Kitabu cha Kwanza cha Samweli 23:1-29

  • Daudi aliokoa jiji la Keila (1-12)

  • Sauli amfuatia Daudi (13-15)

  • Yonathani amtia nguvu Daudi (16-18)

  • Daudi anusurika kukamatwa na Sauli (19-29)

23  Baada ya muda Daudi aliambiwa hivi: “Wafilisti wanashambulia Keila,+ nao wanapora nafaka kwenye viwanja vya kupuria.”  Basi Daudi akamuuliza Yehova:+ “Je, niende nikawaue Wafilisti hawa?” Yehova akamwambia Daudi: “Nenda, waue Wafilisti hao na kuokoa Keila.”  Lakini wanaume wa Daudi wakamwambia: “Tazama! Ikiwa tunaogopa tukiwa hapa Yuda,+ itakuwaje tukienda Keila kupigana na vikosi vya Wafilisti?”+  Kwa hiyo Daudi akamwomba tena Yehova ushauri.+ Sasa Yehova akamjibu hivi: “Ondoka, ushuke kwenda Keila kwa sababu nitawatia Wafilisti mikononi mwako.”+  Basi Daudi akaenda na wanaume wake Keila na kupigana na Wafilisti; akachukua mifugo yao na kuwaua Wafilisti wengi sana, Daudi akawaokoa wakaaji wa Keila.+  Sasa Abiathari+ mwana wa Ahimeleki alipokimbia kwenda kwa Daudi huko Keila, alikuwa na efodi.  Sauli akaambiwa hivi: “Daudi amekuja Keila.” Sauli akasema: “Mungu amemtia mikononi mwangu,*+ kwa maana amejiingiza mwenyewe ndani ya mtego kwa kuingia katika jiji lenye milango na makomeo.”  Kwa hiyo Sauli akawakusanya watu wote waende vitani, washuke Keila na kumzingira Daudi na wanaume wake.  Daudi alipopata habari kwamba Sauli alikuwa akipanga njama dhidi yake, akamwambia kuhani Abiathari: “Ilete efodi hapa.”+ 10  Kisha Daudi akasema: “Ee Yehova Mungu wa Israeli, mimi mtumishi wako nimesikia kwa hakika kwamba Sauli anakusudia kuja Keila kuliangamiza jiji hili kwa sababu yangu.+ 11  Je, viongozi* wa Keila watanitia mikononi mwake? Je, Sauli atashuka kuja hapa kama mimi mtumishi wako nilivyosikia? Ee Yehova Mungu wa Israeli, tafadhali nijulishe mimi mtumishi wako.” Ndipo Yehova akamwambia: “Atashuka.” 12  Daudi akauliza: “Je, viongozi wa Keila watanitia mimi na wanaume wangu mikononi mwa Sauli?” Yehova akajibu: “Watakutia mikononi mwake.” 13  Mara moja Daudi akainuka pamoja na wanaume wake, wapatao 600,+ wakaondoka Keila na kwenda popote walipoweza kwenda. Sauli alipoambiwa kwamba Daudi ametoroka Keila, hakumfuatia. 14  Daudi akakaa nyikani katika sehemu ambazo hazifikiki kwa urahisi, kwenye eneo lenye milima katika nyika ya Zifu.+ Sauli aliendelea kumtafuta,+ lakini Yehova hakumtia Daudi mikononi mwake. 15  Daudi alijua kwamba* Sauli alikuwa akimtafuta ili amuue* Daudi alipokuwa katika nyika ya Zifu huko Horeshi. 16  Sasa Yonathani mwana wa Sauli akaenda kumwona Daudi huko Horeshi, akamsaidia kupata nguvu* katika Yehova.+ 17  Akamwambia: “Usiogope, kwa maana Sauli baba yangu hatakupata; utakuwa mfalme wa Israeli,+ nami nitakuwa wa pili baada yako; na Sauli baba yangu anajua jambo hilo.”+ 18  Kisha wote wawili wakafanya agano+ mbele za Yehova, na Daudi akaendelea kukaa Horeshi, naye Yonathani akaenda nyumbani kwake. 19  Baadaye watu wa Zifu wakapanda kwenda kwa Sauli kule Gibea+ na kumwambia: “Daudi anajificha karibu nasi+ katika sehemu ambazo hazifikiki kwa urahisi kule Horeshi,+ kwenye kilima cha Hakila,+ kilicho upande wa kusini* wa Yeshimoni.*+ 20  Wakati wowote utakaopenda kushuka huko, Ee mfalme, shuka, nasi tutamtia mikononi mwako mfalme.”+ 21  Ndipo Sauli akasema: “Yehova na awabariki kwa sababu mmenihurumia. 22  Tafadhali nendeni mjaribu kutafuta mahali hususa alipo na mtu aliyemwona huko, kwa sababu nimeambiwa kwamba yeye ni mjanja sana. 23  Chunguzeni kwa makini kila mahali anapojificha na mrudi kwangu mkiwa na ushahidi. Kisha nitaenda pamoja nanyi, na ikiwa yuko nchini, nitamsaka kabisa miongoni mwa maelfu yote ya* Yuda.” 24  Basi wakaondoka na kumtangulia Sauli kwenda Zifu,+ na wakati huo Daudi na wanaume wake walikuwa katika nyika ya Maoni,+ kule Araba+ upande wa kusini wa Yeshimoni. 25  Kisha Sauli akaja na wanaume wake kumtafuta.+ Daudi alipoambiwa jambo hilo, akashuka mara moja na kwenda kwenye mwamba,+ naye akakaa katika nyika ya Maoni. Sauli aliposikia hilo, akamfuatia Daudi katika nyika ya Maoni. 26  Sauli alipofika upande mmoja wa mlima, Daudi na wanaume wake walikuwa upande wa pili wa mlima huo. Daudi alikuwa akifanya haraka kumkimbia+ Sauli, lakini Sauli na wanaume wake walikuwa wakimkaribia Daudi na wanaume wake ili wawakamate.+ 27  Lakini mjumbe fulani akaja kwa Sauli na kumwambia: “Njoo haraka, kwa sababu Wafilisti wameivamia nchi!” 28  Ndipo Sauli akaacha kumfuatia Daudi,+ akaenda kukabiliana na Wafilisti. Ndiyo sababu mahali hapo paliitwa Mwamba wa Migawanyiko. 29  Kisha Daudi akapanda kutoka huko na kwenda kukaa katika sehemu ambazo hazifikiki kwa urahisi kule En-gedi.+

Maelezo ya Chini

Tnn., “amemuuza mikononi mwangu.”
Au labda, “wamiliki wa mashamba.”
Au labda, “Daudi aliogopa kwa sababu.”
Au “alikuwa akiitafuta nafsi yake.”
Tnn., “akauimarisha mkono wake.”
Tnn., “upande wa kulia.”
Au labda, “wa jangwa; nyika.”
Au “koo zote za.”