Barua ya Kwanza kwa Timotheo 6:1-21

  • Watumwa wawaheshimu mabwana wao (1, 2)

  • Walimu wa uwongo na kupenda pesa (3-10)

  • Maagizo kwa ajili ya mtu wa Mungu (11-16)

  • Kuwa tajiri katika matendo mema (17-19)

  • Linda mambo uliyokabidhiwa (20, 21)

6  Acheni wale walio chini ya nira ya utumwa waendelee kuwaheshimu kikamili+ mabwana wao, ili watu wasiseme vibaya kuhusu jina la Mungu na lile fundisho.+  Pia, acheni wale walio na mabwana ambao ni waamini wasiwavunjie heshima kwa sababu wao ni ndugu zao. Badala yake, wanapaswa kuwatumikia kwa bidii zaidi, kwa sababu wale wanaonufaika na utumishi wao mzuri ni waamini wenzao wapendwa. Endelea kuwafundisha na kuwahimiza wafanye mambo haya.  Mtu yeyote akifundisha mafundisho tofauti na yanayopingana na fundisho lenye manufaa*+ linalotoka kwa Bwana wetu Yesu Kristo, au mafundisho yasiyopatana na ujitoaji-kimungu,*+  yeye anajivuna kwa kiburi na haelewi chochote.+ Pia, anapenda sana* kubishana na kushindana kuhusu maneno.+ Mambo hayo huleta wivu, mizozo, uchongezi,* na shaka zenye uovu,  mabishano ya kawaida kuhusu mambo madogo madogo ya watu waliopotoka kiakili+ na wasiojua kweli, wakifikiri ujitoaji-kimungu* ni njia ya kupata faida.+  Kwa hakika, kuna faida kubwa ya kuwa na ujitoaji-kimungu*+ na kuridhika.*  Kwa maana hatukuleta chochote ulimwenguni, wala hatuwezi kuondoka na chochote.+  Basi, tukiwa na chakula* na mavazi,* tutaridhika na vitu hivyo.+  Lakini wale ambao wameazimia kuwa matajiri huanguka kwenye majaribu, na mtego,+ na tamaa nyingi za kijinga zenye kudhuru ambazo hutumbukiza watu kwenye maangamizi na uharibifu.+ 10  Kwa maana kupenda pesa ndicho chanzo cha mambo mabaya ya kila aina, na kwa kujitahidi kufikia upendo huo, wengine wamepotoshwa kutoka kwenye imani na kujichoma kila mahali kwa maumivu mengi.+ 11  Ingawa hivyo, wewe, mtu wa Mungu, yakimbie mambo hayo. Badala yake, fuatilia uadilifu, ujitoaji-kimungu,* imani, upendo, uvumilivu, na upole.+ 12  Pigana pigano zuri la imani, ushike imara uzima wa milele ulioitiwa nawe ukatoa tangazo zuri la hadharani mbele ya mashahidi wengi. 13  Mbele za Mungu, anayevihifadhi vitu vyote hai, na Kristo Yesu, ambaye akiwa shahidi alitoa tangazo zuri la hadharani mbele ya Pontio Pilato,+ ninakuagiza 14  uishike amri katika njia safi na isiyolaumika mpaka wakati wa ufunuo wa Bwana wetu Yesu Kristo,+ 15  ambao yule Mtawala Mkuu wa pekee na mwenye furaha atauonyesha katika nyakati zake zilizowekwa. Yeye ndiye Mfalme wa wafalme na Bwana wa mabwana,+ 16  yeye peke yake asiyeweza kufa,+ anayeishi katika nuru isiyoweza kufikiwa+ na ambaye hakuna mwanadamu amemwona wala anayeweza kumwona.+ Kwake na kuwe na heshima na nguvu milele. Amina. 17  Waagize* wale walio matajiri katika mfumo wa mambo* wa sasa wasijivune* wala wasiutumaini utajiri usiotegemeka,+ bali wamtumaini Mungu, ambaye hutupatia kwa wingi vitu vyote tunavyofurahia.+ 18  Waambie watende mema, wawe matajiri katika matendo mazuri, wawe wakarimu, tayari kushiriki vitu na wengine,+ 19  wakijiwekea salama hazina ya msingi mzuri kwa ajili ya wakati ujao,+ ili waushike imara uzima ulio wa kweli.+ 20  Timotheo, linda yote uliyokabidhiwa,+ jiepushe na maneno matupu yanayochafua mambo matakatifu na pia uepuke mawazo yanayopingana ya “ujuzi” wa uwongo.+ 21  Kwa kujisifia ujuzi huo, wengine wameiacha imani. Fadhili zisizostahiliwa na ziwe pamoja nawe.

Maelezo ya Chini

Au “lenye afya; lenye faida.”
Angalia Kamusi.
Au “anapenda isivyo kawaida.”
Au “matusi.”
Angalia Kamusi.
Angalia Kamusi.
Tnn., “pamoja na ujitoshelevu.”
Au “riziki.”
Au “makao.” Tnn., “kitu cha kujifunika.”
Angalia Kamusi.
Au “wasijitakie makuu.”
Angalia Kamusi.
Au “Waamuru.”