme hataki mahari yoyote+ isipokuwa magovi 100 ya Wafilisti,+ ili mfalme awalipize kisasi maadui wake.’” Lakini Sauli alikuwa anapanga njama ili Wafilisti wamuue Daudi. 26  Basi watumishi wake wakamwambia Daudi habari hiyo, na habari hiyo ya kufanya mapatano ya ndoa na mfalme ikampendeza Daudi.+ Kabla ya siku iliyopangwa kufika, 27  Daudi alienda na wanaume wake na kuwaua wanaume 200 Wafilisti, na Daudi akamletea mfalme idadi kamili ya magovi yao, ili afanye mapatano ya ndoa na mfalme. Basi Sauli akampa Daudi Mikali binti yake awe mke wake.+ 28  Sauli akatambua kwamba Yehova alikuwa pamoja na Daudi+ na Mikali binti yake alimpenda Daudi.+ 29  Jambo hilo likamfanya Sauli azidi kumwogopa Daudi, basi Sauli akawa adui ya Daudi maisha yake yote.+ 30  Watawala wa Wafilisti walikuwa wakienda vitani, lakini kadiri walivyoenda, ndivyo Daudi alivyozidi kufanikiwa* kuliko watumishi wote wa Sauli;+ na jina lake liliheshimiwa sana.+

Maelezo ya Chini

Au “kama nafsi yake mwenyewe.”
Au “nafsi ya Yonathani ikashikamana na nafsi ya Daudi.”
Au “kama nafsi yake mwenyewe.”
Au “alitenda kwa hekima.”
Au “kutenda kama nabii.”
Yaani, Sauli.
Tnn., “akitoka nje na kuingia mbele ya watu.”
Au “kutenda kwa hekima.”
Au “Nitakuwa baba mkwe wako.”
Au “alivyozidi kutenda kwa hekima.”