Barua ya Kwanza ya Yohana 4:1-21

  • Kuyajaribu maneno yaliyoongozwa na roho (1-6)

  • Kumjua na kumpenda Mungu (7-21)

    • “Mungu ni upendo” (8, 16)

    • Hakuna woga katika upendo (18)

4  Wapendwa, msiamini kila neno lililoongozwa na roho,*+ lakini yajaribuni maneno yaliyoongozwa na roho ili kuona kama yanatoka kwa Mungu,+ kwa kuwa manabii wengi wa uwongo wameingia ulimwenguni.+  Hivi ndivyo mnavyojua ikiwa neno lililoongozwa na roho limetoka kwa Mungu: Kila neno lililoongozwa na roho linalokiri kwamba Yesu Kristo alikuja katika mwili linatoka kwa Mungu.+  Lakini kila neno lililoongozwa na roho ambalo halimkiri Yesu halitoki kwa Mungu.+ Zaidi ya hayo, hili ndilo neno lililoongozwa na roho la yule mpinga-Kristo ambalo mmesikia kwamba linakuja,+ na sasa tayari limo ulimwenguni.+  Ninyi mnatokana na Mungu, watoto wadogo, nanyi mmewashinda,+ kwa sababu yule aliye katika muungano na ninyi+ ni mkuu kuliko yule aliye katika muungano na ulimwengu.+  Wao hutokana na ulimwengu;+ ndiyo sababu wanasema mambo yanayotokana na ulimwengu na ulimwengu huwasikiliza.+  Sisi tunatokana na Mungu. Yeyote anayemjua Mungu hutusikiliza;+ yeyote ambaye hatokani na Mungu hatusikilizi.+ Hivi ndivyo tunavyolitofautisha neno la kweli lililoongozwa na roho na neno lenye kosa lililoongozwa na roho.+  Wapendwa, na tuendelee kupendana,+ kwa sababu upendo unatoka kwa Mungu, na kila mtu ambaye hupenda amezaliwa kutokana na Mungu na anamjua Mungu.+  Yeyote ambaye hapendi hajamjua Mungu, kwa sababu Mungu ni upendo.+  Hivi ndivyo upendo wa Mungu ulivyofunuliwa kwetu, kwamba Mungu alimtuma Mwana wake mzaliwa-pekee+ ulimwenguni ili tupate uzima kupitia yeye.+ 10  Hivi ndivyo upendo ulivyo, si kwamba sisi tumempenda Mungu, bali kwamba yeye alitupenda akamtuma Mwana wake kuwa dhabihu ya upatanisho*+ kwa ajili ya dhambi zetu.+ 11  Wapendwa, ikiwa Mungu alitupenda hivi, basi sisi pia tuna wajibu wa kupendana.+ 12  Hakuna mtu ambaye amemwona Mungu wakati wowote.+ Tukiendelea kupendana, Mungu hukaa ndani yetu na upendo wake unakamilishwa ndani yetu.+ 13  Hivi ndivyo tunavyojua kwamba tunakaa katika muungano na yeye na yeye katika muungano na sisi, kwa sababu ametupatia roho yake. 14  Isitoshe, sisi wenyewe tumemwona na tunatoa ushahidi kwamba Baba amemtuma Mwana wake kuwa mwokozi wa ulimwengu.+ 15  Yeyote anayekiri kwamba Yesu ni Mwana wa Mungu,+ Mungu hukaa katika muungano na mtu huyo na yeye katika muungano na Mungu.+ 16  Nasi tumejua na tumeamini kwamba Mungu anatupenda.+ Mungu ni upendo,+ na mtu anayekaa katika upendo hukaa katika muungano na Mungu, na Mungu hukaa katika muungano na yeye.+ 17  Kwa njia hii upendo umekamilishwa ndani yetu, ili tuwe na uhuru wa kusema*+ katika siku ya hukumu, kwa sababu, kama huyo alivyo, ndivyo tulivyo katika ulimwengu huu. 18  Hakuna woga katika upendo,+ lakini upendo mkamilifu hutupa* woga nje, kwa sababu woga hutuzuia. Kwa kweli, mtu aliye mwoga hajakamilishwa katika upendo.+ 19  Sisi tuna upendo, kwa sababu alitupenda kwanza.+ 20  Yeyote akisema, “Ninampenda Mungu,” na bado anamchukia ndugu yake, yeye ni mwongo.+ Kwa maana mtu ambaye hampendi ndugu yake,+ ambaye amemwona, hawezi kumpenda Mungu ambaye hajamwona.+ 21  Nasi tuna amri hii kutoka kwake, kwamba yeyote anayempenda Mungu lazima pia ampende ndugu yake.+

Maelezo ya Chini

Tnn., “kila roho.”
Au “dhabihu kwa ajili ya kufunika; njia ya kuleta maelewano.”
Au “tuwe na uhakika.”
Au “husukuma.”