Kitabu cha Kwanza cha Wafalme 22:1-53

  • Yehoshafati aungana na Ahabu (1-12)

  • Mikaya atabiri kwamba watashindwa (13-28)

    • Roho ya udanganyifu itampumbaza Ahabu (21, 22)

  • Ahabu auawa huko Ramothi-gileadi (29-40)

  • Yehoshafati atawala Yuda (41-50)

  • Ahazia mfalme wa Israeli (51-53)

22  Kwa miaka mitatu hakukuwa na vita kati ya Siria na Israeli.  Katika mwaka wa tatu, Mfalme Yehoshafati+ wa Yuda akashuka kwenda kwa mfalme wa Israeli.+  Kisha mfalme wa Israeli akawaambia watumishi wake: “Je, mnajua kwamba Ramothi-gileadi+ ni jiji letu? Na bado tunasitasita kulichukua kutoka kwa mfalme wa Siria.”  Halafu akamuuliza Yehoshafati: “Je, utaenda pamoja nami kupigana kule Ramothi-gileadi?” Yehoshafati akamjibu hivi mfalme wa Israeli: “Mimi ni kama wewe. Watu wangu ni kama watu wako. Farasi wangu ni kama farasi wako.”+  Lakini Yehoshafati akamwambia mfalme wa Israeli: “Tafadhali, kwanza tafuta+ neno la Yehova.”+  Kwa hiyo mfalme wa Israeli akawakusanya pamoja manabii, wanaume wapatao 400, akawauliza: “Je, niende kupigana vita dhidi ya Ramothi-gileadi, au nisiende?” Wakasema: “Panda uende, na Yehova atalitia jiji hilo mikononi mwako.”  Kisha Yehoshafati akasema: “Je, hakuna nabii wa Yehova mahali hapa? Acheni tumuulize yeye pia.”+  Ndipo mfalme wa Israeli akamwambia Yehoshafati: “Bado kuna mtu mmoja ambaye tunaweza kumwomba ushauri kutoka kwa Yehova;+ lakini ninamchukia,+ kwa maana hatabiri kamwe mambo mema kunihusu, ila mabaya tu.+ Anaitwa Mikaya mwana wa Imla.” Hata hivyo, Yehoshafati akasema: “Mfalme, usiseme jambo kama hilo.”  Basi mfalme wa Israeli akamwita ofisa fulani wa makao ya mfalme na kumwambia: “Mlete haraka Mikaya mwana wa Imla.”+ 10  Sasa mfalme wa Israeli na Yehoshafati mfalme wa Yuda walikuwa wameketi kila mmoja wao kwenye kiti chake cha ufalme, akiwa amevaa mavazi ya kifalme, katika uwanja wa kupuria nafaka kwenye lango la kuingia Samaria, na manabii wote walikuwa wakitabiri mbele yao.+ 11  Kisha Sedekia mwana wa Kenaana akajitengenezea pembe za chuma na kusema: “Yehova anasema hivi: ‘Kwa pembe hizi utawapiga* Wasiria mpaka utakapowaangamiza.’” 12  Wale manabii wengine wote walikuwa wakitabiri vivyo hivyo, wakisema: “Panda mpaka Ramothi-gileadi, nawe utafanikiwa; Yehova atalitia jiji hilo mikononi mwako mfalme.” 13  Basi mjumbe aliyeenda kumwita Mikaya akamwambia: “Tazama! Manabii wote kwa pamoja wanasema mema kumhusu mfalme. Tafadhali, acha neno lako liwe kama maneno yao, useme mema.”+ 14  Lakini Mikaya akasema: “Kwa hakika kama Yehova anavyoishi, jambo lolote ambalo Yehova ataniambia ndilo nitakalosema.” 15  Kisha akaingia kwa mfalme, naye mfalme akamuuliza: “Mikaya, je, twende kupigana vita dhidi ya Ramothi-gileadi, au tusiende?” Mara moja akajibu: “Panda uende nawe utafanikiwa; Yehova atalitia jiji hilo mikononi mwako.” 16  Ndipo mfalme akamuuliza: “Nitakuapisha mara ngapi kwamba hupaswi kuniambia jambo lingine lolote isipokuwa ukweli katika jina la Yehova?” 17  Basi Mikaya akasema: “Ninawaona Waisraeli wote wakiwa wametawanyika milimani,+ kama kondoo wasio na mchungaji. Yehova akasema: ‘Hawa hawana bwana. Acha kila mmoja wao arudi kwa amani nyumbani kwake.’” 18  Kisha mfalme wa Israeli akamwambia Yehoshafati: “Je, sikukwambia, ‘Hatatabiri mambo mema kunihusu, ila mabaya’?”+ 19  Ndipo Mikaya akasema: “Basi, sikia neno la Yehova: Nilimwona Yehova akiwa ameketi kwenye kiti chake cha ufalme+ na jeshi lote la mbinguni likiwa limesimama kando yake, upande wake wa kulia na upande wake wa kushoto.+ 20  Halafu Yehova akauliza, ‘Ni nani atakayemdanganya Ahabu, ili apande kwenda na kufia huko Ramothi-gileadi?’ Na malaika mmoja akasema jambo moja na mwingine akasema jambo lingine. 21  Kisha roho*+ fulani akaja na kusimama mbele za Yehova na kusema, ‘Mimi nitamdanganya.’ Yehova akamuuliza, ‘Utatumia njia gani?’ 22  Akajibu, ‘Nitaenda na kuwa roho ya udanganyifu katika vinywa vya manabii wake wote.’+ Kwa hiyo akasema, ‘Utamdanganya, na zaidi ya hilo, utafanikiwa. Nenda ukafanye hivyo.’ 23  Na sasa Yehova ametia roho ya udanganyifu katika vinywa vya hawa manabii wako wote,+ lakini Yehova ametangaza kwamba utapata msiba.”+ 24  Sasa Sedekia mwana wa Kenaana akamkaribia Mikaya na kumpiga kwenye shavu na kumuuliza: “Roho ya Yehova iliniacha jinsi gani na kuja kuzungumza nawe?”+ 25  Mikaya akamjibu: “Tazama! Utajua ni jinsi gani utakapoingia katika chumba cha ndani zaidi kujificha.” 26  Ndipo mfalme wa Israeli akasema: “Mchukue Mikaya umpeleke kwa Amoni mkuu wa jiji na kwa Yoashi mwana wa mfalme. 27  Waambie, ‘Mfalme anasema hivi: “Mfungeni mtu huyu gerezani+ na kumlisha kiasi kidogo cha mkate na maji mpaka nitakaporudi kwa amani.”’” 28  Lakini Mikaya akasema: “Ukirudi kwa amani, basi Yehova hajazungumza nami.”+ Kisha akasema: “Zingatieni maneno yangu, enyi watu wote.” 29  Basi mfalme wa Israeli na Yehoshafati mfalme wa Yuda wakapanda kwenda Ramothi-gileadi.+ 30  Ndipo mfalme wa Israeli akamwambia Yehoshafati: “Nitabadili sura yangu na kuingia vitani, lakini wewe vaa mavazi yako ya kifalme.” Kwa hiyo mfalme wa Israeli akabadili sura yake+ na kuingia vitani. 31  Sasa mfalme wa Siria alikuwa amewaagiza hivi makamanda wake 32 wa magari ya vita:+ “Msipigane na yeyote, mdogo au mkubwa, isipokuwa mfalme wa Israeli.” 32  Na mara tu makamanda hao wa magari ya vita walipomwona Yehoshafati, wakaambiana: “Hakika huyu ndiye mfalme wa Israeli.” Basi wakamgeukia ili kupigana naye; na Yehoshafati akaanza kulilia msaada. 33  Makamanda hao wa magari ya vita walipoona kwamba hakuwa mfalme wa Israeli, mara moja wakaacha kumfuatia. 34  Lakini mtu fulani alivuta upinde wake bila kukusudia na kumpiga mfalme wa Israeli katikati ya sehemu ambazo koti lake la vita linaungana. Basi mfalme akamwambia mtu aliyeendesha gari lake: “Geuka uniondoe vitani,* kwa sababu nimejeruhiwa vibaya.”+ 35  Vita vikapamba moto siku hiyo yote, nao wakalazimika kumsimamisha mfalme ndani ya gari akiwaelekea Wasiria. Damu ya jeraha lake ikamwagika ndani ya gari lake la vita, akafa jioni.+ 36  Jua lilipokuwa likitua amri hii ikatangazwa kambini: “Kila mtu aende katika jiji lake! Kila mtu aende katika nchi yake!”+ 37  Basi mfalme akafa, akaletwa Samaria; wakamzika mfalme huko Samaria. 38  Walipolisafisha gari hilo la vita kando ya kidimbwi cha Samaria, mbwa waliramba damu yake na makahaba wakaogea mahali hapo,* kama Yehova alivyokuwa amesema.+ 39  Na mambo mengine katika historia ya Ahabu, mambo yote aliyofanya na nyumba aliyojenga ya* pembe za tembo+ na majiji yote aliyojenga, je, hayajaandikwa katika kitabu cha historia ya nyakati za wafalme wa Israeli? 40  Kisha Ahabu akafa na kuzikwa pamoja na mababu zake;+ na Ahazia+ mwana wake akawa mfalme baada yake. 41  Yehoshafati+ mwana wa Asa aliwekwa kuwa mfalme wa Yuda katika mwaka wa nne wa utawala wa Mfalme Ahabu wa Israeli. 42  Yehoshafati alikuwa na umri wa miaka 35 alipowekwa kuwa mfalme, naye alitawala kwa miaka 25 huko Yerusalemu. Mama yake aliitwa Azuba binti ya Shilhi. 43  Yehoshafati aliendelea kutembea katika njia yote ya Asa+ baba yake. Hakugeuka na kuiacha njia hiyo, naye alitenda yaliyokuwa sawa machoni pa Yehova.+ Hata hivyo, mahali pa juu hapakuondolewa, na bado watu walikuwa wakitoa dhabihu na kufukiza moshi wa dhabihu mahali pa juu.+ 44  Yehoshafati alidumisha mahusiano ya amani na mfalme wa Israeli.+ 45  Na mambo mengine katika historia ya Yehoshafati, mambo makuu aliyotekeleza na jinsi alivyopigana vita, je, hayajaandikwa katika kitabu cha historia ya nyakati za wafalme wa Yuda? 46  Pia aliwaondoa kabisa nchini wanaume wote makahaba wa hekaluni+ waliobaki katika siku za Asa baba yake.+ 47  Wakati huo hakukuwa na mfalme katika nchi ya Edomu;+ naibu ndiye aliyetawala kama mfalme.+ 48  Yehoshafati pia akatengeneza meli* za Tarshishi za kwenda Ofiri kuleta dhahabu,+ lakini hazikwenda kwa sababu meli hizo zilivunjika huko Esion-geberi.+ 49  Wakati huo ndipo Ahazia mwana wa Ahabu alipomwambia Yehoshafati: “Waruhusu watumishi wangu wasafiri na watumishi wako katika meli hizo,” lakini Yehoshafati hakukubali. 50  Kisha Yehoshafati akafa na kuzikwa pamoja na mababu zake+ katika Jiji la Daudi babu yake; na Yehoramu+ mwanawe akawa mfalme baada yake. 51  Ahazia+ mwana wa Ahabu akawa mfalme wa Israeli huko Samaria katika mwaka wa 17 wa utawala wa Mfalme Yehoshafati wa Yuda, naye alitawala Israeli kwa miaka miwili. 52  Aliendelea kutenda maovu machoni pa Yehova na kutembea katika njia ya baba yake+ na mama yake+ na katika njia ya Yeroboamu mwana wa Nebati, aliyesababisha Waisraeli watende dhambi.+ 53  Aliendelea kumwabudu Baali+ na kumwinamia, akaendelea kumkasirisha Yehova Mungu wa Israeli,+ kama baba yake alivyokuwa amefanya.

Maelezo ya Chini

Au “utawasukuma.”
Au “malaika.”
Tnn., “kambini.”
Au labda, “mbwa waliramba damu yake mahali ambapo makahaba waliogea.”
Au “jumba la mfalme alilojenga la.”
Angalia Kamusi.