Kitabu cha Kwanza cha Wafalme 13:1-34

  • Unabii dhidi ya madhabahu ya Betheli (1-10)

    • Madhabahu yapasuka (5)

  • Mtu wa Mungu akosa kutii (11-34)

13  Kwa neno la Yehova, mtu fulani wa Mungu+ alikuja Betheli kutoka Yuda wakati Yeroboamu alipokuwa amesimama karibu na madhabahu+ ili kufukiza moshi wa dhabihu.  Kisha kwa neno la Yehova akapaza sauti dhidi ya madhabahu hiyo na kusema: “Ee madhabahu, madhabahu! Hivi ndivyo Yehova anavyosema, ‘Tazama! Mwana anayeitwa Yosia,+ atazaliwa katika nyumba ya Daudi! Na juu yako atawatoa dhabihu makuhani wa mahali pa juu, wanaofukiza moshi wa dhabihu juu yako, naye atateketeza mifupa ya wanadamu juu yako.’”+  Akatoa ishara* siku hiyo, akisema: “Hii ndiyo ishara* ambayo Yehova ametangaza: Tazama! Madhabahu itapasuka, na majivu* yaliyo juu yake yatamwagika.”  Mara tu mfalme aliposikia neno ambalo mtu wa Mungu wa kweli alikuwa amesema dhidi ya madhabahu huko Betheli, Yeroboamu akanyoosha mkono wake kutoka kwenye madhabahu na kusema: “Mkamateni!”+ Mara moja mkono aliokuwa amemnyooshea ukakauka,* naye hakuweza kuurudisha nyuma.+  Kisha madhabahu ikapasuka na majivu yakamwagika kutoka kwenye madhabahu kulingana na ile ishara* ambayo mtu wa Mungu wa kweli alitoa kwa neno la Yehova.  Sasa mfalme akamwambia mtu wa Mungu wa kweli: “Tafadhali, niombee kibali kutoka kwa* Yehova Mungu wako, na usali kwa ajili yangu ili nirudishiwe mkono wangu.”+ Ndipo yule mtu wa Mungu wa kweli akaomba kibali kutoka kwa Yehova, na mkono wa mfalme ukarudi kama ulivyokuwa mwanzoni.  Kisha mfalme akamwambia mtu wa Mungu wa kweli: “Twende nyumbani ukale chakula, nami nitakupa zawadi.”  Lakini mtu wa Mungu wa kweli akamwambia mfalme: “Hata ukinipa nusu ya nyumba yako, siwezi kwenda pamoja nawe na kula mkate au kunywa maji mahali hapa.  Kwa maana hivi ndivyo nilivyoamriwa kwa neno la Yehova: ‘Hupaswi kula mkate wala kunywa maji, nawe hupaswi kurudi kwa kutumia njia uliyopitia ulipokuja hapa.’” 10  Basi akaondoka kupitia njia nyingine, naye hakurudi kwa kutumia njia aliyopitia alipokuja Betheli. 11  Kulikuwa na nabii fulani mzee aliyekaa Betheli, wanawe wakaja nyumbani na kumsimulia mambo yote ambayo mtu wa Mungu wa kweli alikuwa amefanya siku hiyo kule Betheli na maneno aliyomwambia mfalme. Baada ya kumsimulia baba yao mambo hayo, 12  baba yao akawauliza: “Alipitia njia gani?” Kwa hiyo wanawe wakamwonyesha njia aliyopitia mtu huyo wa Mungu wa kweli aliyetoka Yuda. 13  Sasa akawaambia wanawe: “Niwekeeni matandiko juu ya punda.” Basi wakamwekea matandiko juu ya punda, naye akapanda juu yake. 14  Akamfuata mtu wa Mungu wa kweli na kumkuta ameketi chini ya mti mkubwa. Kisha akamuuliza: “Je, wewe ndiye yule mtu wa Mungu wa kweli aliyetoka Yuda?”+ Akajibu: “Ni mimi.” 15  Akamwambia: “Twende nyumbani ukale mkate.” 16  Lakini akasema: “Siwezi kurudi pamoja nawe wala kukubali mwaliko wako, nami siwezi kula mkate wala kunywa maji pamoja nawe mahali hapa. 17  Kwa maana niliambiwa kwa neno la Yehova, ‘Hupaswi kula mkate wala kunywa maji huko. Hupaswi kurudi kupitia njia uliyotumia kuja.’” 18  Ndipo akamwambia: “Mimi pia ni nabii kama wewe, na malaika aliniambia hivi kwa neno la Yehova: ‘Mwambie arudi pamoja nawe nyumbani kwako ili ale mkate na kunywa maji.’” (Alimdanganya.) 19  Basi akarudi pamoja naye ili ale mkate na kunywa maji nyumbani kwake. 20  Walipokuwa wameketi mezani, neno la Yehova likamjia nabii aliyekuwa amemrudisha, 21  naye akamwambia kwa sauti yule mtu wa Mungu wa kweli aliyetoka Yuda: “Yehova anasema hivi: ‘Kwa sababu uliasi agizo la Yehova, nawe hukushika amri ambayo Yehova Mungu wako alikupa, 22  lakini ulirudi kula mkate na kunywa maji mahali ambapo uliambiwa, “Usile mkate wala kunywa maji,” maiti yako haitazikwa katika makaburi ya mababu zako.’”+ 23  Baada ya mtu wa Mungu wa kweli kula mkate na kunywa maji, nabii mzee akaweka matandiko juu ya punda kwa ajili ya nabii aliyekuwa amemrudisha. 24  Kisha akaenda zake, lakini simba akakutana naye barabarani na kumuua.+ Maiti yake ikatupwa barabarani, na punda akasimama kando yake; simba pia alikuwa amesimama kando ya maiti hiyo. 25  Watu waliokuwa wakipita hapo waliona maiti hiyo ikiwa imetupwa barabarani na simba akiwa amesimama kando yake. Wakaenda na kusimulia habari hizo katika jiji ambamo yule nabii mzee alikuwa akiishi. 26  Nabii huyo aliyekuwa amemrudisha njiani aliposikia habari hizo, mara moja akasema: “Ni yule mtu wa Mungu wa kweli aliyeasi agizo la Yehova;+ kwa hiyo Yehova alimkabidhi kwa simba, amrarue na kumuua, kulingana na neno la Yehova alilokuwa amemwambia.”+ 27  Kisha akawaambia hivi wanawe: “Niwekeeni matandiko juu ya punda.” Basi wakaweka matandiko juu yake. 28  Halafu akaenda zake na kuikuta ile maiti imetupwa barabarani, punda na simba wakiwa wamesimama kando ya maiti hiyo. Simba hakuwa ameila maiti, wala hakuwa amemrarua punda. 29  Nabii huyo mzee akaibeba maiti ya mtu wa Mungu wa kweli na kuiweka juu ya punda, akairudisha katika jiji lake mwenyewe ili kumwombolezea na kumzika. 30  Basi akailaza maiti hiyo katika kaburi lake mwenyewe, nao wakaendelea kumlilia kwa sauti wakisema: “Ole wako, ndugu yangu!” 31  Baada ya kumzika, akawaambia wanawe: “Nitakapokufa, nizikeni mahali ambapo mtu wa Mungu wa kweli amezikwa. Ilazeni mifupa yangu kando ya mifupa yake.+ 32  Neno la Yehova alilokuwa ametangaza dhidi ya madhabahu iliyoko Betheli na dhidi ya nyumba zote za ibada zilizo mahali pa juu+ katika majiji ya Samaria hakika litatimia.”+ 33  Hata baada ya mambo hayo kutendeka, Yeroboamu hakuacha njia yake mbaya, lakini aliendelea kuchagua makuhani kutoka miongoni mwa watu wa kawaida ili wahudumu mahali pa juu.+ Alimweka kuwa kuhani* mtu yeyote aliyetaka kuwa kuhani, akisema: “Na awe mmoja wa makuhani wa mahali pa juu.”+ 34  Dhambi hiyo ya nyumba ya Yeroboamu+ ilisababisha waharibiwe na kuangamizwa kutoka duniani.+

Maelezo ya Chini

Au “alama.”
Au “alama.”
Au “majivu yenye mafuta,” yaani, majivu yaliyojaa mafuta ya dhabihu.
Au “ukapooza.”
Au “alama.”
Au “utulize uso wa.”
Tnn., “Aliujaza mkono wa.”