Kitabu cha Kwanza cha Wafalme 4:1-34

  • Wasimamizi katika utawala wa Sulemani (1-19)

  • Ufanisi katika utawala wa Sulemani (20-28)

    • Wakaa kwa usalama chini ya mzabibu na mtini (25)

  • Hekima na methali za Sulemani (29-34)

4  Mfalme Sulemani alitawala Israeli yote.+  Hawa ndio waliokuwa maofisa wake wakuu:* Azaria mwana wa Sadoki+ alikuwa kuhani;  Elihorefu na Ahiya wana wa Shisha walikuwa waandishi;+ Yehoshafati+ mwana wa Ahiludi alifanya kazi ya kuweka kumbukumbu;  Benaya+ mwana wa Yehoyada alikuwa mkuu wa jeshi; Sadoki na Abiathari+ walikuwa makuhani;  Azaria mwana wa Nathani+ alikuwa mkuu wa wasaidizi; Zabudi mwana wa Nathani alikuwa kuhani na rafiki ya mfalme;+  Ahishari alikuwa msimamizi wa nyumba; na Adoniramu+ mwana wa Abda aliwasimamia wale walioandikishwa kufanya kazi ya kulazimishwa.+  Sulemani alikuwa na wasaidizi 12 waliowasimamia Waisraeli wote waliomwandalia chakula mfalme na nyumba yake. Kila mmoja wao alikuwa na jukumu la kuandaa chakula mwezi mmoja kwa mwaka.+  Haya ndiyo majina yao: Mwana wa Huru, katika eneo lenye milima la Efraimu;  mwana wa Dekeri, kule Makazi, Shaalbimu,+ Beth-shemeshi, na Elon-beth-hanani; 10  mwana wa Hesedi, kule Arubothi (alisimamia Soko na nchi yote ya Heferi); 11  mwana wa Abinadabu, katika milima yote ya Dori (Tafathi, binti ya Sulemani, akawa mke wake); 12  Baana mwana wa Ahiludi, kule Taanaki, Megido,+ na eneo lote la Beth-sheani,+ ambalo liko kando ya Sarethani chini ya Yezreeli, kuanzia Beth-sheani mpaka Abel-mehola hadi eneo la Yokmeamu;+ 13  mwana wa Geberi, kule Ramothi-gileadi+ (alisimamia vijiji vya mahema vya Yairi+ mwana wa Manase, vilivyoko Gileadi;+ alisimamia pia eneo la Argobu,+ lililoko Bashani:+ majiji makubwa 60 yenye kuta na makomeo ya shaba); 14  Ahinadabu mwana wa Ido, kule Mahanaimu;+ 15  Ahimaazi, kule Naftali (alimwoa Basemathi, binti mwingine wa Sulemani); 16  Baana mwana wa Hushai, kule Asheri na Bealothi; 17  Yehoshafati mwana wa Parua, kule Isakari; 18  Shimei+ mwana wa Ela, kule Benjamini;+ 19  Geberi mwana wa Uri, katika nchi ya Gileadi,+ nchi ya Sihoni+ mfalme wa Waamori, na ya Ogu+ mfalme wa Bashani. Kulikuwa pia na msaidizi mmoja aliyewasimamia wasaidizi hao wengine wote nchini. 20  Watu wa Yuda na Israeli walikuwa wengi sana kama chembe za mchanga kando ya bahari;+ walikuwa wakila na kunywa na kushangilia.+ 21  Sulemani alitawala falme zote kuanzia Mto Efrati+ mpaka nchi ya Wafilisti hadi kwenye mpaka wa Misri. Walimletea Sulemani ushuru na kumtumikia siku zote za maisha yake.+ 22  Chakula cha kila siku cha Sulemani kilikuwa kori 30* za unga laini na kori 60 za unga, 23  ng’ombe 10 waliononeshwa, ng’ombe 20 waliopelekwa malishoni, na kondoo 100, pamoja na paa kadhaa, swala, kulungu, na ndege waliononeshwa. 24  Kwa maana alitawala kila kitu upande huu wa Mto Efrati,*+ kuanzia Tifsa mpaka Gaza,+ pamoja na wafalme wote upande huu wa Mto Efrati; naye alikuwa na amani katika maeneo yake yote.+ 25  Watu wa Yuda na Israeli waliishi kwa usalama, kila mtu chini ya mzabibu wake mwenyewe na chini ya mtini wake mwenyewe, kuanzia Dani mpaka Beer-sheba, siku zote za Sulemani. 26  Na Sulemani alikuwa na mabanda 4,000* ya farasi wa magari yake ya vita, na farasi* 12,000.+ 27  Wasaidizi hao walimletea chakula Mfalme Sulemani na pia kila mtu aliyekula mezani pa Mfalme Sulemani. Kila mmoja wao alikuwa na jukumu la kuleta chakula mwezi aliopangiwa na kuhakikisha kwamba hakuna chochote kilichokosekana.+ 28  Walipeleka pia shayiri na majani mahali popote yalipohitajiwa kwa ajili ya farasi na kwa ajili ya farasi waliokokota magari, kila mmoja kulingana na kiasi alichogawiwa. 29  Naye Mungu akampa Sulemani hekima na utambuzi mwingi sana na moyo wenye uelewaji mwingi kama mchanga kwenye ufuo wa bahari.+ 30  Hekima ya Sulemani ilizidi hekima ya watu wote wa Mashariki na hekima yote ya Misri.+ 31  Alikuwa na hekima kuliko mwanadamu mwingine yeyote; alikuwa na hekima kuliko Ethani+ Mwezra na Hemani,+ Kalkoli,+ na Darda, wana wa Maholi; umaarufu wake ulienea katika mataifa yote yaliyomzunguka.+ 32  Alitunga* methali 3,000+ na nyimbo zake+ zilikuwa 1,005. 33  Alizungumza kuhusu miti, kuanzia mwerezi wa Lebanoni mpaka mhisopo+ unaomea ukutani; alizungumza kuhusu wanyama,+ ndege,*+ viumbe wanaotambaa,*+ na samaki. 34  Watu kutoka katika mataifa yote walikuja kuisikia hekima ya Sulemani, pamoja na wafalme kutoka kotekote duniani waliokuwa wamesikia kuhusu hekima yake.+

Maelezo ya Chini

Au “wakuu wake.”
Kori moja ilikuwa sawa na lita 220 (kilogramu 170 hivi). Angalia Nyongeza B14.
Yaani, upande wa magharibi wa Mto Efrati.
Idadi hii inapatikana katika baadhi ya hati na pia katika simulizi lingine kama hili. Hati nyingine zinasema mabanda hayo yalikuwa 40,000.
Au “wapanda farasi.”
Au “Alinena.”
Au “viumbe wanaoruka.”
Huenda viumbe hao walitia ndani wanyama wanaotambaa na wadudu.