Kitabu cha Kwanza cha Samweli 7:1-17

  • Sanduku la agano laletwa Kiriath-yearimu (1)

  • Samweli ahimiza hivi: ‘Mtumikieni Yehova peke yake’ (2-6)

  • Ushindi wa Waisraeli kule Mispa (7-14)

  • Samweli awa mwamuzi wa Israeli (15-17)

7  Basi watu wa Kiriath-yearimu wakaja na kulichukua Sanduku la Yehova na kulipandisha katika nyumba ya Abinadabu+ juu ya kilima, nao wakamtakasa Eleazari mwanawe ili alilinde Sanduku la Yehova.  Muda mrefu ulipita, jumla ya miaka 20, tangu Sanduku hilo lilipoletwa Kiriath-yearimu, na nyumba yote ya Israeli kuanza kumtafuta* Yehova.+  Kisha Samweli akaiambia nyumba yote ya Israeli: “Ikiwa mnamrudia Yehova kwa moyo wenu wote,+ ondoeni miungu ya kigeni+ na sanamu za Ashtorethi+ kutoka kati yenu, nanyi elekezeni moyo wenu kwa Yehova bila kuyumbayumba na kumtumikia yeye peke yake,+ naye atawaokoa kutoka mikononi mwa Wafilisti.”+  Kwa hiyo Waisraeli wakaondoa Mabaali na sanamu za Ashtorethi na kumtumikia Yehova peke yake.+  Kisha Samweli akasema: “Wakusanyeni Waisraeli wote Mispa,+ nami nitasali kwa Yehova kwa ajili yenu.”+  Basi wakakusanyika pamoja huko Mispa, nao wakachota maji na kuyamwaga mbele za Yehova na kufunga siku hiyo.+ Wakiwa huko wakasema: “Tumemtendea dhambi Yehova.”+ Naye Samweli akaanza kutumikia akiwa mwamuzi+ wa Waisraeli huko Mispa.  Wafilisti waliposikia kwamba Waisraeli wamekusanyika pamoja Mispa, watawala wa Wafilisti+ wakapanda kwenda kuwashambulia Waisraeli. Waisraeli waliposikia habari hizo, waliogopa kwa sababu ya Wafilisti.  Kwa hiyo Waisraeli wakamwambia Samweli: “Usiache kumwomba Yehova Mungu wetu atusaidie+ na kutuokoa kutoka mikononi mwa Wafilisti.”  Ndipo Samweli akachukua mwanakondoo anayenyonya, akamtoa kwa Yehova kuwa dhabihu nzima ya kuteketezwa;+ na Samweli akamwomba Yehova awasaidie Waisraeli, naye Yehova akamjibu.+ 10  Samweli alipokuwa akitoa dhabihu hiyo ya kuteketezwa, Wafilisti wakakaribia ili kupigana na Waisraeli. Basi siku hiyo Yehova akawaletea Wafilisti mngurumo mkubwa sana,+ Naye akawavuruga,+ wakashindwa mbele ya Waisraeli.+ 11  Ndipo wanaume wa Israeli wakatoka Mispa na kuwafuatia Wafilisti, wakawaua mpaka upande wa kusini wa Beth-kari. 12  Kisha Samweli akachukua jiwe+ na kuliweka kati ya Mispa na Yeshana, akaliita Ebenezeri,* kwa kuwa alisema: “Yehova ametusaidia mpaka sasa.”+ 13  Kwa hiyo Wafilisti wakashindwa, nao hawakuja tena katika eneo la Waisraeli;+ na mkono wa Yehova ukaendelea kuwashinda Wafilisti siku zote za Samweli.+ 14  Pia, majiji ambayo Wafilisti walikuwa wamechukua kutoka kwa Waisraeli yalirudishwa kwa Waisraeli, kuanzia Ekroni mpaka Gathi, na Waisraeli wakayakomboa maeneo yao kutoka mikononi mwa Wafilisti. Pia kukawa na amani kati ya Waisraeli na Waamori.+ 15  Samweli akaendelea kuwa mwamuzi wa Israeli maisha yake yote.+ 16  Kila mwaka alisafiri na kuzunguka Betheli,+ Gilgali,+ na Mispa,+ naye alikuwa mwamuzi wa Israeli katika maeneo hayo yote. 17  Lakini alikuwa akirudi Rama,+ kwa sababu nyumba yake ilikuwa huko, na huko pia alitumikia akiwa mwamuzi wa Israeli. Alimjengea Yehova madhabahu huko.+

Maelezo ya Chini

Au “kuomboleza mbele za.”
Maana yake “Jiwe la Msaada.”