Kitabu cha Kwanza cha Samweli 8:1-22

  • Waisraeli wataka mfalme (1-9)

  • Samweli awaonya watu (10-18)

  • Yehova akubali ombi la kutaka mfalme (19-22)

8  Samweli alipokuwa amezeeka, aliwaweka wanawe kuwa waamuzi wa Israeli.  Mwana wake wa kwanza aliitwa Yoeli, na wa pili aliitwa Abiya;+ walikuwa waamuzi huko Beer-sheba.  Lakini wanawe hawakufuata njia zake; walikuwa na mwelekeo wa kujitafutia faida isiyo ya haki,+ walipokea rushwa,+ na kupotosha haki.+  Baada ya muda wazee wote wa Waisraeli walikusanyika pamoja na kuja kumwona Samweli huko Rama.  Wakamwambia: “Tazama! Umezeeka, lakini wana wako hawatembei katika njia zako. Basi tuchagulie mfalme awe mwamuzi wetu kama mataifa mengine yote.”+  Lakini Samweli hakufurahi waliposema: “Tupe mfalme awe mwamuzi wetu.” Kwa hiyo Samweli akasali kwa Yehova,  Yehova akamwambia Samweli: “Sikiliza mambo yote ambayo watu wanakuambia; kwa maana hawajakukataa wewe, bali wamenikataa mimi nisiwe mfalme wao.+  Wanatenda kama walivyozoea kutenda tangu nilipowatoa Misri mpaka leo hii; wamekuwa wakiniacha+ na kuabudu miungu mingine,+ na hivyo ndivyo wanavyokutendea wewe pia.  Sasa wasikilize. Hata hivyo, unapaswa kuwaonya vikali; waambie mambo ambayo mfalme atakayewatawala atakuwa na haki ya kudai.” 10  Basi Samweli akawaambia maneno yote ya Yehova watu waliokuwa wakimwomba awape mfalme. 11  Akasema: “Mfalme atakayewatawala atakuwa na haki ya kudai mambo haya:+ Atawachukua wana wenu+ na kuwafanya wawe waendeshaji wa magari yake ya farasi+ na wapanda farasi wake,+ na baadhi yao watalazimika kukimbia mbele ya magari yake. 12  Naye atajichagulia wakuu wa maelfu+ na wakuu wa hamsini,+ na baadhi yao watamlimia mashamba yake,+ watavuna mazao yake,+ na kutengeneza silaha zake za vita na vifaa vya magari yake.+ 13  Atachukua mabinti wenu na kuwafanya kuwa watengenezaji wa marashi,* wapishi, na waokaji.+ 14  Atachukua mashamba yenu bora, mashamba yenu bora ya mizabibu, na mashamba yenu bora ya mizeituni+ na kuwapa watumishi wake. 15  Atachukua sehemu ya kumi ya mashamba yenu ya nafaka na mashamba yenu ya mizabibu na kuwapa maofisa wa makao yake na watumishi wake. 16  Naye atachukua watumishi wenu wa kiume na wa kike, ng’ombe wenu walio bora, na punda wenu na kuwatumia kufanya kazi zake.+ 17  Atachukua sehemu ya kumi ya kondoo wenu na mbuzi wenu,+ nanyi mtakuwa watumishi wake. 18  Siku itafika mtakapolia kwa sababu ya mfalme ambaye mlijichagulia wenyewe,+ lakini Yehova hatawajibu siku hiyo.” 19  Hata hivyo, watu wakakataa kusikiliza mambo ambayo Samweli aliwaambia, wakasema: “Hatutaki, tumeazimia kuwa na mfalme wa kututawala. 20  Kisha tutakuwa kama mataifa mengine yote, na mfalme wetu atakuwa mwamuzi wetu, atatuongoza, na kupigana vita vyetu.” 21  Baada ya Samweli kusikia maneno yote ya watu, akayarudia masikioni mwa Yehova. 22  Yehova akamwambia Samweli: “Wasikilize, na uweke mfalme wa kuwatawala.”+ Basi Samweli akawaambia Waisraeli: “Kila mmoja wenu arudi katika jiji lake.”

Maelezo ya Chini

Au “wachanganyaji wa manukato.”