Kitabu cha Kwanza cha Wafalme 15:1-34

  • Abiyamu, mfalme wa Yuda (1-8)

  • Asa, mfalme wa Yuda (9-24)

  • Nadabu, mfalme wa Israeli (25-32)

  • Baasha, mfalme wa Israeli (33, 34)

15  Katika mwaka wa 18 wa utawala wa Mfalme Yeroboamu+ mwana wa Nebati, Abiyamu akawa mfalme wa Yuda.+  Alitawala kwa miaka mitatu huko Yerusalemu. Mama yake aliitwa Maaka,+ mjukuu wa Abishalomu.  Aliendelea kutembea katika dhambi zote ambazo baba yake alitenda kabla yake, na moyo wake haukuwa kamili kwa* Yehova Mungu wake kama moyo wa Daudi babu yake.  Hata hivyo, kwa sababu ya Daudi,+ Yehova Mungu wake alimpa taa huko Yerusalemu+ kwa kumwinua mwana wake atawale baada yake na kufanya jiji la Yerusalemu lidumu.  Kwa maana Daudi alitenda yaliyokuwa sawa machoni pa Yehova, naye hakugeuka na kuacha jambo lolote ambalo Yeye alikuwa amemwamuru sikuzote za maisha yake, isipokuwa kuhusiana na kisa cha Uria, Mhiti.+  Na kulikuwa na vita kati ya Rehoboamu na Yeroboamu sikuzote za maisha yake.+  Na mambo mengine katika historia ya Abiyamu, mambo yote aliyofanya, je, hayajaandikwa katika kitabu cha historia ya nyakati za wafalme wa Yuda?+ Kulikuwa pia na vita kati ya Abiyamu na Yeroboamu.+  Kisha Abiyamu akafa na kuzikwa pamoja na mababu zake katika Jiji la Daudi; na Asa mwanawe+ akawa mfalme baada yake.+  Katika mwaka wa 20 wa Mfalme Yeroboamu wa Israeli, Asa alianza kutawala Yuda. 10  Alitawala Yerusalemu kwa miaka 41. Nyanya yake aliitwa Maaka,+ mjukuu wa Abishalomu. 11  Asa alitenda yaliyokuwa sawa machoni pa Yehova,+ kama Daudi babu yake. 12  Aliwafukuza wanaume makahaba wa hekaluni kutoka nchini+ na kuondoa sanamu zote zenye kuchukiza* ambazo mababu zake walikuwa wametengeneza.+ 13  Hata alimwondoa Maaka+ nyanya yake kutoka katika cheo chake cha mama malkia, kwa sababu alikuwa ametengeneza sanamu chafu sana* kwa ajili ya ibada ya mti mtakatifu.* Asa akaikatakata sanamu hiyo chafu sana+ na kuiteketeza katika Bonde la Kidroni.+ 14  Lakini mahali pa juu hapakuondolewa.+ Hata hivyo, moyo wa Asa ulikuwa kamili kwa* Yehova maisha yake yote.* 15  Naye alileta katika nyumba ya Yehova vitu ambavyo yeye na baba yake walikuwa wamevifanya kuwa vitakatifu—fedha, dhahabu, na vyombo mbalimbali.+ 16  Kulikuwa na vita daima kati ya Asa na Baasha+ mfalme wa Israeli. 17  Basi Mfalme Baasha wa Israeli alikuja kushambulia Yuda, akaanza kujenga* Rama+ ili kumzuia mtu yeyote asitoke wala kuingia kwa* Mfalme Asa wa Yuda.+ 18  Ndipo Asa akachukua fedha yote na dhahabu iliyokuwa imebaki katika hazina za nyumba ya Yehova na hazina za nyumba ya* mfalme na kuwapa watumishi wake. Kisha Mfalme Asa akawatuma kwa Ben-hadadi mwana wa Tabrimoni mwana wa Hezioni, mfalme wa Siria,+ aliyekuwa akiishi Damasko, akamwambia: 19  “Kuna mkataba* kati yangu na wewe na kati ya baba yangu na baba yako. Ninakutumia zawadi ya fedha na dhahabu. Njoo, vunja mkataba wako* na Mfalme Baasha wa Israeli, ili aondoke kwangu.” 20  Ben-hadadi akamsikiliza Mfalme Asa, akawatuma wakuu wa majeshi yake kushambulia majiji ya Israeli, wakashinda Iyoni,+ Dani,+ Abel-beth-maaka, eneo lote la Kinerethi, na nchi yote ya Naftali. 21  Baasha aliposikia habari hizo, mara moja akaacha kujenga* Rama, akaendelea kuishi Tirsa.+ 22  Kisha Mfalme Asa akawaita watu wote wa Yuda—hakuna aliyeachwa—nao wakabeba mawe na mbao zilizokuwa zikitumiwa na Baasha kujenga Rama, Mfalme Asa akazitumia kujenga* Geba+ kule Benjamini, na pia Mispa.+ 23  Na mambo mengine katika historia ya Asa, ukuu wake wote na mambo yote aliyofanya na majiji aliyojenga,* je, hayajaandikwa katika kitabu cha historia ya nyakati za wafalme wa Yuda? Lakini alipozeeka alishikwa na ugonjwa miguuni.+ 24  Kisha Asa akafa na kuzikwa pamoja na mababu zake katika Jiji la Daudi babu yake; na Yehoshafati+ mwanawe akawa mfalme baada yake. 25  Nadabu+ mwana wa Yeroboamu akawa mfalme wa Israeli katika mwaka wa pili wa Mfalme Asa wa Yuda, naye alitawala Israeli kwa miaka miwili. 26  Aliendelea kutenda maovu machoni pa Yehova na kufuata njia ya baba yake+ na dhambi yake aliyosababisha Waisraeli kutenda.+ 27  Baasha mwana wa Ahiya wa nyumba ya Isakari akapanga njama dhidi yake, na Baasha akamuua kule Gibethoni,+ jiji la Wafilisti, wakati Nadabu na Waisraeli wote walipokuwa wakilizingira Gibethoni. 28  Kwa hiyo Baasha akamuua katika mwaka wa tatu wa Mfalme Asa wa Yuda, akawa mfalme baada yake. 29  Mara tu alipokuwa mfalme, aliiangamiza nyumba yote ya Yeroboamu. Hakumwacha mtu yeyote wa Yeroboamu akipumua; aliagiza waangamizwe kama Yehova alivyokuwa amesema kupitia Ahiya, mtumishi wake kutoka Shilo.+ 30  Alifanya hivyo kwa sababu ya dhambi ambazo Yeroboamu alikuwa ametenda na kusababisha Waisraeli wazitende na kwa sababu alikuwa amemkasirisha sana Yehova Mungu wa Israeli. 31  Na mambo mengine katika historia ya Nadabu, mambo yote aliyofanya, je, hayajaandikwa katika kitabu cha historia ya nyakati za wafalme wa Israeli? 32  Na kulikuwa na vita daima kati ya Asa na Mfalme Baasha wa Israeli.+ 33  Katika mwaka wa tatu wa Mfalme Asa wa Yuda, Baasha mwana wa Ahiya akawa mfalme wa Waisraeli wote kule Tirsa, alitawala kwa miaka 24.+ 34  Lakini aliendelea kutenda maovu machoni pa Yehova,+ akafuata njia ya Yeroboamu na dhambi yake ambayo alisababisha Waisraeli kutenda.+

Maelezo ya Chini

Au “haukumtumikia kikamili.”
Huenda neno la Kiebrania linahusiana na neno “mavi,” nalo hutumiwa kuonyesha dharau.
Yaani, kingono.
Angalia Kamusi.
Au “ulimtumikia kikamili.”
Tnn., “siku zake zote.”
Au “kuimarisha; kujenga upya.”
Au “asiondoke wala kuingia katika eneo la.”
Au “jumba la.”
Au “agano.”
Au “agano lako.”
Au “kuimarisha; kujenga upya.”
Au “kuimarisha; kujenga upya.”
Au “aliyoimarisha; aliyojenga upya.”