Kitabu cha Kwanza cha Samweli 26:1-25

  • Daudi amwacha hai tena Sauli (1-25)

    • Daudi amheshimu mtiwa-mafuta wa Yehova (11)

26  Baada ya muda watu wa Zifu+ wakaja kwa Sauli huko Gibea,+ wakisema: “Daudi amejificha kwenye kilima cha Hakila, ng’ambo ya Yeshimoni.”*+  Basi Sauli akaondoka na kushuka kwenda katika nyika ya Zifu akiwa na wanaume 3,000 mashujaa wa Israeli ili kumtafuta Daudi katika nyika ya Zifu.+  Sauli akapiga kambi kwenye kilima cha Hakila, kilicho ng’ambo ya Yeshimoni, kando ya barabara. Wakati huo Daudi alikuwa akiishi nyikani, akapata habari kwamba Sauli alikuwa amekuja nyikani kumtafuta.  Basi Daudi akatuma wapelelezi ili wathibitishe kwamba kwa kweli Sauli alikuwa amekuja.  Baadaye Daudi akaenda mahali ambapo Sauli alikuwa amepiga kambi, na Daudi akaona mahali ambapo Sauli na Abneri+ mwana wa Neri, mkuu wa jeshi lake, walikuwa wamelala; Sauli alikuwa amelala ndani ya kambi akiwa amezungukwa na wanajeshi.  Kisha Daudi akamuuliza hivi Ahimeleki Mhiti+ na Abishai+ mwana wa Seruya,+ ndugu ya Yoabu: “Ni nani atakayeshuka pamoja nami kwenda kwa Sauli kambini?” Abishai akajibu: “Mimi nitashuka pamoja nawe.”  Basi Daudi na Abishai wakaenda kwa jeshi hilo usiku, wakamkuta Sauli amelala ndani ya kambi mkuki wake ukiwa umedungwa ardhini karibu na kichwa chake; Abneri na wanajeshi walikuwa wamelala kumzunguka Sauli.  Ndipo Abishai akamwambia Daudi: “Leo Mungu amemtia adui yako mikononi mwako.+ Na sasa tafadhali, acha nimpigilie ardhini kwa mkuki mara moja tu, wala sitafanya hivyo mara mbili.”  Hata hivyo, Daudi akamwambia Abishai: “Usimdhuru, kwa maana ni nani anayeweza kuinua mkono wake dhidi ya mtiwa-mafuta wa Yehova+ na asiwe na hatia?”+ 10  Daudi akaendelea kusema: “Kwa hakika kama Yehova anavyoishi, Yehova mwenyewe atampiga,+ au siku yake itafika+ naye atakufa, au ataenda vitani na kuuawa.+ 11  Ni jambo nisiloweza kamwe kuwazia, kulingana na maoni ya Yehova, kwamba niinue mkono wangu dhidi ya mtiwa-mafuta wa Yehova!+ Sasa, tafadhali, chukua huo mkuki ulio karibu na kichwa chake na hilo gudulia la maji, twende zetu.” 12  Basi Daudi akachukua mkuki na gudulia la maji karibu na kichwa cha Sauli, wakaenda zao. Hakuna yeyote aliyejua wala kuwaona+ wala kuamka, kwa maana wote walikuwa wamelala, kwa sababu walikuwa wameshikwa na usingizi mzito kutoka kwa Yehova. 13  Kisha Daudi akavuka ng’ambo na kusimama juu ya mlima uliokuwa umbali fulani kutoka kwenye kambi ya Sauli. 14  Daudi akawaita kwa sauti wanajeshi hao na Abneri+ mwana wa Neri, akisema: “Abneri, unanisikia?” Abneri akajibu: “Wewe ni nani unayemwita mfalme?” 15  Daudi akamwambia Abneri: “Je, wewe si mwanamume? Na ni nani aliye kama wewe katika Israeli? Kwa nini basi hukumlinda bwana wako mfalme? Kwa sababu mwanajeshi mmoja aliingia kambini ili kumwangamiza bwana wako mfalme.+ 16  Jambo ulilofanya si zuri. Kwa hakika kama Yehova anavyoishi, mnastahili kufa, kwa sababu hamkuendelea kumlinda bwana wenu, mtiwa-mafuta wa Yehova.+ Sasa angalia kila mahali! Uko wapi mkuki wa mfalme na gudulia la maji+ lililokuwa karibu na kichwa chake?” 17  Ndipo Sauli akaitambua sauti ya Daudi na kumuuliza: “Je, hiyo ni sauti yako mwanangu Daudi?”+ Daudi akajibu: “Ni sauti yangu, bwana wangu mfalme.” 18  Halafu akaendelea kusema: “Bwana wangu kwa nini unanifuatia mimi mtumishi wako,+ nimefanya nini, nami nina hatia ya kosa gani?+ 19  Tafadhali, bwana wangu mfalme, yasikilize maneno yangu mimi mtumishi wako: Ikiwa ni Yehova aliyekuchochea dhidi yangu, acha akubali* toleo langu la nafaka. Lakini ikiwa ni wanadamu wamekuchochea,+ wamelaaniwa mbele za Yehova, kwa sababu leo wamenifukuza ili nisiungane na urithi wa Yehova,+ wakisema, ‘Nenda, abudu miungu mingine!’ 20  Na sasa usiache damu yangu imwagike ardhini mbali kutoka mbele za* Yehova, kwa maana mfalme wa Israeli ametoka kwenda kutafuta kiroboto mmoja,+ kama mtu anayewinda kware milimani.” 21  Ndipo Sauli akasema: “Nimetenda dhambi.+ Rudi, mwanangu Daudi, kwa maana sitakudhuru tena, kwa sababu umeona uhai wangu kuwa wenye* thamani+ leo. Naam, nimetenda kipumbavu, nami nimekosea sana.” 22  Daudi akamwambia: “Mkuki wa mfalme ndio huu. Mruhusu mmoja wa vijana wako aje kuuchukua. 23  Yehova ndiye atakayemlipa kila mtu kulingana na uadilifu wake mwenyewe+ na uaminifu wake mwenyewe, kwa kuwa leo Yehova alikutia mikononi mwangu, lakini sikutaka kuinua mkono wangu dhidi ya mtiwa-mafuta wa Yehova.+ 24  Tazama! Kama nilivyoona uhai wako kuwa wenye* thamani leo, uhai wangu na uwe wenye* thamani machoni pa Yehova, na aniokoe kutoka katika mateso yote.”+ 25  Sauli akamwambia Daudi: “Ubarikiwe, mwanangu Daudi. Hakika utatenda mambo makubwa, na hakika utashinda.”+ Kisha Daudi akaenda zake, na Sauli akarudi kwake.+

Maelezo ya Chini

Au labda, “jangwa; nyika.”
Tnn., “anuse.”
Au “kutoka kwenye uwepo wa.”
Au “umeona nafsi yangu kuwa yenye.”
Au “nafsi yako kuwa yenye.”
Au “nafsi yangu na iwe yenye.”