Kitabu cha Kwanza cha Samweli 2:1-36

  • Sala ya Hana (1-11)

  • Dhambi za wana wawili wa Eli (12-26)

  • Yehova aihukumu nyumba ya Eli (27-36)

2  Kisha Hana akasema hivi katika sala: “Moyo wangu unashangilia katika Yehova;+Pembe yangu imekwezwa* na Yehova. Kinywa changu kimefunguliwa wazi dhidi ya maadui wangu,Kwa maana ninashangilia kwa sababu ya matendo yako ya wokovu.   Hakuna aliye mtakatifu kama Yehova,Hakuna mwingine isipokuwa wewe,+Na hakuna mwamba kama Mungu wetu.+   Msiendelee kuzungumza kwa kiburi;Neno lolote la majivuno lisitoke vinywani mwenu,Kwa maana Yehova ni Mungu wa ujuzi,+Naye hupima matendo kwa njia ya haki.   Pinde za mashujaa huvunjwavunjwa,Lakini wale wanaojikwaa hutiwa nguvu.+   Walioshiba lazima waajiriwe ili wapate mkate,Lakini wenye njaa hawana njaa tena.+ Aliye tasa amezaa watoto saba,+Lakini mwanamke aliyekuwa na wana wengi ameachwa mpweke.*   Yehova huua, naye huhifadhi uhai;*Hushusha Kaburini,* naye hufufua.+   Yehova humfanya mtu awe maskini, naye hutajirisha;+Hushusha, naye hukweza.+   Humwinua mtu wa hali ya chini kutoka mavumbini;Humwinua maskini kutoka katika rundo la majivu,*+Ili awafanye wakae pamoja na wakuu,Na kuwapa kiti cha heshima. Nguzo za dunia ni za Yehova,+Naye huweka nchi inayozaa juu yake.   Hulinda hatua za washikamanifu wake;+Lakini waovu watanyamazishwa gizani,+Kwa maana mwanadamu hashindi kwa nguvu.+ 10  Yehova atawavunjavunja wale wanaopigana naye;*+Atanguruma dhidi yao kutoka mbinguni.+ Yehova atahukumu mpaka miisho ya dunia,+Atampa nguvu mfalme wake,+Na kuikweza pembe ya* mtiwa-mafuta wake.”+ 11  Basi Elkana akaenda nyumbani kwake Rama, lakini yule mvulana akawa mhudumu wa* Yehova+ chini ya uangalizi wa kuhani Eli. 12  Sasa wana wa Eli walikuwa watu waovu;+ hawakumheshimu Yehova. 13  Hivi ndivyo walivyofanya kuhusu vitu vilivyoletwa na watu ambavyo vilikuwa haki ya makuhani:+ Kila mara mtu yeyote alipokuwa akitoa dhabihu, mtumishi wa kuhani alikuja na uma wenye meno matatu mkononi mwake nyama ilipokuwa ikichemka, 14  naye aliutia kwa nguvu ndani ya beseni, chungu cha kupikia chenye mikono miwili, sufuria kubwa, au chungu cha kupikia chenye mkono mmoja. Nyama yoyote iliyoinuliwa na uma huo, ilichukuliwa na kuhani. Hivyo ndivyo walivyokuwa wakiwatendea Waisraeli wote waliokuja Shilo. 15  Pia, hata kabla ya mtu anayetoa dhabihu kuyafanya mafuta yafuke moshi,+ mtumishi wa kuhani alikuwa akija na kumwambia, “Mpe kuhani nyama akachome. Hatachukua nyama iliyochemshwa kutoka kwako, atachukua nyama mbichi tu.” 16  Mtu huyo alipomwambia, “Acha kwanza wahakikishe kwamba mafuta yamefuka moshi,+ kisha ujichukulie chochote upendacho,”* alisema: “Hapana, nipe sasa hivi; la sivyo, nitaichukua kwa nguvu!” 17  Kwa hiyo dhambi ya watumishi hao ikawa kubwa sana mbele za Yehova,+ kwa maana watu hao hawakuheshimu dhabihu ya Yehova. 18  Basi Samweli alikuwa akihudumu+ mbele za Yehova, akiwa amevaa* efodi ya kitani,+ ingawa alikuwa mvulana tu. 19  Pia, mama yake alikuwa akimshonea joho dogo lisilo na mikono na kumletea mwaka baada ya mwaka alipokuja na mume wake kutoa dhabihu ya kila mwaka.+ 20  Eli akambariki Elkana na mke wake akisema, “Yehova na akupe mtoto kutoka kwa mke huyu ili achukue nafasi ya yule aliyekabidhiwa kwa Yehova.”+ Kisha wakarudi nyumbani. 21  Yehova akamkazia uangalifu Hana, ili aweze kupata mimba;+ basi akazaa wana watatu zaidi na mabinti wawili. Naye mvulana Samweli akaendelea kukua mbele za Yehova.+ 22  Sasa Eli alikuwa amezeeka sana, lakini alikuwa amesikia mambo yote ambayo wanawe walikuwa wakiwatendea+ Waisraeli wote na jinsi walivyokuwa wakilala na wanawake waliotumikia kwenye mlango wa hema la mkutano.+ 23  Alikuwa akiwaambia hivi: “Kwa nini mnaendelea kufanya mambo ya aina hii? Kwa maana mambo ninayosikia kuwahusu kutoka kwa watu wote ni mabaya. 24  Msifanye hivyo wanangu, kwa sababu habari ninazosikia zikienea miongoni mwa watu wa Yehova si nzuri. 25  Mwanadamu akimtendea dhambi mwanadamu mwenzake, mtu fulani anaweza kumsihi Yehova kwa niaba yake;* lakini mwanadamu akimtendea dhambi Yehova,+ ni nani anayeweza kusali kwa ajili yake?” Lakini walikataa kumsikiliza baba yao, kwa sababu Yehova alikuwa ameazimia kuwaua.+ 26  Lakini mvulana Samweli aliendelea kukua na kupendwa na Yehova na pia wanadamu.+ 27  Mtu wa Mungu alimjia Eli na kumwambia, “Yehova anasema hivi: ‘Je, sikujitambulisha waziwazi kwa watu wa nyumba ya baba yako walipokuwa Misri wakiwa watumwa wa nyumba ya Farao?+ 28  Naye alichaguliwa kutoka katika makabila yote ya Israeli+ ili anitumikie akiwa kuhani wangu na kupanda juu ya madhabahu yangu+ kutoa dhabihu, kufukiza uvumba,* na kuvaa efodi mbele zangu; nami niliwapa watu wa nyumba ya babu yako dhabihu zote zinazochomwa kwa moto zilizotolewa na Waisraeli.*+ 29  Kwa nini ninyi wanaume mnadharau* dhabihu yangu na toleo langu ambalo nimeamuru katika makao yangu?+ Kwa nini unaendelea kuwaheshimu wana wako kuliko mimi kwa kujinenepesha kwa sehemu bora za kila dhabihu inayotolewa na watu wangu Waisraeli?+ 30  “‘Ndiyo sababu Yehova Mungu wa Israeli anasema hivi: “Hakika nilisema kwamba nyumba yako na nyumba ya babu yako itatembea mbele zangu daima.”+ Lakini sasa Yehova anatangaza hivi: “Ni jambo nisiloweza kamwe kuwazia, kwa sababu wale wanaoniheshimu nitawaheshimu,+ lakini wale wanaonidharau watadharauliwa.” 31  Tazama! Siku zinakuja nitakapokata nguvu zako na za* nyumba ya baba yako, hivi kwamba hakuna mwanamume yeyote wa nyumba yako atakayeishi na kuzeeka.+ 32  Nawe utamwona adui katika makao yangu miongoni mwa mambo yote mema wanayofanyiwa Waisraeli,+ na kamwe hakutakuwa tena na mzee katika nyumba yako. 33  Mwanamume wako ambaye nitamwacha aendelee kutumikia kwenye madhabahu yangu atayadhoofisha macho yako na kukuletea huzuni, lakini idadi kubwa ya watu wa nyumba yako itauawa kwa upanga.+ 34  Na mambo yatakayowapata wana wako wawili, Hofni na Finehasi, yatakuwa ishara kwako: Wote wawili watakufa siku ileile.+ 35  Kisha nitajiinulia kuhani mwaminifu.+ Atatenda kulingana na mapenzi ya moyo wangu;* nami nitamjengea nyumba ya kudumu, naye atatembea mbele ya mtiwa-mafuta wangu daima. 36  Mtu yeyote atakayebaki katika nyumba yako atakuja na kumwinamia ili alipwe pesa na kupata mkate, naye atasema: “Tafadhali, niweke katika nafasi yoyote ya ukuhani ili nile kipande cha mkate.”’”+

Maelezo ya Chini

Au “Nguvu zangu zimekwezwa.” Angalia Kamusi.
Tnn., “amedhoofika.”
Au “huhuisha.”
Au “Sheoli.” Angalia Kamusi.
Au labda, “jaa la takataka; jalalani.”
Au labda, “Wale wanaoshindana na Yehova wataogopeshwa.”
Au “nguvu za.” Angalia Kamusi.
Au “alikuwa akimtumikia.”
Au “ambacho nafsi yako inatamani.”
Tnn., “amefungwa.”
Au labda, “Mungu atakuwa mpatanishi wake.”
Tnn., “wana wa Israeli.”
Au labda, “kufanya moshi wa dhabihu upae juu.”
Tnn., “mnapiga teke.”
Tnn., “mkono wenu na wa.”
Au “kilicho katika moyo wangu na nafsi yangu.”