Kitabu cha Kwanza cha Wafalme 17:1-24

  • Nabii Eliya atabiri ukame (1)

  • Eliya alishwa na kunguru (2-7)

  • Eliya amtembelea mjane kule Sarefathi (8-16)

  • Mwana wa mjane afa na kufufuliwa (17-24)

17  Sasa Eliya*+ Mtishbi, mkaaji wa Gileadi,+ alimwambia hivi Ahabu: “Kwa hakika kama anavyoishi Yehova Mungu wa Israeli ninayemtumikia,* katika miaka hii hakutakuwa na umande wala mvua isipokuwa kwa neno langu!”+  Neno hili la Yehova likamjia:  “Ondoka hapa, ugeuke kwenda upande wa mashariki, ujifiche katika Bonde* la Kerithi, upande wa mashariki wa Yordani.  Utakunywa maji kutoka katika kijito, nami nitawaamuru kunguru wakuletee chakula huko.”+  Akaenda mara moja na kutenda kulingana na neno la Yehova; alienda kukaa katika Bonde* la Kerithi, upande wa mashariki wa Yordani.  Na kunguru walikuwa wakimletea mkate na nyama asubuhi na mkate na nyama jioni, naye alikunywa maji kutoka katika kile kijito.+  Lakini baada ya siku kadhaa, kijito hicho kikakauka+ kwa sababu mvua haikunyesha nchini.  Basi neno hili la Yehova likamjia:  “Ondoka, nenda Sarefathi ya Sidoni, nawe ukae huko. Tazama! Nitamwamuru mjane fulani huko akupe chakula.”+ 10  Basi akainuka na kwenda Sarefathi. Alipofika kwenye lango la jiji, kulikuwa na mwanamke fulani mjane aliyekuwa akiokota kuni. Basi akamwita mwanamke huyo na kumwambia: “Tafadhali, niletee maji kidogo kwenye kikombe ninywe.”+ 11  Alipokuwa akienda kuyaleta, Eliya akamwita na kumwambia: “Tafadhali, niletee kipande cha mkate.” 12  Ndipo mwanamke huyo akasema: “Kwa hakika kama Yehova Mungu wako anavyoishi, sina mkate, nina konzi moja tu ya unga katika mtungi mkubwa na mafuta kidogo katika mtungi mdogo.+ Sasa ninaokota kuni chache tu, kisha niende nyumbani na kupika chakula kidogo kwa ajili yangu na mwanangu. Baada ya kula chakula hicho, tutakufa.” 13  Kisha Eliya akamwambia: “Usiogope. Nenda nyumbani ufanye kama ulivyosema. Lakini kwanza nitayarishie mkate mdogo wa mviringo kwa unga na mafuta uliyo nayo. Kisha unaweza kutayarisha chochote baadaye kwa ajili yako na mwanao. 14  Kwa maana Yehova Mungu wa Israeli anasema hivi: ‘Unga ulio katika huo mtungi mkubwa hautakwisha, na mafuta yaliyo katika huo mtungi mdogo hayatakwisha mpaka siku ambayo Yehova ataleta mvua nchini.’”+ 15  Basi akaenda na kufanya kama Eliya alivyosema; mwanamke huyo pamoja na Eliya na familia ya mwanamke huyo wakawa na chakula kwa siku nyingi.+ 16  Unga uliokuwa katika mtungi huo mkubwa haukwisha, na mafuta yaliyokuwa katika mtungi ule mdogo hayakwisha, kama Yehova alivyokuwa amesema kupitia Eliya. 17  Baada ya mambo hayo, mwana wa mwanamke huyo mwenye nyumba akawa mgonjwa, na hali yake ikawa mbaya sana hivi kwamba akakata pumzi.+ 18  Ndipo mwanamke huyo akamuuliza Eliya: “Nimekukosea nini, ewe mtu wa Mungu wa kweli? Je, umekuja kunikumbusha hatia yangu na kumuua mwanangu?”+ 19  Lakini Eliya akamwambia: “Nipe mwana wako.” Kisha akamchukua kutoka mikononi mwake, akambeba hadi katika chumba cha darini, alimokuwa akikaa, akamlaza kwenye kitanda chake mwenyewe.+ 20  Akamlilia Yehova kwa sauti akisema: “Ee Yehova Mungu wangu,+ je, unamdhuru pia mjane ninayekaa kwake kwa kumuua mwanawe?” 21  Kisha akajinyoosha juu ya mtoto huyo mara tatu na kumlilia Yehova kwa sauti akisema: “Ee Yehova Mungu wangu, tafadhali, acha uhai wa mtoto huyu umrudie.” 22  Yehova akasikiliza ombi la Eliya,+ na uhai wa mtoto huyo ukamrudia, akawa hai tena.+ 23  Eliya akamchukua mtoto huyo, akamleta chini kutoka katika kile chumba cha darini, akampa mama yake; Eliya akasema: “Tazama, mwana wako yuko hai.”+ 24  Ndipo mwanamke huyo akamwambia Eliya: “Sasa ninajua kwamba kwa kweli wewe ni mtu wa Mungu+ na kwamba neno la Yehova kutoka kinywani mwako ni kweli.”

Maelezo ya Chini

Maana yake “Mungu Wangu Ni Yehova.”
Tnn., “ninayesimama mbele zake.”
Au “Korongo.”
Au “Korongo.”