Kitabu cha Kwanza cha Samweli 3:1-21

  • Samweli aitwa awe nabii (1-21)

3  Wakati huo, mvulana Samweli alikuwa akimhudumia+ Yehova chini ya uangalizi wa Eli, lakini neno la Yehova lilikuwa haba siku hizo; maono+ hayakuwa mengi.  Siku moja Eli alikuwa amelala mahali alipozoea kulala, na macho yake yalikuwa yamedhoofika; hangeweza kuona.+  Taa ya Mungu+ haikuwa imezimwa, na Samweli alikuwa amelala katika hekalu*+ la Yehova, mahali ambapo Sanduku la Mungu lilikuwa.  Kisha Yehova akamwita Samweli. Samweli akajibu: “Mimi hapa.”  Akakimbia kwa Eli na kusema, “Nimekuja, kwa kuwa umeniita.” Lakini Eli akasema: “Sikukuita. Rudi ukalale.” Basi akaenda kulala.  Yehova akaita tena: “Samweli!” Basi Samweli akaamka na kwenda kwa Eli, akamwambia: “Nimekuja, kwa kuwa umeniita.” Lakini Eli akamwambia: “Sikukuita, mwanangu. Rudi ukalale.”  (Wakati huo Samweli alikuwa bado hajamjua Yehova, na neno la Yehova lilikuwa bado halijafunuliwa kwake.)+  Yehova akaita tena mara ya tatu: “Samweli!” Basi akaamka, akaenda kwa Eli na kumwambia: “Nimekuja, kwa kuwa umeniita.” Ndipo Eli akatambua kwamba ni Yehova aliyekuwa akimwita mvulana huyo.  Kwa hiyo Eli akamwambia Samweli: “Rudi ukalale, na akikuita, mwambie, ‘Sema, Yehova, kwa maana mtumishi wako anasikiliza.’” Basi Samweli akaenda na kulala mahali alipokuwa akilala. 10  Yehova akaja na kusimama mahali hapo, akaita kama alivyofanya awali: “Samweli, Samweli!” Ndipo Samweli akajibu: “Sema, kwa maana mtumishi wako anasikiliza.” 11  Yehova akamwambia Samweli: “Tazama! Ninafanya jambo fulani katika Israeli ambalo litawasha masikio yote mawili ya mtu yeyote atakayelisikia.+ 12  Siku hiyo nitamtendea Eli mambo yote niliyosema kuhusu nyumba yake, kuanzia mwanzo mpaka mwisho.+ 13  Ni lazima umwambie kwamba ninailetea nyumba yake hukumu ya kudumu kwa sababu ya dhambi ambayo anaijua,+ kwa maana wanawe wanamtukana Mungu,+ lakini hajawakemea.+ 14  Ndiyo sababu nimeiapia nyumba ya Eli kwamba dhambi ya nyumba ya Eli haitafunikwa kamwe kwa dhabihu au kwa matoleo.”+ 15  Samweli akaendelea kulala mpaka asubuhi; kisha akafungua milango ya nyumba ya Yehova. Samweli akaogopa kumwambia Eli maono hayo. 16  Lakini Eli akaagiza Samweli aitwe, akamwambia: “Samweli, mwanangu!” Naye akasema: “Naam.”⁠ 17  Eli akamuuliza, “Alikupa ujumbe gani? Tafadhali, usinifiche. Mungu na akuadhibu, tena vikali, ukinificha neno hata moja kati ya maneno yote ambayo alikwambia.” 18  Basi Samweli akamwambia kila jambo, wala hakumficha lolote. Eli akasema: “Ni Yehova. Na afanye yaliyo mema machoni pake.” 19  Samweli akaendelea kukua, na Yehova mwenyewe alikuwa pamoja naye+ na hakuruhusu neno lolote kati ya maneno yake yote likose kutimia.* 20  Waisraeli wote kuanzia Dani mpaka Beer-sheba wakapata habari kwamba Samweli alikuwa amewekwa rasmi kuwa nabii wa Yehova. 21  Na Yehova akaendelea kutokea huko Shilo, kwa kuwa Yehova alijidhihirisha kwa Samweli huko Shilo kwa neno lake Yehova.+

Maelezo ya Chini

Yaani, hema la ibada.
Tnn., “lianguke ardhini.”