Kitabu cha Kwanza cha Wafalme 7:1-51

  • Majengo yaliyozunguka jumba la Mfalme Sulemani (1-12)

  • Hiramu mwenye ustadi amsaidia Sulemani (13-47)

    • Nguzo mbili za shaba (15-22)

    • Bahari ya madini yaliyoyeyushwa (23-26)

    • Magari kumi na mabeseni ya shaba (27-39)

  • Vyombo vya dhahabu vyakamilishwa (48-51)

7  Sulemani alijenga nyumba yake mwenyewe*+ kwa miaka 13, mpaka alipoikamilisha nyumba yake yote.+  Naye alijenga Nyumba ya Msitu wa Lebanoni+ yenye urefu wa mikono 100,* upana wa mikono 50, na kimo cha mikono 30 juu ya safu nne za nguzo za mierezi; na boriti za mierezi+ zilikuwa juu ya nguzo hizo.  Nayo ilifunikwa juu kwa mbao za mierezi zilizokuwa juu ya mihimili iliyolala juu ya nguzo hizo; mihimili hiyo ilikuwa 45, kila safu ilikuwa na mihimili 15.  Kulikuwa na safu tatu za madirisha yenye viunzi, na kila dirisha lilielekeana na dirisha lingine katika mistari mitatu.  Milango yote na miimo ya milango ilikuwa na viunzi vya mraba,* na sehemu ya mbele ya madirisha yaliyoelekeana katika mistari mitatu ilikuwa pia ya mraba.  Naye alijenga Ukumbi wa Nguzo wenye urefu wa mikono 50 na upana wa mikono 30, na mbele yake kulikuwa na ukumbi mwingine wenye nguzo na paa dogo lililochomoza mbele.  Alijenga pia Ukumbi wa Kiti cha Ufalme+ ambamo alisikiliza kesi—Ukumbi wa Hukumu+—nao waliufunika kwa mbao za mierezi kuanzia sakafuni mpaka kwenye maboriti.  Nyumba* ambamo angeishi, katika ule ua mwingine,+ ilijengwa nyuma mbali na Ukumbi,* na muundo wake ulifanana na wa majengo mengine. Alimjengea pia binti ya Farao nyumba iliyofanana na Ukumbi huo; Sulemani alikuwa amemwoa binti huyo.+  Majengo hayo yote yalijengwa kwa mawe ghali+ yaliyochongwa kwa vipimo, yaliyokatwa ndani na nje kwa misumeno ya mawe, kuanzia kwenye msingi mpaka juu ya ukuta, na upande wa nje mpaka kwenye ule ua mkuu.+ 10  Na msingi ulijengwa kwa mawe makubwa sana na yaliyo ghali; baadhi ya mawe yalikuwa na ukubwa wa mikono kumi, na mawe mengine mikono minane. 11  Na juu ya mawe hayo kulikuwa na mawe ghali, yaliyochongwa kwa vipimo, na pia mbao za mierezi. 12  Ua mkuu ulizungukwa na ukuta wenye safu tatu za mawe yaliyochongwa na safu ya maboriti ya mierezi, kama ulivyokuwa ua wa ndani+ wa nyumba ya Yehova na ukumbi wa nyumba.+ 13  Mfalme Sulemani akawatuma watu wamwite Hiramu,+ akaletwa kutoka Tiro. 14  Alikuwa mwana wa mwanamke mjane kutoka katika kabila la Naftali, na baba yake alikuwa mfua shaba+ kutoka Tiro; Hiramu alikuwa na ustadi wa hali ya juu, uelewaji,+ na uzoefu wa kutengeneza vitu vya shaba vya kila aina. Basi akaja kwa Mfalme Sulemani na kufanya kazi yake yote. 15  Alitengeneza nguzo mbili kwa kutumia shaba iliyoyeyushwa;+ kila nguzo ilikuwa na urefu wa mikono 18, na kila moja ya nguzo hizo mbili ingeweza kuzungukwa kwa kamba yenye urefu wa mikono 12.*+ 16  Naye alitumia shaba iliyoyeyushwa kutengeneza vifuniko viwili ambavyo vingewekwa juu ya nguzo hizo. Kifuniko kimoja kilikuwa na urefu wa mikono mitano, na kingine kilikuwa na urefu wa mikono mitano. 17  Kifuniko cha kila nguzo kilikuwa na wavu uliofumwa wa minyororo;+ nguzo moja ilikuwa na nyavu saba na nguzo nyingine nyavu saba. 18  Naye alitengeneza safu mbili za makomamanga kuzunguka wavu uliofunika vifuniko vilivyokuwa juu ya nguzo; alifanya hivyo kwa kila nguzo. 19  Vifuniko vilivyokuwa juu ya nguzo za ukumbi vilikuwa na umbo la yungiyungi, na urefu wake ulikuwa mikono minne. 20  Vifuniko hivyo vilikuwa juu ya zile nguzo mbili, juu tu ya sehemu ya mviringo iliyoungana na zile nyavu; na kulikuwa na safu za makomamanga 200 kuzunguka kila kifuniko cha nguzo.+ 21  Alisimamisha nguzo za ukumbi wa hekalu.*+ Alisimamisha nguzo ya kulia* na kuiita Yakini,* kisha akasimamisha nguzo ya kushoto* na kuiita Boazi.*+ 22  Sehemu ya juu ya nguzo hizo ilikuwa na umbo la yungiyungi. Basi kazi ya kutengeneza nguzo ikakamilika. 23  Kisha akatengeneza Bahari* kwa madini yaliyoyeyushwa.+ Ilikuwa ya mviringo, yenye upana wa mikono 10 ukingo hadi ukingo na kimo cha mikono 5, na ingeweza kuzungukwa na kamba yenye urefu wa mikono 30.*+ 24  Na chini ya ukingo wake kulikuwa na mapambo ya vibuyu,+ nayo yalizunguka ukingo wote, vibuyu kumi kwa kila mkono mmoja kuzunguka Bahari yote, na safu mbili za vibuyu zilitengenezwa kwa kuyeyushwa zikiwa sehemu ya Bahari hiyo. 25  Ilikuwa juu ya ng’ombe dume 12,+ watatu wakitazama kaskazini, watatu wakitazama magharibi, watatu wakitazama kusini, na watatu wakitazama mashariki; na Bahari hiyo ilikuwa juu yao, na sehemu zao zote za nyuma zilielekea katikati. 26  Na unene wake ulikuwa upana wa kiganja kimoja;* na ukingo wake ulitengenezwa kama ukingo wa kikombe, kama ua la yungiyungi. Ingeweza kujaa maji kiasi cha bathi 2,000.* 27  Kisha akatengeneza magari kumi*+ ya shaba. Kila gari lilikuwa na urefu wa mikono minne, upana wa mikono minne, na kimo cha mikono mitatu. 28  Na hivi ndivyo magari hayo yalivyotengenezwa: Yalikuwa na kuta za pembeni, na kuta hizo za pembeni zilikuwa kati ya mihimili. 29  Na kwenye kuta hizo za pembeni kati ya mihimili hiyo kulikuwa na simba,+ ng’ombe dume, na makerubi,+ na muundo huohuo ulikuwa kwenye mihimili. Juu na chini ya simba na ng’ombe dume hao kulikuwa na mashada ya maua yaliyoyeyushwa. 30  Na kila gari lilikuwa na magurudumu manne ya shaba na vyuma vya katikati vya shaba vinavyozungusha magurudumu hayo, na nguzo nne za pembeni ziliyashikilia. Na kila upande chini ya beseni kulikuwa na vitegemezo vilivyotengenezwa kwa mashada ya maua yaliyoyeyushwa. 31  Mdomo wake ulikuwa katika sehemu ya juu, nao ulichomoza juu kwa kipimo cha mkono mmoja; na mdomo huo ulikuwa wa mviringo, na kitako chote kilikuwa na urefu wa mkono mmoja na nusu, na mdomo wake ulikuwa na michongo. Na kuta za pembeni za magari hayo zilikuwa za mraba, si mviringo. 32  Na yale magurudumu manne yalikuwa chini ya kuta hizo, na nguzo zilizoshikilia magurudumu ziliunganishwa na gari, na kila gurudumu lilikuwa na kimo cha mkono mmoja na nusu. 33  Na magurudumu hayo yalitengenezwa kama magurudumu ya gari la vita. Nguzo zake, mizingo yake, njukuti,* na vitovu vya magudurumu, vyote vilitengenezwa kwa kuyeyushwa. 34  Kulikuwa na nguzo nne kwenye pembe nne za kila gari; nguzo hizo zilitengenezwa kwa kuyeyushwa zikiwa sehemu ya gari hilo.* 35  Juu ya gari hilo kulikuwa na utepe wa mviringo wenye kimo cha nusu mkono, na viunzi vyake na kuta zake za pembeni zilikuwa juu ya gari hilo, nazo zilitengenezwa kwa kuyeyushwa zikiwa sehemu ya gari hilo.* 36  Juu ya viunzi vyake na kwenye kuta zake za pembeni alichonga makerubi, simba, na mitende kulingana na nafasi iliyopatikana kwenye kila kipande, na mashada ya maua kuzunguka pande zote.+ 37  Hivyo ndivyo alivyoyatengeneza magari hayo kumi;+ yote yalitengenezwa kwa kuyeyushwa kwa njia ileile,+ yakiwa na vipimo na umbo lilelile. 38  Alitengeneza mabeseni kumi ya shaba;+ kila beseni lingeweza kujaa kiasi cha bathi 40 za maji. Kila beseni lilikuwa na upana wa mikono 4.* Kulikuwa na beseni moja kwa ajili ya kila mojawapo ya magari hayo kumi. 39  Kisha akaweka magari matano upande wa kulia wa nyumba, na matano upande wa kushoto wa nyumba; akaiweka ile Bahari upande wa kulia wa nyumba, kuelekea kusini mashariki.+ 40  Hiramu+ alitengeneza pia mabeseni, sepetu,+ na mabakuli.+ Basi Hiramu akamaliza kazi yote aliyomfanyia Mfalme Sulemani kuhusiana na nyumba ya Yehova:+ 41  zile nguzo mbili+ na vifuniko vyenye umbo la bakuli vilivyokuwa juu ya nguzo hizo; na nyavu mbili+ za kufunika vifuniko hivyo viwili vyenye umbo la bakuli vilivyokuwa juu ya nguzo hizo; 42  yale makomamanga 400+ kwa ajili ya zile nyavu mbili, safu mbili za makomamanga kwa ajili ya kila wavu, ili kufunika vile vifuniko viwili vyenye umbo la bakuli vilivyokuwa juu ya zile nguzo mbili; 43  yale magari kumi+ na yale mabeseni kumi+ yaliyokuwa juu ya magari hayo; 44  ile Bahari+ na wale ng’ombe dume 12 waliokuwa chini ya Bahari hiyo; 45  na ndoo za kuondolea majivu, sepetu, mabakuli, na vyombo vyote ambavyo Hiramu alimtengenezea Mfalme Sulemani kwa shaba iliyong’arishwa kwa ajili ya nyumba ya Yehova. 46  Mfalme alivitengeneza katika kalibu za udongo wa mfinyanzi katika wilaya ya Yordani, kati ya Sukothi na Sarethani. 47  Sulemani hakupima uzito wa chombo chochote kwa sababu vyombo hivyo vilikuwa vingi sana. Uzito wa shaba haukujulikana.+ 48  Sulemani alivitengeneza vitu vyote vya nyumba ya Yehova: madhabahu+ ya dhahabu; meza ya dhahabu+ ya kuwekea mikate ya wonyesho; 49  vinara vya taa+ vya dhahabu safi, vitano upande wa kulia na vitano upande wa kushoto mbele ya chumba cha ndani zaidi; na maua,+ taa, na koleo, vyote vya dhahabu;+ 50  mabeseni, mikasi ya kukatia tambi za taa,+ mabakuli, vikombe,+ na vyetezo,+ vyote vya dhahabu safi; na bawaba za milango ya nyumba ya ndani,+ yaani, Patakatifu Zaidi, na za milango ya nyumba ya hekalu,+ vyote vya dhahabu. 51  Kwa hiyo Mfalme Sulemani akakamilisha kazi yote aliyopaswa kufanya kwa ajili ya nyumba ya Yehova. Kisha Sulemani akaingiza ndani vitu ambavyo Daudi baba yake alikuwa amevifanya kuwa vitakatifu,+ naye akaweka fedha, dhahabu, na vitu hivyo katika hazina za nyumba ya Yehova.+

Maelezo ya Chini

Au “jumba lake la mfalme.”
Mkono mmoja ulilingana na sentimita 44.5 (inchi 17.5). Angalia Nyongeza B14.
Au “mstatili.”
Tnn., “nyumba ya Ukumbi.”
Au “Jumba la mfalme.”
Au “na kila moja ya nguzo hizo mbili ilikuwa na mzingo wa mikono 12.”
Yaani, Patakatifu.
Au “ya kusini.”
Maana yake “Naye [yaani, Yehova] Aimarishe Kabisa.”
Au “ya kaskazini.”
Labda inamaanisha “Katika Nguvu.”
Au “tangi.”
Au “ilikuwa na mzingo wa mikono 30.”
Bathi ilikuwa sawa na lita 22. Angalia Nyongeza B14.
Karibu sentimita 7.4 (inchi 2.9). Angalia Nyongeza B14.
Au “mikokoteni kumi ya maji.”
Au “tindi.”
Au “zilikuwa kipande kimoja na gari hilo.”
Au “zikiwa kipande kimoja na gari hilo.”
Au “kipenyo cha mikono minne.”