Kitabu cha Kwanza cha Wafalme 11:1-43

  • Wake za Sulemani waugeuza moyo wake (1-13)

  • Wapinzani wa Sulemani (14-25)

  • Yeroboamu aahidiwa makabila kumi (26-40)

  • Sulemani afa; Rehoboamu awekwa kuwa mfalme (41-43)

11  Lakini mbali na binti ya Farao,+ Mfalme Sulemani aliwapenda wanawake wengi wa kigeni:+ wanawake Wamoabu,+ Waamoni,+ Waedomu, Wasidoni,+ na Wahiti.+  Walitoka katika mataifa ambayo Yehova alikuwa amewaambia hivi Waisraeli kuyahusu: “Hampaswi kuingia miongoni mwao,* nao hawapaswi kuingia miongoni mwenu; kwa maana kwa hakika wataigeuza mioyo yenu ifuate miungu yao.”+ Lakini Sulemani alishikamana nao na kuwapenda.  Naye alikuwa na wake 700 waliokuwa mabinti wa wafalme na masuria 300, na hatua kwa hatua wake zake wakaugeuza moyo wake.*  Sulemani alipozeeka,+ wake zake waliugeuza* moyo wake ukaifuata miungu mingine,+ na moyo wake haukuwa kamili kwa* Yehova Mungu wake kama moyo wa Daudi baba yake.  Na Sulemani akamfuata Ashtorethi,+ mungu wa kike wa Wasidoni, na Milkomu,+ mungu mwenye kuchukiza wa Waamoni.  Na Sulemani akatenda maovu machoni pa Yehova, naye hakumfuata Yehova kikamili kama Daudi baba yake alivyomfuata.+  Wakati huo ndipo Sulemani alipojenga mahali pa juu+ kwa ajili ya Kemoshi, mungu mwenye kuchukiza wa Moabu, kwenye mlima uliokuwa mbele ya Yerusalemu, na kwa ajili ya Moleki,+ mungu mwenye kuchukiza wa Waamoni.+  Hivyo ndivyo alivyowafanyia wake zake wote wa kigeni waliokuwa wakifukiza moshi wa dhabihu na kuitolea dhabihu miungu yao.  Yehova akamkasirikia vikali Sulemani, kwa sababu moyo wake ulikuwa umegeuka na kumwacha Yehova Mungu wa Israeli,+ aliyekuwa amemtokea mara mbili+ 10  na kumwonya kuhusu jambo hilohilo, kwamba hapaswi kuifuata miungu mingine.+ Lakini hakutii amri ya Yehova. 11  Sasa Yehova akamwambia Sulemani: “Kwa sababu umefanya jambo hili, nawe hukushika agano langu na sheria zangu nilizokuamuru, kwa hakika nitaurarua ufalme kutoka kwako, nami nitampa mmoja wa watumishi wako.+ 12  Hata hivyo, kwa ajili ya Daudi baba yako, sitafanya hivyo maishani mwako. Nitaurarua kutoka mikononi mwa mwana wako,+ 13  lakini sitaurarua ufalme wote.+ Kabila moja nitampa mwana wako,+ kwa ajili ya Daudi mtumishi wangu na kwa ajili ya Yerusalemu, jiji ambalo nimechagua.”+ 14  Ndipo Yehova akatokeza mtu wa kumpinga Sulemani,+ yaani, Hadadi Mwedomu, wa ukoo wa kifalme wa Edomu.+ 15  Daudi aliposhinda Edomu,+ Yoabu mkuu wa jeshi alipanda kwenda kuwazika waliouawa, naye akajaribu kumuua kila mwanamume huko Edomu. 16  (Kwa maana Yoabu na Waisraeli wote walikaa huko kwa miezi sita mpaka alipokuwa amemwangamiza kila mwanamume huko Edomu.) 17  Lakini Hadadi alikimbia pamoja na baadhi ya Waedomu waliokuwa watumishi wa baba yake, wakaenda Misri; wakati huo Hadadi alikuwa mvulana mdogo. 18  Basi wakaondoka Midiani na kufika Parani. Walichukua wanaume kutoka Parani+ na kwenda Misri, kwa Farao mfalme wa Misri, ambaye alimpa nyumba, akaamuru awe akipewa chakula, na pia akampa ardhi. 19  Hadadi alipata kibali machoni pa Farao, hivi kwamba akampa dada ya mke wake mwenyewe, dada ya malkia Tapenesi,* ili amwoe. 20  Baada ya muda dada ya Tapenesi akamzalia mwana, Genubathi, na Tapenesi alimlelea* katika nyumba ya Farao; Genubathi aliendelea kukaa katika nyumba ya Farao miongoni mwa wana wa Farao. 21  Hadadi akasikia akiwa Misri kwamba Daudi alikuwa amekufa na kuzikwa pamoja na mababu zake+ na kwamba Yoabu mkuu wa jeshi alikuwa amekufa.+ Basi Hadadi akamwambia Farao: “Niruhusu niende zangu, niende katika ardhi yangu mwenyewe.” 22  Lakini Farao akamuuliza: “Ni nini ulichokosa kwangu hivi kwamba unataka kwenda katika ardhi yako mwenyewe?” Hadadi akamjibu: “Sijakosa chochote, lakini tafadhali niruhusu niende zangu.” 23  Mungu akatokeza pia mtu mwingine wa kumpinga Sulemani,+ yaani, Rezoni mwana wa Eliada, aliyekuwa amemkimbia bwana wake, Hadadezeri+ mfalme wa Soba. 24  Alijikusanyia wanaume akawa kiongozi wa kundi la wavamizi wakati Daudi alipowashinda.*+ Basi wakaenda Damasko,+ wakakaa huko na kuanza kutawala huko Damasko. 25  Naye akawa mpinzani wa Waisraeli siku zote za Sulemani, kuongezea madhara yaliyosababishwa na Hadadi, naye aliwachukia sana Waisraeli alipokuwa akitawala Siria. 26  Pia kulikuwa na Yeroboamu+ mwana wa Nebati, Mwefraimu kutoka Sereda, mtumishi wa Sulemani,+ na mama yake aliyekuwa mjane aliitwa Serua. Yeye pia alianza kumwasi* mfalme.+ 27  Hii ndiyo sababu iliyomfanya amwasi mfalme: Sulemani alikuwa amejenga Kilima*+ na kuziba mwanya katika ukuta wa Jiji la Daudi baba yake.+ 28  Sasa huyu Yeroboamu alikuwa mwanamume mwenye uwezo mkubwa. Sulemani alipoona kwamba kijana huyo alikuwa mfanyakazi mwenye bidii, alimweka kuwa msimamizi+ wa utumishi wote wa lazima wa nyumba ya Yosefu. 29  Wakati huo Yeroboamu alitoka Yerusalemu, na nabii Ahiya,+ Mshilo, akamkuta njiani. Ahiya alikuwa amevaa nguo mpya, na wote wawili walikuwa peke yao shambani. 30  Ahiya akashika nguo mpya aliyokuwa amevaa na kuirarua vipande 12. 31  Kisha akamwambia Yeroboamu: “Jichukulie vipande kumi, kwa maana Yehova Mungu wa Israeli anasema hivi: ‘Tazama, ninaurarua ufalme kutoka mikononi mwa Sulemani, nami nitakupa makabila kumi.+ 32  Lakini atabaki na kabila moja+ kwa ajili ya mtumishi wangu Daudi+ na kwa ajili ya Yerusalemu, jiji ambalo nimechagua miongoni mwa makabila yote ya Israeli.+ 33  Nitafanya hivyo kwa sababu wameniacha,+ nao wanamwinamia Ashtorethi, mungu wa kike wa Wasidoni, na Kemoshi, mungu wa Moabu, na Milkomu, mungu wa Waamoni, nao hawajatembea katika njia zangu kwa kufanya yaliyo sawa machoni pangu na kushika maagizo yangu na sheria zangu* kama Daudi baba yake alivyofanya. 34  Lakini sitauchukua ufalme wote kutoka mikononi mwake, nami nitamwacha aendelee kuwa mkuu sikuzote za maisha yake, kwa ajili ya Daudi mtumishi wangu niliyemchagua,+ kwa sababu alitii amri zangu na sheria zangu. 35  Lakini nitauchukua ufalme kutoka mikononi mwa mwana wake na kukupa wewe, yaani, makabila kumi.+ 36  Nitampa mwana wake kabila moja, ili sikuzote Daudi mtumishi wangu awe na taa mbele zangu Yerusalemu,+ jiji ambalo nimejichagulia liwe mahali pa kuweka jina langu. 37  Nitakuchukua wewe, nawe utatawala kila kitu unachotamani,* nawe utakuwa mfalme wa Israeli. 38  Na ikiwa utatii mambo yote ninayokuamuru na kutembea katika njia zangu na kufanya yaliyo sawa machoni pangu kwa kutii sheria zangu na amri zangu, kama Daudi mtumishi wangu alivyofanya,+ nitakuwa pia pamoja nawe. Nitakujengea nyumba inayodumu, kama nilivyomjengea Daudi,+ nami nitakupa Israeli. 39  Nami nitauaibisha uzao wa Daudi kwa sababu ya jambo hili,+ lakini sitafanya hivyo sikuzote.’”+ 40  Basi Sulemani akajaribu kumuua Yeroboamu, lakini Yeroboamu akakimbilia Misri, kwa Mfalme Shishaki+ wa Misri,+ akaendelea kukaa Misri mpaka Sulemani alipokufa. 41  Na mambo mengine katika historia ya Sulemani, mambo yote aliyofanya na hekima yake, je, hayajaandikwa katika kitabu cha historia ya Sulemani?+ 42  Sulemani alitawala nchi yote ya Israeli kwa miaka 40 akiwa Yerusalemu. 43  Kisha Sulemani akafa na kuzikwa pamoja na mababu zake katika Jiji la Daudi baba yake; na Rehoboamu+ mwanawe akawa mfalme baada yake.

Maelezo ya Chini

Au “Hampaswi kuoana nao.”
Au “wake zake wakawa na uvutano mkubwa kwake.”
Au “waliupotosha.”
Au “haukumtumikia kikamili.”
Hakuwa malkia aliyetawala.
Au labda, “alimwachisha kunyonya.”
Tnn., “alipowaua.”
Tnn., “kuinua mkono wake dhidi ya.”
Au “Milo.” Neno la Kiebrania linalomaanisha “jaza.”
Tnn., “maamuzi yangu.”
Au “ambacho nafsi yako inatamani.”