Barua ya Kwanza kwa Wakoritho 9:1-27

  • Mfano wa Paulo akiwa mtume (1-27)

    • “Hupaswi kumfunga kinywa ng’ombe dume” (9)

    • ‘Ole wangu nisipohubiri!’ (16)

    • Kuwa vitu vyote kwa watu wote (19-23)

    • Kujidhibiti katika mbio za uzima (24-27)

9  Je, mimi siko huru? Je, mimi si mtume? Je, mimi sijamwona Yesu Bwana wetu?+ Je, ninyi si kazi yangu katika Bwana?  Hata kama mimi si mtume kwa wengine, hakika mimi ni mtume kwenu! Kwa maana ninyi ndio muhuri unaothibitisha utume wangu katika Bwana.  Kwa wale wanaonichunguza, ninajitetea hivi:⁠  Sisi tuna haki* ya kula na kunywa, sivyo?  Sisi tuna haki ya kuambatana na mke ambaye ni mwamini,*+ kama wale mitume wengine na ndugu za Bwana+ na Kefa,*+ sivyo?  Au je, ni Barnaba+ na mimi pekee ambao hatuna haki ya kupata riziki bila kufanya kazi?  Ni mwanajeshi gani ambaye hutumika kwa gharama yake mwenyewe? Ni nani anayepanda shamba la mizabibu naye asile matunda yake?+ Au ni nani anayechunga mifugo naye asinywe maziwa ya mifugo yake?  Je, ninasema mambo haya kwa maoni ya kibinadamu? Au je, Sheria haisemi mambo hayo pia?  Kwa maana imeandikwa katika Sheria ya Musa: “Hupaswi kumfunga kinywa ng’ombe dume anapopura nafaka.”+ Je, ng’ombe dume ndio Mungu anaohangaikia? 10  Au, je, kweli anasema hivyo kwa ajili yetu? Kwa hakika hilo liliandikwa kwa ajili yetu, kwa sababu mtu anayelima na mtu anayepura anapaswa kufanya hivyo akiwa na tumaini la kupata fungu. 11  Ikiwa tumepanda vitu vya kiroho miongoni mwenu, je, ni jambo kubwa tukivuna kutoka kwenu vitu vya kimwili?+ 12  Ikiwa watu wengine wana haki ya kuwadai ninyi jambo hilo, je, sisi hatuna haki hiyo hata zaidi? Hata hivyo, hatujatumia haki* hii,+ bali tunavumilia mambo yote, ili kwa vyovyote tusiizuie habari njema kumhusu Kristo.+ 13  Je, hamjui kwamba watu wanaofanya kazi takatifu hula vitu vya hekalu, na kwamba wale wanaohudumu kwa kawaida kwenye madhabahu hupata fungu lao kutoka kwenye madhabahu?+ 14  Vivyo hivyo, pia, Bwana aliamuru kwamba wale wanaotangaza habari njema waishi kupitia habari njema.+ 15  Lakini kati ya mipango hiyo sijatumia hata mmoja.+ Kwa kweli, sijaandika mambo haya ili nifanyiwe jambo hilo, kwa maana ingekuwa bora kwangu kufa kuliko—hakuna mtu atakayeondoa sababu zangu za kujisifu!+ 16  Sasa ikiwa ninatangaza habari njema, hiyo si sababu ya kufanya nijisifu, kwa maana nimewekewa sharti. Kwa kweli, ole wangu nisipotangaza habari njema!+ 17  Nikifanya hivyo kwa kupenda, nina thawabu; lakini hata nikifanya hivyo bila kupenda, bado nimekabidhiwa usimamizi.+ 18  Basi, thawabu yangu ni nini? Kwamba ninapotangaza habari njema, niitoe habari njema bila gharama, ili nisitumie vibaya mamlaka* yangu katika habari njema. 19  Kwa maana, ingawa niko huru kutoka kwa watu wote, nimejifanya kuwa mtumwa kwa wote, ili niwapate watu wengi iwezekanavyo. 20  Kwa Wayahudi nilikuwa kama Myahudi, ili niwapate Wayahudi;+ kwa wale walio chini ya sheria nilikuwa kama aliye chini ya sheria, ingawa mimi mwenyewe siko chini ya sheria, ili niwapate wale walio chini ya sheria.+ 21  Kwa wale wasio na sheria nilikuwa kama asiye na sheria, ingawa mimi siko bila sheria kwa Mungu bali niko chini ya sheria kwa Kristo,+ ili niwapate wale wasio na sheria. 22  Kwa walio dhaifu nilikuwa dhaifu, ili niwapate walio dhaifu.+ Nimekuwa mambo yote kwa watu wa namna zote, ili kwa vyovyote niwaokoe wengine. 23  Lakini ninafanya mambo yote kwa ajili ya habari njema, ili niishiriki pamoja na wengine.+ 24  Je, hamjui kwamba wakimbiaji wote katika mbio hukimbia, lakini ni mmoja tu anayepokea tuzo? Kimbieni kwa njia itakayowawezesha kushinda tuzo.+ 25  Sasa kila mtu anayeshiriki katika shindano* hujizuia* katika mambo yote. Bila shaka, wao hushindana ili wapate taji linaloweza kuharibika,+ lakini sisi taji lisiloharibika.+ 26  Kwa hiyo, jinsi ninavyokimbia si bila kusudi;+ jinsi ninavyoelekeza ngumi zangu ni ili nisiwe nikipiga hewa; 27  lakini ninaupigapiga* mwili wangu+ na kuuongoza kama mtumwa, ili baada ya kuwahubiria wengine, kwa njia fulani mimi mwenyewe nisikataliwe.*

Maelezo ya Chini

Tnn., “mamlaka.”
Au “kuwa na dada akiwa mke.”
Pia anaitwa Petro.
Tnn., “mamlaka.”
Au “haki.”
Au “kila mwanariadha.”
Au “hujidhibiti.”
Au “ninauadhibu; ninautia nidhamu sana.”
Au “nikose kustahili.”