Kitabu cha Kwanza cha Samweli 20:1-42

  • Yonathani awa mshikamanifu kwa Daudi (1-42)

20  Kisha Daudi akakimbia kutoka Naiothi huko Rama. Hata hivyo, akaenda kwa Yonathani na kumuuliza: “Nimefanya nini?+ Nimefanya kosa gani, nami nimemtendea baba yako dhambi gani hivi kwamba anataka kuniua?”  Yonathani akamwambia: “Ni jambo lisiloweza kuwaziwa kamwe!+ Hutakufa. Baba yangu hawezi kufanya jambo lolote, liwe kubwa au dogo, bila kuniambia. Kwa nini baba yangu anifiche jambo hilo? Hawezi kufanya hivyo.”  Lakini Daudi akaapa hivi tena: “Bila shaka baba yako anajua kwamba unanipenda+ na hivyo atasema, ‘Msimwambie Yonathani jambo hili asije akahuzunika.’ Lakini kwa hakika kama Yehova anavyoishi na kwa hakika kama unavyoishi,* kuna hatua moja tu kati yangu na kifo!”+  Ndipo Yonathani akamwambia Daudi: “Nitakufanyia lolote unalosema.”  Daudi akamwambia Yonathani: “Kesho ni mwezi mpya,+ na hakika ninatazamiwa kuketi pamoja na mfalme ili kula naye; niache niende, nitajificha shambani mpaka siku ya tatu jioni.  Ikiwa baba yako atanikosa, mwambie, ‘Daudi alinisihi nimruhusu aende mara moja katika jiji lake la Bethlehemu,+ kwa sababu kuna dhabihu ya kila mwaka huko kwa ajili ya familia yote.’+  Akisema, ‘Ni vema!’ mimi mtumishi wako nitakuwa na amani. Lakini akikasirika, uwe na hakika kwamba ameazimia kunidhuru.  Nitendee mimi mtumishi wako kwa upendo mshikamanifu,+ kwa kuwa umeniingiza mimi mtumishi wako katika agano ulilofanya na Yehova.+ Lakini ikiwa nina hatia,+ niue wewe mwenyewe. Kwa nini unitie mikononi mwa baba yako?”  Kwa hiyo Yonathani akasema: “Ni jambo nisiloweza kamwe kuwazia kwamba nipendekeze utendewe hivyo! Nikipata habari kwamba baba yangu ameazimia kukudhuru, kwa nini nisikwambie?”+ 10  Kisha Daudi akamuuliza Yonathani: “Ni nani atakayeniambia baba yako akikujibu kwa ukali?” 11  Yonathani akamwambia Daudi: “Njoo, twende shambani.” Basi wote wawili wakaenda shambani. 12  Yonathani akamwambia Daudi: “Yehova Mungu wa Israeli na awe shahidi kwamba nitamchunguza baba yangu wakati kama huu kesho au siku ya tatu. Ikiwa ana mtazamo mzuri kukuelekea, je, sitakujulisha au kukufunulia jambo hilo? 13  Lakini ikiwa baba yangu anakusudia kukudhuru, Yehova na aniadhibu, tena vikali, ikiwa sitakufunulia jambo hilo na kuacha uende zako kwa amani. Yehova na awe pamoja nawe,+ kama alivyokuwa na baba yangu.+ 14  Na je, hutanitendea kwa upendo mshikamanifu wa Yehova ningali hai na hata nikifa?+ 15  Usiache kamwe kuitendea nyumba yangu kwa upendo mshikamanifu,+ hata Yehova atakapowafagilia mbali maadui wote wa Daudi duniani pote.” 16  Basi Yonathani akafanya agano pamoja na nyumba ya Daudi, akisema: “Yehova atadai jambo hilo na kuwaadhibu maadui wa Daudi.” 17  Basi Yonathani akamwapisha tena Daudi kwa msingi wa upendo aliokuwa nao kumwelekea, kwa sababu alimpenda kama alivyojipenda mwenyewe.*+ 18  Kisha Yonathani akamwambia: “Kesho ni mwezi mpya,+ nawe utakosekana kwa sababu kiti chako kitakuwa wazi. 19  Kufikia siku ya tatu, wataona wazi kwamba haupo, utakuja mahali hapa ulipojificha ile siku nyingine* na ukae hapa karibu na jiwe. 20  Kisha nitapiga mishale mitatu upande mmoja wa jiwe hili kana kwamba ninalenga shabaha fulani. 21  Nitakapomtuma mtumishi, nitasema, ‘Nenda, ukaitafute mishale.’ Nikimwambia mtumishi, ‘Angalia! Mishale iko upande huu wako, ichukue,’ basi unaweza kurudi, kwa maana kwa hakika kama Yehova anavyoishi, hilo linamaanisha kwamba kuna amani katika mambo yako yote na hakuna hatari. 22  Lakini nikimwambia mvulana huyo, ‘Angalia! Mishale iko mbele yako,’ basi ondoka, kwa sababu Yehova anataka uende zako. 23  Kuhusu ahadi ambayo tumeweka,+ mimi na wewe, Yehova na awe kati yetu milele.”+ 24  Basi Daudi akajificha shambani. Mwezi mpya ulipofika, mfalme aliketi kwenye kiti chake ili ale.+ 25  Mfalme alikuwa ameketi mahali pake alipoketi kwa kawaida karibu na ukuta. Yonathani aliketi kumwelekea, na Abneri+ aliketi kando ya Sauli, lakini mahali pa Daudi palikuwa wazi. 26  Sauli hakusema lolote siku hiyo, kwa maana alisema moyoni mwake: ‘Jambo fulani limetokea ambalo limemfanya asiwe safi.+ Naam, yeye si safi.’ 27  Siku ya pili baada ya mwezi mpya, bado mahali pa Daudi palikuwa wazi. Kwa hiyo Sauli akamuuliza Yonathani mwana wake: “Kwa nini mwana wa Yese+ hakuja kwenye mlo jana wala leo?” 28  Yonathani akamjibu Sauli: “Daudi alinisihi nimruhusu aende Bethlehemu.+ 29  Aliniambia, ‘Tafadhali niruhusu niende, kwa sababu tuna dhabihu ya familia jijini, na ndugu yangu mwenyewe aliniita. Basi ikiwa nimepata kibali machoni pako, tafadhali acha niende kisiri nikawaone ndugu zangu.’ Ndiyo sababu hajaja kwenye meza ya mfalme.” 30  Kisha Sauli akamkasirikia Yonathani na kumwambia: “Wewe mwana wa mwanamke mwasi, unafikiri sijui kwamba umeamua kumuunga mkono mwana wa Yese, kwa aibu yako mwenyewe na kwa aibu ya mama yako?* 31  Maadamu mwana wa Yese anaishi duniani, wewe wala ufalme wako hautadumu.+ Basi sasa mtume mtu fulani amlete kwangu, kwa maana lazima afe.”*+ 32  Hata hivyo, Yonathani akamwambia Sauli baba yake: “Kwa nini auawe?+ Amefanya nini?” 33  Ndipo Sauli akamtupia mkuki ili amuue,+ basi Yonathani akajua kwamba baba yake alikuwa ameazimia kumuua Daudi.+ 34  Yonathani akainuka mara moja kutoka mezani akiwa amekasirika sana, naye hakula chakula chochote siku ya pili baada ya mwezi mpya, kwa maana alikuwa amehuzunika sana kwa sababu ya Daudi+ na kwa sababu baba yake mwenyewe alikuwa amemwaibisha. 35  Asubuhi Yonathani akaenda shambani kukutana na Daudi kama walivyokubaliana, na mtumishi fulani kijana alikuwa pamoja naye.+ 36  Akamwambia mtumishi wake: “Tafadhali kimbia utafute mishale nitakayopiga.” Mtumishi huyo akakimbia, kisha Yonathani akapiga mshale mbele yake. 37  Mtumishi huyo alipofika mahali ambapo Yonathani alikuwa amepiga mshale, Yonathani akamwambia hivi mtumishi huyo kwa sauti: “Mshale uko mbele yako!” 38  Yonathani akaendelea kumwambia mtumishi huyo kwa sauti: “Fanya haraka! Kimbia! Usikawie!” Mtumishi wa Yonathani akaiokota ile mishale na kurudi kwa bwana wake. 39  Lakini mtumishi huyo hakuelewa lolote kuhusu jambo hilo; Yonathani na Daudi peke yao ndio walioelewa jambo hilo. 40  Kisha Yonathani akampa mtumishi wake silaha zake na kumwambia: “Nenda, zipeleke jijini.” 41  Mtumishi huyo alipoondoka, Daudi akatoka mahali alipokuwa amejificha hapo karibu upande wa kusini. Kisha akaanguka chini kifudifudi na kuinama mara tatu, nao wakabusiana na kulia pamoja, lakini Daudi alilia zaidi. 42  Yonathani akamwambia Daudi: “Nenda kwa amani, kwa maana sote wawili tumeapa+ kwa jina la Yehova tukisema, ‘Yehova na awe kati yangu na wewe na kati ya uzao wangu* na uzao wako* milele.’”+ Kisha Daudi akainuka na kuondoka, naye Yonathani akarudi jijini.

Maelezo ya Chini

Au “nafsi yako inavyoishi.”
Au “kama nafsi yake mwenyewe.”
Tnn., “siku ya kazi.”
Tnn., “kwa aibu ya uchi wa mama yako?”
Tnn., “kwa maana yeye ni mwana wa kifo.”
Tnn., “mbegu yangu.”
Tnn., “mbegu yako.”