Kitabu cha Kwanza cha Samweli 24:1-22

  • Daudi amwacha hai Sauli (1-22)

    • Daudi amheshimu mtiwa-mafuta wa Yehova (6)

24  Mara tu Sauli aliporudi baada ya kuwafuatia Wafilisti, aliambiwa hivi: “Tazama! Daudi yuko katika nyika ya En-gedi.”+  Basi Sauli akachukua wanaume 3,000 mashujaa kutoka nchi yote ya Israeli na kwenda kumtafuta Daudi na wanaume wake kwenye miamba ya mbuzi wa milimani.  Sauli akafika kwenye mazizi ya kondoo yaliyojengwa kwa mawe kando ya barabara, mahali ambapo palikuwa na pango, akaingia pangoni kwenda haja,* wakati huo Daudi na wanaume wake walikuwa wameketi ndani kabisa ya pango hilo.+  Wanaume wa Daudi wakamwambia: “Hii ndiyo siku ambayo Yehova anakwambia, ‘Tazama! Ninamtia adui yako mikononi mwako,+ nawe unaweza kumtendea jambo lolote unalotaka.’” Kwa hiyo Daudi akasimama, akakata kimyakimya upindo wa joho la Sauli lisilo na mikono.  Lakini baadaye moyo wa Daudi ukaendelea kumchoma*+ kwa sababu alikuwa amekata upindo wa joho la Sauli lisilo na mikono.  Akawaambia wanaume wake: “Siwezi kamwe kuwazia, kulingana na maoni ya Yehova, kumtendea jambo kama hilo bwana wangu, mtiwa-mafuta wa Yehova, kwa kuinua mkono wangu dhidi yake, kwa kuwa yeye ni mtiwa-mafuta wa Yehova.”+  Basi Daudi akawazuia* wanaume wake kwa maneno hayo, naye hakuwaruhusu wamshambulie Sauli. Sauli akaondoka pangoni na kwenda zake.  Baadaye Daudi akainuka na kutoka pangoni, akamwita Sauli: “Bwana wangu mfalme!”+ Sauli alipoangalia nyuma, Daudi aliinama hadi chini kifudifudi na kusujudu.  Daudi akamuuliza Sauli: “Kwa nini unasikiliza maneno ya watu wanaosema, ‘Tazama! Daudi anataka kukudhuru’?+ 10  Siku hii ya leo umeona kwa macho yako mwenyewe jinsi Yehova alivyokutia mikononi mwangu pangoni. Lakini mtu fulani aliposema nikuue,+ nilikusikitikia nikasema, ‘Sitainua mkono wangu dhidi ya bwana wangu, kwa maana yeye ni mtiwa-mafuta wa Yehova.’+ 11  Tazama baba yangu, angalia nimeshika upindo wa joho lako lisilo na mikono; kwa sababu nilipokata upindo wa joho lako lisilo na mikono, sikukuua. Sasa unaweza kuona na kuelewa kwamba sikusudii kukudhuru wala kukuasi, nami sijakutendea dhambi,+ lakini wewe unaniwinda ili kuniua.*+ 12  Yehova na ahukumu kati yangu na wewe,+ na Yehova anilipizie kisasi mambo unayonitendea,+ lakini sitainua mkono wangu dhidi yako.+ 13  Kama methali ya kale inavyosema, ‘Kutoka kwa mwovu hutoka uovu,’ lakini sitainua mkono wangu dhidi yako. 14  Mfalme wa Israeli ametoka kumtafuta nani? Unamfuatia nani? Mbwa aliyekufa? Kiroboto mmoja?+ 15  Yehova na awe mwamuzi, atahukumu kati yangu na wewe, naye ataona na kunitetea na kuamua kesi yangu+ na kuniokoa kutoka mikononi mwako.” 16  Mara tu Daudi alipomaliza kumwambia maneno hayo, Sauli akasema: “Je, hiyo ni sauti yako, Daudi mwanangu?”+ Kisha Sauli akaanza kulia kwa sauti kubwa. 17  Akamwambia Daudi: “Wewe ni mwadilifu kuliko mimi, kwa maana umenitendea mema lakini mimi nimekulipa kwa uovu.+ 18  Naam, leo umeniambia mema uliyotenda kwa kukosa kuniua Yehova aliponitia mikononi mwako.+ 19  Ni mtu gani anayempata adui yake na kumwacha aende zake bila kumdhuru? Yehova atakuthawabisha wewe kwa mema+ kwa sababu ya mambo uliyonifanyia leo. 20  Sasa tazama! Najua kwa hakika kwamba utatawala ukiwa mfalme+ na kwamba ufalme wa Israeli utadumu mikononi mwako. 21  Sasa niapie mbele za Yehova+ kwamba hutawafagilia mbali wazao wangu* baada yangu na kwamba hutalifutilia mbali jina langu kutoka katika nyumba ya baba yangu.”+ 22  Kwa hiyo Daudi akamwapia Sauli, kisha Sauli akaenda nyumbani kwake.+ Lakini Daudi na wanaume wake wakapanda kwenda ndani ya ngome.+

Maelezo ya Chini

Tnn., “afunike miguu yake.”
Au “dhamiri ya Daudi ikaendelea kumchoma.”
Au labda, “akawatawanya.”
Au “kuiua nafsi yangu.”
Tnn., “mbegu yangu.”