Kitabu cha Kwanza cha Samweli 6:1-21

  • Wafilisti warudisha sanduku la agano Israeli (1-21)

6  Sanduku+ la Yehova lilikaa katika eneo la Wafilisti kwa miezi saba.  Wafilisti wakawaita makuhani na wabashiri,+ wakawauliza: “Tulifanyie nini Sanduku la Yehova? Tuambieni jinsi tunavyopaswa kulirudisha mahali pake.”  Wakajibu: “Mkilirudisha sanduku la agano la Yehova, Mungu wa Israeli, msilirudishe bila dhabihu. Kwa vyovyote vile mnapaswa kumrudishia pamoja na dhabihu ya hatia.+ Ndipo tu mtakapoponywa, nanyi mtajulishwa kwa nini mkono wake unaendelea kuwaadhibu.”  Basi wakauliza: “Tunapaswa kumpelekea dhabihu gani ya hatia?” Wakasema: “Kulingana na idadi ya watawala wa Wafilisti,+ pelekeni bawasiri tano za dhahabu na panya watano wa dhahabu, kwa maana kila mmoja wenu pamoja na watawala wenu wamepatwa na pigo lilelile.  Mnapaswa kutengeneza sanamu za bawasiri zenu na sanamu za panya+ wenu wanaoiharibu nchi, nanyi mnapaswa kumheshimu Mungu wa Israeli. Labda atapunguza adhabu ya mkono wake dhidi yenu na dhidi ya mungu wenu na nchi yenu.+  Kwa nini mfanye mioyo yenu iwe migumu kama Wamisri na Farao walivyofanya mioyo yao kuwa migumu?+ Alipowaadhibu vikali,+ walilazimika kuwaruhusu Waisraeli waende zao, nao wakaondoka.+  Sasa tayarisheni gari jipya la kukokotwa na ng’ombe wawili wanaonyonyesha ambao hawajawahi kamwe kufungwa nira. Kisha muwafunge ng’ombe hao kwenye gari hilo, lakini muwarudishe ndama wao nyumbani ili wasiwafuate.  Chukueni Sanduku la Yehova na kuliweka juu ya gari hilo, nanyi wekeni ndani ya sanduku lingine kando yake vitu vya dhahabu mnavyompelekea kuwa dhabihu ya hatia.+ Kisha mliache gari liende  huku mkilitazama: Ikiwa litapanda kwenye barabara inayoelekea Beth-shemeshi,+ kwenye eneo lake, basi yeye ndiye ametutendea uovu huu mkubwa. Lakini lisipopanda huko, tutajua kwamba si mkono wake uliotuadhibu; ni msiba wa kawaida tu uliotupata.” 10  Watu hao wakafanya hivyo. Wakachukua ng’ombe wawili wanaonyonyesha, wakawafunga kwenye gari hilo, na kuwafungia ndama wao nyumbani ndani ya zizi. 11  Kisha wakaliweka Sanduku la Yehova juu ya gari hilo, pamoja na sanduku lenye panya wa dhahabu na sanamu za bawasiri zao. 12  Ng’ombe hao wakaenda moja kwa moja kwenye barabara inayoelekea Beth-shemeshi.+ Walibaki kwenye barabara hiyo kuu, nao walikuwa wakilia walipokuwa wakienda; hawakugeuka kulia wala kushoto. Wakati huo wote, watawala wa Wafilisti walikuwa wakitembea nyuma yao hadi kwenye mpaka wa Beth-shemeshi. 13  Watu wa Beth-shemeshi walikuwa wakivuna ngano katika bonde tambarare. Walipoinua macho yao na kuona lile Sanduku, wakashangilia sana kuliona. 14  Gari hilo likafika kwenye shamba la Yoshua Mbeth-shemeshi, likasimama karibu na jiwe kubwa. Basi wakapasua mbao za gari hilo, na kuwatoa ng’ombe+ hao kuwa dhabihu ya kuteketezwa kwa Yehova. 15  Walawi+ wakalishusha Sanduku la Yehova na sanduku lililokuwa kando yake ambalo lilikuwa na vile vitu vya dhahabu, wakaviweka juu ya lile jiwe kubwa. Watu wa Beth-shemeshi+ wakamtolea Yehova dhabihu za kuteketezwa na dhabihu nyingine siku hiyo. 16  Watawala watano wa Wafilisti walipoona hayo, wakarudi Ekroni siku hiyo. 17  Basi hizi ndizo bawasiri za dhahabu ambazo Wafilisti walimletea Yehova kuwa dhabihu ya hatia:+ moja kwa ajili ya Ashdodi,+ moja kwa ajili ya Gaza, moja kwa ajili ya Ashkeloni, moja kwa ajili ya Gathi,+ moja kwa ajili ya Ekroni.+ 18  Na idadi ya panya wa dhahabu ililingana na idadi ya majiji yote ya Wafilisti ya wale watawala watano, majiji yenye ngome na vijiji vya mashambani visivyo na kuta. Na jiwe kubwa ambalo waliweka Sanduku la Yehova juu yake ni ushahidi mpaka leo katika shamba la Yoshua Mbeth-shemeshi. 19  Lakini Mungu akawaua watu wa Beth-shemeshi, kwa sababu walilitazama Sanduku la Yehova. Aliwaua watu 50,070* miongoni mwao, basi watu wakaanza kuomboleza kwa sababu Yehova alikuwa amewaua kwa mauaji makubwa.+ 20  Kwa hiyo watu wa Beth-shemeshi wakauliza: “Ni nani atakayeweza kusimama mbele za Yehova, huyu Mungu mtakatifu,+ naye ataenda kwa nani akitoka kwetu?”+ 21  Basi wakawatuma wajumbe kwa wakaaji wa Kiriath-yearimu,+ wakisema: “Wafilisti wamelirudisha Sanduku la Yehova. Shukeni mlichukue na kupanda nalo.”+

Maelezo ya Chini

Tnn., “wanaume 70, wanaume 50,000.”