Kitabu cha Kwanza cha Samweli 5:1-12

  • Sanduku la agano katika eneo la Wafilisti (1-12)

    • Dagoni aaibishwa (1-5)

    • Wafilisti waletewa pigo (6-12)

5  Wafilisti walipoliteka Sanduku la Mungu+ wa kweli walilibeba kutoka Ebenezeri mpaka Ashdodi.  Wafilisti wakalichukua Sanduku la Mungu wa kweli, wakaliingiza ndani ya nyumba ya* Dagoni na kuliweka kando ya Dagoni.+  Siku iliyofuata Waashdodi walipoamka asubuhi na mapema, walimkuta Dagoni ameanguka kifudifudi mbele ya Sanduku la Yehova.+ Basi wakamchukua Dagoni na kumrudisha mahali pake.+  Walipoamka asubuhi na mapema siku iliyofuata, walimkuta Dagoni ameanguka kifudifudi mbele ya Sanduku la Yehova. Kichwa cha Dagoni na vitanga vya mikono yake miwili vilikuwa vimekatwa, navyo vilikuwa chini kwenye kizingiti. Ni sehemu tu yenye umbo la samaki ndiyo iliyobaki.*  Ndiyo sababu mpaka leo hii, makuhani wa Dagoni na wote wanaoingia katika nyumba ya Dagoni hawakanyagi kizingiti cha Dagoni kule Ashdodi.  Mkono wa Yehova uliwaadhibu vikali* Waashdodi, naye akawaangamiza kwa kuleta bawasiri* huko Ashdodi na katika maeneo yake.+  Watu wa Ashdodi walipoona mambo yaliyokuwa yakitukia wakasema: “Msiruhusu Sanduku la Mungu wa Israeli likae pamoja nasi, kwa sababu mkono wake umetuadhibu vikali sisi pamoja na mungu wetu Dagoni.”  Basi wakatuma ujumbe na kuwakusanya watawala wote wa Wafilisti na kuwauliza: “Tulifanyie nini Sanduku la Mungu wa Israeli?” Wakajibu: “Acheni Sanduku la Mungu wa Israeli lihamishiwe kule Gathi.”+ Basi wakalihamishia huko Sanduku la Mungu wa Israeli.  Baada ya kulihamishia huko, mkono wa Yehova ukaja dhidi ya jiji hilo, na kusababisha hofu kubwa. Akawapiga wanaume wa jiji hilo, kuanzia mdogo mpaka mkubwa, wakatokwa na majipu ya bawasiri.+ 10  Basi wakalipeleka Sanduku la Mungu wa kweli kule Ekroni,+ lakini mara tu Sanduku la Mungu wa kweli lilipofika Ekroni, Waekroni wakaanza kulia kwa sauti wakisema: “Wametuletea Sanduku la Mungu wa Israeli ili watuue sisi pamoja na watu wetu!”+ 11  Kwa hiyo wakatuma ujumbe na kuwakusanya watawala wote wa Wafilisti na kuwaambia: “Liondoeni hapa Sanduku la Mungu wa Israeli; lirudisheni mahali pake ili sisi pamoja na watu wetu tusiuawe.” Kwa maana hofu ya kifo ilikuwa imeenea katika jiji lote; mkono wa Mungu wa kweli ulikuwa umewaadhibu vikali sana watu wa jiji hilo,+ 12  na watu ambao hawakufa walikuwa wamepigwa na bawasiri. Na kilio cha jiji hilo cha kuomba msaada kikapanda mpaka mbinguni.

Maelezo ya Chini

Au “hekalu la.”
Tnn., “Ni Dagoni tu aliyebaki.”
Tnn., “ulikuwa mzito dhidi ya.”
Au “ugonjwa wa puru.”