Kitabu cha Kwanza cha Wafalme 18:1-46

  • Eliya akutana na Obadia na Ahabu (1-18)

  • Eliya apambana na manabii wa Baali kule Karmeli (19-40)

    • “Kuyumbayumba kati ya maoni mawili” (21)

  • Ukame wa miaka mitatu na nusu waisha (41-46)

18  Baada ya muda fulani, katika mwaka wa tatu,+ neno la Yehova likamjia Eliya likisema: “Nenda ukamwone Ahabu, nami nitaleta mvua nchini.”+  Basi Eliya akaenda kumwona Ahabu, wakati huo kulikuwa na njaa kali sana+ Samaria.  Wakati huo, Ahabu akamwita Obadia, aliyekuwa msimamizi wa nyumba yake. (Obadia alimwogopa sana Yehova,  na Yezebeli+ alipokuwa akiwaua manabii wa Yehova, Obadia aliwachukua manabii 100 na kuwaficha katika mapango mawili, manabii 50 katika kila pango, naye alikuwa akiwapa mikate na maji.)  Kisha Ahabu akamwambia Obadia: “Pita kotekote nchini kwenye chemchemi zote za maji na mabonde* yote. Huenda tukapata majani ya kutosha ili farasi na nyumbu waendelee kuishi, wanyama wetu wote wasife.”  Kwa hiyo wakagawana maeneo ya nchi ambako wangeenda kutafuta nyasi. Ahabu akaenda peke yake upande mmoja, na Obadia akaenda peke yake upande mwingine.  Obadia alipokuwa akienda zake, akakutana na Eliya. Mara moja Obadia akamtambua, akaanguka chini kifudifudi na kumuuliza: “Je, ni wewe, bwana wangu Eliya?”+  Akamjibu: “Ni mimi. Nenda ukamwambie bwana wako, ‘Eliya yuko hapa.’”  Lakini akasema: “Nimetenda dhambi gani hivi kwamba unanitia mimi mtumishi wako mikononi mwa Ahabu ili aniue? 10  Kwa hakika kama Yehova Mungu wako anavyoishi, hakuna taifa wala ufalme ambamo bwana wangu hakuwatuma watu wakutafute. Waliposema, ‘Hayuko hapa,’ aliagiza ufalme na taifa hilo liape kwamba limeshindwa kukupata.+ 11  Sasa unasema, ‘Nenda ukamwambie bwana wako: “Eliya yuko hapa.”’ 12  Nitakapokuacha, roho ya Yehova itakubeba na kukupeleka+ mahali ambapo sitajua, nami nikimwambia Ahabu naye asikupate, kwa hakika ataniua. Lakini mimi mtumishi wako nimemwogopa Yehova tangu nilipokuwa kijana. 13  Je, bwana wangu hukuambiwa niliyofanya Yezebeli alipokuwa akiwaua manabii wa Yehova, jinsi nilivyowaficha manabii 100 wa Yehova, manabii 50 katika kila pango, na jinsi nilivyokuwa nikiwapa mikate na maji?+ 14  Lakini sasa unasema, ‘Nenda ukamwambie bwana wako: “Eliya yuko hapa.”’ Hakika ataniua.” 15  Hata hivyo, Eliya akamwambia: “Kwa hakika kama anavyoishi Yehova wa majeshi ninayemtumikia,* nitaenda kumwona leo.” 16  Basi Obadia akaenda kukutana na Ahabu na kumwambia habari hizo, kisha Ahabu akaenda kukutana na Eliya. 17  Mara tu Ahabu alipomwona Eliya akamwambia: “Kumbe ni wewe unayeiletea Israeli taabu kubwa!”* 18  Eliya akasema: “Sijailetea Israeli taabu, lakini ni wewe na nyumba ya baba yako mliofanya hivyo kwa kuziacha amri za Yehova na kufuata Mabaali.+ 19  Na sasa nikusanyie Waisraeli wote kwenye Mlima Karmeli,+ pamoja na manabii 450 wa Baali na manabii 400 wa mti mtakatifu,*+ wanaokula kwenye meza ya Yezebeli.” 20  Basi Ahabu akatuma ujumbe kwa Waisraeli wote, akawakusanya pamoja manabii kwenye Mlima Karmeli. 21  Kisha Eliya akawakaribia watu wote na kusema: “Mtaendelea kuyumbayumba kati ya maoni mawili tofauti*+ mpaka wakati gani? Ikiwa Yehova ndiye Mungu wa kweli, mfuateni;+ lakini ikiwa ni Baali, mfuateni!” Hata hivyo, watu hawakumjibu neno lolote. 22  Ndipo Eliya akawaambia watu: “Mimi peke yangu ndiye nabii wa Yehova aliyebaki,+ lakini manabii wa Baali ni 450. 23  Na watupatie ng’ombe dume wachanga wawili, kisha wachague ng’ombe dume mmoja mchanga na kumkata vipandevipande na kuviweka juu ya kuni, lakini wasiwashe moto. Nitamtayarisha ng’ombe dume mchanga wa pili na kumweka juu ya kuni, lakini sitawasha moto. 24  Kisha mtaliita jina la mungu wenu,+ nami nitaliita jina la Yehova. Mungu atakayejibu kwa moto, atathibitisha kwamba yeye ndiye Mungu wa kweli.”+ Ndipo watu wote wakasema: “Jambo unalosema ni jema.” 25  Sasa Eliya akawaambia manabii wa Baali: “Chagueni ng’ombe dume mmoja mchanga na kumtayarisha kwanza, kwa sababu ninyi ni wengi. Kisha mliite jina la mungu wenu, lakini msiwashe moto.” 26  Basi wakamchukua huyo ng’ombe dume mchanga waliyepewa, wakamtayarisha, na kuendelea kuliita jina la Baali kuanzia asubuhi mpaka adhuhuri, wakisema: “Ee Baali, tujibu!” Lakini hapakuwa na sauti yoyote, wala yeyote aliyewajibu.+ Nao wakazidi kurukaruka kuizunguka madhabahu waliyokuwa wametengeneza. 27  Karibu wakati wa adhuhuri Eliya akaanza kuwadhihaki na kusema: “Iteni kwa sauti yenu yote! Je, si yeye ni mungu?+ Labda amezama katika mawazo au ameenda chooni.* Au pengine amelala usingizi na mtu fulani anahitaji kumwamsha!” 28  Walikuwa wakiita kwa sauti yao yote na kujikatakata kwa visu na mikuki, kulingana na desturi yao, mpaka walipotokwa na damu nyingi mwili mzima. 29  Wakati wa adhuhuri ukapita lakini wakaendelea kutenda kiwazimu* mpaka jioni wakati ambapo toleo la nafaka hutolewa, lakini hapakuwa na sauti yoyote wala yeyote aliyejibu; hakuna aliyewasikiliza.+ 30  Hatimaye Eliya akawaambia watu wote: “Nikaribieni.” Basi watu wote wakamkaribia. Kisha akairekebisha madhabahu ya Yehova iliyokuwa imebomolewa.+ 31  Halafu Eliya akachukua mawe 12, kulingana na idadi ya makabila ya wana wa Yakobo, ambaye neno la Yehova lilikuwa limemjia likisema: “Jina lako litakuwa Israeli.”+ 32  Akatumia mawe hayo kujenga madhabahu+ katika jina la Yehova. Kisha akachimba mtaro kuzunguka madhabahu hiyo, eneo kubwa ambalo lilitosha kupandwa sea mbili* za mbegu. 33  Kisha akapanga kuni, akamkata yule ng’ombe dume mchanga vipandevipande na kuviweka juu ya hizo kuni.+ Halafu akasema: “Ijazeni maji mitungi mikubwa minne, myamwage juu ya dhabihu ya kuteketezwa na juu ya kuni.” 34  Kisha akasema: “Fanyeni hivyo tena.” Basi wakafanya hivyo tena. Akasema tena: “Fanyeni hivyo mara ya tatu.” Basi wakafanya hivyo mara ya tatu. 35  Maji yakajaa kuizunguka madhabahu, na pia akaujaza mtaro maji. 36  Karibu wakati wa kutoa toleo la nafaka la jioni,+ nabii Eliya akaja mbele na kusema: “Ee Yehova, Mungu wa Abrahamu,+ Isaka,+ na Israeli, acha leo ijulikane kwamba wewe ni Mungu katika Israeli na kwamba mimi ni mtumishi wako na kwamba nimefanya mambo haya yote kwa neno lako.+ 37  Nijibu, Ee Yehova! Nijibu ili watu hawa wajue kwamba wewe, Yehova, ndiye Mungu wa kweli na kwamba wewe unaigeuza mioyo yao ikurudie.”+ 38  Ndipo moto wa Yehova ukashuka kutoka juu, ukaiteketeza hiyo dhabihu ya kuteketezwa,+ kuni, mawe, na mavumbi, nao ukayaramba maji yaliyokuwa mtaroni.+ 39  Watu wote walipoona jambo hilo, mara moja wakaanguka chini kifudifudi na kusema: “Yehova ndiye Mungu wa kweli! Yehova ndiye Mungu wa kweli!” 40  Kisha Eliya akawaambia: “Wakamateni manabii wa Baali! Msimwache hata mmoja wao atoroke!” Mara moja wakawakamata, na Eliya akawaleta chini kwenye kijito cha* Kishoni+ na kuwachinja huko.+ 41  Sasa Eliya akamwambia Ahabu: “Panda juu, ukale na kunywa, kwa maana kuna sauti ya mvua kubwa sana.”+ 42  Basi Ahabu akapanda juu kwenda kula na kunywa, lakini Eliya akapanda kwenye kilele cha Karmeli, akajikunyata ardhini, uso wake ukiwa katikati ya magoti yake.+ 43  Kisha akamwambia mtumishi wake: “Panda juu, tafadhali, utazame upande wa bahari.” Basi akapanda juu, akatazama na kusema: “Hakuna kitu chochote.” Eliya akamwambia mara saba, “Rudi.” 44  Mara ya saba mtumishi wake akamwambia: “Tazama! Kuna wingu dogo kama mkono wa mwanadamu linalopanda kutoka baharini.” Ndipo Eliya akasema: “Nenda, mwambie hivi Ahabu: ‘Funga farasi kwenye gari! Teremka ili mvua kubwa isikuzuie!’” 45  Wakati huo, mawingu mazito yakatanda angani, upepo ukavuma, na mvua kubwa sana ikanyesha;+ naye Ahabu akaendesha gari mpaka Yezreeli.+ 46  Lakini mkono wa Yehova ukaja juu ya Eliya, akajifunga vazi lake kiunoni, akakimbia na kumpita Ahabu na kutangulia kufika Yezreeli.

Maelezo ya Chini

Au “makorongo.”
Tnn., “ninayesimama mbele zake.”
Au “unayesababisha Israeli itengwe.”
Angalia Kamusi.
Au “kuchechemea kwa kutumia magongo mawili.”
Au labda, “amesafiri.”
Au “kama manabii.”
Sea moja ilikuwa sawa na lita 7.33 (vibaba 6.66). Angalia Nyongeza B14.
Au “korongo la.”