Kitabu cha Kwanza cha Wafalme 19:1-21

  • Eliya akimbia ghadhabu ya Yezebeli (1-8)

  • Yehova amtokea Eliya kule Horebu (9-14)

  • Eliya aambiwa amtie mafuta Hazaeli, Yehu, Elisha (15-18)

  • Elisha awekwa rasmi kuchukua nafasi ya Eliya (19-21)

19  Kisha Ahabu+ akamwambia Yezebeli+ mambo yote ambayo Eliya alikuwa amefanya na jinsi alivyowaua manabii wote kwa upanga.+  Ndipo Yezebeli akamtuma mjumbe kwa Eliya, akisema: “Miungu na iniadhibu, tena vikali, ikiwa kufikia kesho wakati kama huu sitakufanya uwe kama* kila mmoja wa manabii hao!”  Basi Eliya akaogopa, akaondoka na kukimbia ili kuokoa uhai wake.*+ Akafika Beer-sheba,+ jiji la Yuda,+ akamwacha mtumishi wake huko.  Akaingia nyikani safari ya siku moja, akafika na kuketi chini ya mti wa mretemu, naye akaomba afe. Akasema: “Imetosha! Sasa, Ee Yehova, niue,*+ kwa sababu mimi si bora kuliko mababu zangu.”  Kisha akalala chini na kushikwa na usingizi chini ya mti huo wa mretemu. Lakini kwa ghafla malaika akamgusa+ na kumwambia: “Amka, ule.”+  Alipoangalia, aliona karibu na kichwa chake mkate wa mviringo ukiwa juu ya mawe yenye moto na pia gudulia la maji. Akala na kunywa na kulala chini tena.  Baadaye malaika wa Yehova akarudi mara ya pili, akamgusa na kusema: “Amka, ule, kwa maana safari itakuwa ngumu sana kwako.”  Basi akaamka, akala na kunywa, na kwa nguvu za chakula hicho akasafiri kwa siku 40, mchana na usiku, mpaka alipofika Horebu, mlima wa Mungu wa kweli.+  Huko akaingia pangoni+ na kulala humo usiku; na tazama! neno la Yehova likamjia na kumuuliza: “Unafanya nini hapa, Eliya?” 10  Akajibu: “Nimekuwa na bidii kwelikweli kwa ajili ya Yehova Mungu wa majeshi;+ kwa maana Waisraeli wameliacha agano lako,+ wamebomoa madhabahu zako, na kuwaua manabii wako kwa upanga,+ nimebaki mimi peke yangu. Sasa wanataka kuniua.”*+ 11  Lakini Akasema: “Toka nje, ukasimame mlimani mbele za Yehova.” Na tazama! Yehova alikuwa akipita karibu,+ na upepo mkali na wenye nguvu ulikuwa ukipasua milima na kuvunja miamba mbele za Yehova,+ lakini Yehova hakuwa katika upepo huo. Baada ya upepo, kukawa na tetemeko la ardhi,+ lakini Yehova hakuwa katika tetemeko hilo. 12  Baada ya tetemeko la ardhi, kukawa na moto,+ lakini Yehova hakuwa katika moto huo. Baada ya moto, kukawa na sauti tulivu, ya chini.+ 13  Mara tu Eliya alipoisikia, aliufunika uso wake kwa vazi lake rasmi,+ akatoka nje na kusimama kwenye mlango wa pango. Kisha sauti ikamuuliza: “Unafanya nini hapa, Eliya?” 14  Akasema: “Nimekuwa na bidii kwelikweli kwa ajili ya Yehova Mungu wa majeshi; kwa maana Waisraeli wameliacha agano lako,+ wamebomoa madhabahu zako, na kuwaua manabii wako kwa upanga, nimebaki mimi peke yangu. Sasa wanataka kuniua.”*+ 15  Yehova akamwambia: “Rudi, nenda katika nyika ya Damasko. Utakapofika huko, mtie mafuta Hazaeli+ awe mfalme wa Siria. 16  Pia unapaswa kumtia mafuta Yehu+ mjukuu wa Nimshi awe mfalme wa Israeli, na umtie mafuta Elisha mwana wa Shafati kutoka Abel-mehola awe nabii baada yako.+ 17  Mtu yeyote atakayeponyoka upanga wa Hazaeli,+ Yehu atamuua;+ na yeyote atakayeponyoka upanga wa Yehu, Elisha atamuua.+ 18  Na bado nina watu 7,000 waliobaki Israeli,+ watu wote ambao hawakumpigia magoti Baali,+ na ambao hawakumbusu kwa midomo yao.”+ 19  Basi akaondoka huko, akamkuta Elisha mwana wa Shafati akilima kwa jozi 12 za ng’ombe dume, naye alikuwa na jozi ya 12. Basi Eliya akamkaribia, akalitupa vazi lake rasmi+ juu yake. 20  Ndipo akawaacha wale ng’ombe dume, akamfuata Eliya mbio na kusema: “Tafadhali, niruhusu nimbusu baba yangu na mama yangu. Kisha nitakufuata.” Eliya akamwambia: “Nenda, rudi nyumbani, nimekuzuia kwa njia gani?” 21  Basi akarudi, akachukua jozi moja ya ng’ombe dume na kuwatoa dhabihu, naye akatumia vifaa vya kulimia kuchemsha nyama ya ng’ombe dume hao, kisha akawapa watu, nao wakala. Baada ya hapo akaondoka na kumfuata Eliya na kuanza kumhudumia.+

Maelezo ya Chini

Au “sitafanya nafsi yako iwe kama nafsi ya.”
Au “nafsi yake.”
Au “iondoe nafsi yangu.”
Au “kuiondoa nafsi yangu.”
Au “kuiondoa nafsi yangu.”