Kitabu cha Kwanza cha Wafalme 2:1-46

  • Daudi ampa maagizo Sulemani (1-9)

  • Daudi afa; Sulemani aketi kwenye kiti cha ufalme (10-12)

  • Njama ya Adoniya yasababisha auawe (13-25)

  • Abiathari afukuzwa; Yoabu auawa (26-35)

  • Shimei auawa (36-46)

2  Daudi alipokaribia kufa, alimpa Sulemani mwanawe maagizo haya:  “Nakaribia kufa.* Kwa hiyo, uwe imara+ na ujithibitishe kuwa mwanamume.+  Ni lazima utimize wajibu wako kwa Yehova Mungu wako kwa kutembea katika njia zake na kushika maagizo yake, amri zake, sheria zake,* na vikumbusho vyake kama vilivyoandikwa katika Sheria ya Musa;+ ndipo utakapofanikiwa* katika kila jambo unalofanya na kila mahali unapogeuka kwenda.  Na Yehova atatimiza ahadi aliyotoa kunihusu aliposema hivi: ‘Ikiwa wana wako wataikazia uangalifu njia yao kwa kutembea kwa uaminifu mbele zangu kwa moyo wao wote na kwa nafsi* yao yote,+ hutakosa kamwe mwanamume wa uzao wako atakayeketi kwenye kiti cha ufalme cha Israeli.’+  “Pia unajua vizuri jambo ambalo Yoabu mwana wa Seruya alinitendea, jambo alilowatendea wakuu wawili wa majeshi ya Israeli, Abneri+ mwana wa Neri na Amasa+ mwana wa Yetheri. Aliwaua, na hivyo akamwaga damu+ ya vita wakati wa amani, akapaka damu ya vita kwenye mshipi uliokuwa kiunoni mwake na kwenye viatu alivyokuwa amevaa miguuni.  Ni lazima utende kulingana na hekima yako, nawe usimruhusu ashuke Kaburini* kwa amani akiwa amezeeka.*+  “Lakini watendee wana wa Barzilai+ Mgileadi kwa upendo mshikamanifu, nao wanapaswa kuwa miongoni mwa wale wanaokula mezani pako, kwa maana hivyo ndivyo walivyonisaidia+ nilipomkimbia Absalomu ndugu yako.+  “Pia, Shimei mwana wa Gera, Mbenjamini, kutoka Bahurimu yuko pamoja nawe. Yeye ndiye aliyenitukana vikali+ siku niliyokuwa nikienda Mahanaimu;+ lakini aliposhuka kuja kunipokea kwenye Mto Yordani, nilimwapia hivi kwa jina la Yehova: ‘Sitakuua kwa upanga.’+  Sasa usikose kumwadhibu,+ kwa maana wewe ni mtu mwenye hekima nawe unajua unalopaswa kumtendea; usimruhusu azeeke na kushuka Kaburini.”**+ 10  Kisha Daudi akafa na kuzikwa pamoja na mababu zake katika Jiji la Daudi.+ 11  Daudi alitawala Israeli kwa miaka 40. Alitawala Hebroni+ kwa miaka 7, na Yerusalemu kwa miaka 33.+ 12  Kisha Sulemani akaketi kwenye kiti cha ufalme cha Daudi baba yake, na ufalme wake ukaimarishwa kabisa hatua kwa hatua.+ 13  Baada ya muda Adoniya mwana wa Hagithi akaja kwa Bath-sheba, mama ya Sulemani. Bath-sheba akamuuliza: “Je, umekuja kwa amani?” Akamjibu: “Ni kwa amani.” 14  Adoniya akasema: “Ningependa kukwambia jambo fulani.” Basi akamwambia: “Sema.” 15  Adoniya akasema: “Unajua vizuri kwamba ufalme ulipaswa kuwa wangu, na Waisraeli wote walitarajia niwe mfalme;+ lakini ufalme uliniponyoka ukawa wa ndugu yangu, kwa maana Yehova ndiye aliyempa.+ 16  Lakini sasa nakuomba jambo moja tu. Usikatae ombi langu.” Basi Bath-sheba akamwambia: “Sema.” 17  Adoniya akasema: “Tafadhali, mwombe Mfalme Sulemani—kwa maana hawezi kukataa ombi lako—anipe Abishagi,+ Mshunamu, awe mke wangu.” 18  Ndipo Bath-sheba akasema: “Sawa kabisa! Nitazungumza na mfalme kwa niaba yako.” 19  Kwa hiyo Bath-sheba akaenda kuzungumza na Mfalme Sulemani kwa niaba ya Adoniya. Mara moja mfalme akainuka ili kumpokea, akamwinamia. Kisha akaketi kwenye kiti chake cha ufalme, akaagiza pia mama yake aletewe kiti cha ufalme, ili aketi upande wake wa kulia. 20  Bath-sheba akasema: “Nina ombi moja dogo. Usikatae ombi langu.” Basi mfalme akamwambia: “Mama yangu, sema ombi lako; kwa sababu sitalikataa.” 21  Akasema: “Mruhusu Abishagi, Mshunamu, awe mke wa Adoniya ndugu yako.” 22  Ndipo Mfalme Sulemani akamjibu mama yake: “Kwa nini unaomba Abishagi Mshunamu awe mke wa Adoniya? Huenda ukamwombea pia ufalme,+ kwa sababu yeye ni ndugu yangu mkubwa,+ naye anaungwa mkono na kuhani Abiathari na Yoabu+ mwana wa Seruya.”+ 23  Kwa hiyo Mfalme Sulemani akaapa hivi kwa jina la Yehova: “Mungu na aniadhibu, tena vikali, ikiwa Adoniya hakuomba jambo hilo akijua kwamba anahatarisha uhai wake.* 24  Na sasa, kwa hakika kama Yehova anavyoishi, ambaye ameniimarisha kabisa+ na kuniketisha kwenye kiti cha ufalme cha Daudi baba yangu na kunijengea nyumba* kama alivyoahidi,+ Adoniya atauawa+ leo.” 25  Mara moja Mfalme Sulemani akamtuma Benaya+ mwana wa Yehoyada, akatoka na kwenda kumpiga Adoniya, akafa. 26  Mfalme akamwambia kuhani Abiathari:+ “Nenda Anathothi+ kwenye mashamba yako! Unastahili kufa, lakini leo sitakuua kwa sababu ulibeba Sanduku la Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova mbele ya baba yangu Daudi+ na kwa sababu ulishiriki katika mateso yote ya baba yangu.”+ 27  Basi Sulemani akamwondoa Abiathari asiendelee kutumikia akiwa kuhani wa Yehova, ili kutimiza neno ambalo Yehova alisema dhidi ya nyumba ya Eli+ kule Shilo.+ 28  Habari hizo zilipomfikia Yoabu—kwa maana Yoabu alikuwa amemuunga mkono Adoniya+ lakini hakuwa amemuunga mkono Absalomu+—Yoabu akakimbilia katika hema la Yehova+ na kushika kwa nguvu pembe za madhabahu. 29  Kisha Mfalme Sulemani akaambiwa hivi: “Yoabu amekimbilia katika hema la Yehova, na yuko humo kando ya madhabahu.” Kwa hiyo Sulemani akamtuma Benaya mwana wa Yehoyada, akisema: “Nenda ukamuue!” 30  Basi Benaya akaenda katika hema la Yehova na kumwambia, “Mfalme anasema hivi: ‘Toka nje!’” Lakini Yoabu akasema: “Hapana! Nitafia hapa.” Benaya akarudi kwa mfalme na kumwambia: “Hivi ndivyo alivyosema Yoabu, na hivi ndivyo alivyonijibu.” 31  Kisha mfalme akamwambia: “Fanya kama alivyosema; muue na umzike, uniondolee mimi na nyumba ya baba yangu damu ambayo Yoabu alimwaga kwa njia isiyo ya haki.+ 32  Yehova atamlipiza kwa sababu ya damu aliyomwaga,* kwa sababu bila Daudi baba yangu kujua, aliwapiga na kuwaua kwa upanga wanaume wawili walio waadilifu na bora kuliko yeye, yaani, Abneri+ mwana wa Neri mkuu wa jeshi la Israeli,+ na Amasa+ mwana wa Yetheri, mkuu wa jeshi la Yuda.+ 33  Hatia ya damu yao itakuwa juu ya kichwa cha Yoabu na juu ya kichwa cha uzao* wake milele;+ lakini amani kutoka kwa Yehova na iwe milele juu ya Daudi, uzao* wake, nyumba yake, na kiti chake cha ufalme.” 34  Kisha Benaya mwana wa Yehoyada akapanda kwenda huko, akampiga Yoabu na kumuua, akazikwa nyumbani kwake nyikani. 35  Halafu mfalme akamweka Benaya+ mwana wa Yehoyada kuwa mkuu wa jeshi baada yake, na mfalme akamweka Sadoki+ kuwa kuhani badala ya Abiathari. 36  Kisha mfalme akamwita Shimei+ na kumwambia: “Jijengee nyumba Yerusalemu, uishi huko; usitoke huko na kwenda mahali pengine popote. 37  Siku utakapotoka na kuvuka Bonde la Kidroni,+ ujue kwa hakika kwamba utakufa. Damu yako itakuwa juu ya kichwa chako mwenyewe.” 38  Shimei akamwambia mfalme: “Jambo ulilosema si baya. Mimi mtumishi wako nitafanya kama ulivyosema bwana wangu mfalme.” Basi Shimei akakaa Yerusalemu kwa siku nyingi. 39  Lakini baada ya miaka mitatu, watumwa wawili wa Shimei wakatoroka na kwenda kwa Akishi+ mwana wa Maaka mfalme wa Gathi. Shimei alipoambiwa, “Tazama! Watumwa wako wameenda Gathi,” 40  mara moja Shimei akaweka matandiko juu ya punda wake, akaenda Gathi kwa Akishi kuwatafuta watumwa wake. Shimei aliporudi kutoka Gathi pamoja na watumwa wake, 41  Sulemani akaambiwa: “Shimei aliondoka Yerusalemu na kwenda Gathi, naye amerudi.” 42  Ndipo mfalme akamwita Shimei na kumuuliza: “Je, sikukuapisha kwa jina la Yehova na kukuonya kwa kusema, ‘Siku utakapotoka hapa na kwenda mahali pengine popote, ujue kwa hakika kwamba utakufa’? Na je, wewe hukuniambia, ‘Jambo ulilosema ni sawa; nitatii’?+ 43  Kwa nini basi, hukutii kiapo cha Yehova na amri niliyokupa?” 44  Kisha mfalme akamwambia Shimei: “Unajua moyoni mwako madhara yote uliyomtendea baba yangu Daudi,+ basi Yehova atakulipiza kwa sababu ya madhara hayo.*+ 45  Lakini mimi Mfalme Sulemani nitabarikiwa,+ na kiti cha ufalme cha Daudi kitaimarishwa kabisa mbele za Yehova milele.” 46  Ndipo mfalme akamwamuru Benaya mwana wa Yehoyada, basi akatoka nje na kumpiga Shimei, akamuua.+ Hivyo, ufalme ukaimarishwa kabisa mikononi mwa Sulemani.+

Maelezo ya Chini

Tnn., “Ninafuata njia ya dunia yote.”
Tnn., “maamuzi yake.”
Au “utakapotenda kwa hekima.”
Angalia Kamusi.
Au “Sheoli.” Angalia Kamusi.
Tnn., “usiruhusu mvi zake zishuke kwa amani Kaburini.”
Au “Sheoli.” Angalia Kamusi.
Tnn., “ni lazima ushushe mvi zake Kaburini pamoja na damu.”
Au “dhidi ya nafsi yake.”
Au “ukoo wa kifalme.”
Tnn., “atarudisha damu yake juu ya kichwa chake mwenyewe.”
Au “wazao.”
Au “wazao.”
Tnn., “ataleta madhara hayo juu ya kichwa chako mwenyewe.”