Kitabu cha Pili cha Mambo ya Nyakati 1:1-17

  • Sulemani aomba hekima (1-12)

  • Utajiri wa Sulemani (13-17)

1  Sulemani mwana wa Daudi alizidi kuimarika katika utawala wake, na Yehova Mungu wake alikuwa pamoja naye, akamfanya kuwa mkuu sana.+  Sulemani aliagiza Waisraeli wote wakusanywe, wakuu wa maelfu na wa mamia, waamuzi, na viongozi wote wa Israeli, viongozi wa koo.*  Kisha Sulemani na Waisraeli wote wakaenda mahali pa juu kule Gibeoni,+ kwa maana hema la mkutano la Mungu wa kweli lilikuwa huko, hema ambalo Musa mtumishi wa Yehova alitengeneza nyikani.  Hata hivyo, Daudi alikuwa amelipandisha Sanduku la Mungu wa kweli kutoka Kiriath-yearimu+ na kulileta mahali ambapo Daudi alikuwa ametayarisha kwa ajili yake; alikuwa amepiga hema kwa ajili ya Sanduku hilo huko Yerusalemu.+  Na ile madhabahu ya shaba+ ambayo Bezaleli+ mwana wa Uri mwana wa Huru alikuwa ametengeneza ilikuwa imewekwa mbele ya hema la ibada la Yehova; na Sulemani na Waisraeli wote walikuwa wakisali mbele yake.*  Kisha Sulemani akamtolea Yehova dhabihu mahali hapo, alitoa dhabihu 1,000 za kuteketezwa kwenye madhabahu ya shaba+ ya hema la mkutano.  Usiku huo Mungu akamtokea Sulemani na kumwambia: “Niombe unachotaka nikupe.”+  Basi Sulemani akamwambia Mungu: “Umemtendea Daudi+ baba yangu kwa upendo mwingi mshikamanifu, nawe umeniweka kuwa mfalme baada yake.+  Sasa, Ee Yehova Mungu, ahadi uliyompa Daudi baba yangu na ithibitike kuwa ya uaminifu,+ kwa maana umeniweka kuwa mfalme juu ya watu wengi sana kama chembe za mavumbi ya dunia.+ 10  Sasa nipe hekima na ujuzi+ ili niwaongoze watu hawa,* kwa maana ni nani anayeweza kulihukumu taifa hili lako lililo kubwa?”+ 11  Kisha Mungu akamwambia Sulemani: “Kwa sababu moyo wako unatamani jambo hilo, nawe hukuomba mali, utajiri, wala heshima wala hukuomba wale wanaokuchukia wafe, wala hukuomba maisha marefu,* lakini umeomba hekima na ujuzi ili uwahukumu watu wangu ambao nimekuweka uwe mfalme wao,+ 12  nitakupa hekima na ujuzi; lakini nitakupa pia mali na utajiri na heshima, kuliko mfalme yeyote kabla yako na mfalme yeyote baada yako.”+ 13  Basi Sulemani akatoka mahali pa juu huko Gibeoni,+ kutoka mbele ya hema la mkutano, akaja Yerusalemu; naye akatawala Israeli. 14  Sulemani akaendelea kukusanya magari ya vita na farasi;* akawa na magari 1,400 ya vita na farasi* 12,000,+ naye aliwaweka katika majiji ya magari ya vita+ karibu naye huko Yerusalemu.+ 15  Mfalme alifanya fedha na dhahabu huko Yerusalemu iwe nyingi kama mawe,+ na mbao za mierezi ziwe nyingi kama mikuyu katika Shefela.+ 16  Farasi wa Sulemani waliletwa kutoka Misri,+ na wafanyabiashara wa mfalme walinunua makundi ya farasi* kwa bei moja.+ 17  Kila gari kutoka Misri lilinunuliwa kwa vipande 600 vya fedha, na farasi alinunuliwa kwa vipande 150; kisha waliwauzia wafalme wote wa Wahiti na wafalme wa Siria.

Maelezo ya Chini

Yaani, ukoo wa upande wa baba.
Au “walikuwa wakitafuta ushauri Wake hapo.”
Tnn., “nitoke nje mbele ya watu hawa na kurudi ndani.”
Tnn., “siku nyingi.”
Au “wapanda farasi.”
Au “wapanda farasi.”
Au labda, “kutoka Misri na kutoka Kue; wafanyabiashara wa mfalme waliwanunua kutoka Kue,” huenda ni Kilikia.