Kitabu cha Pili cha Mambo ya Nyakati 18:1-34

  • Yehoshafati aungana na Ahabu (1-11)

  • Mikaya atabiri kwamba watashindwa (12-27)

  • Ahabu auawa Ramoth-gileadi (28-34)

18  Yehoshafati alikuwa na utajiri na utukufu mwingi,+ lakini alifanya mapatano ya ndoa pamoja na Ahabu.+  Basi miaka kadhaa baadaye alishuka kwenda kwa Ahabu kule Samaria,+ na Ahabu akamtolea yeye na watu waliokuwa pamoja naye dhabihu ya kondoo na ng’ombe wengi. Naye akamhimiza* apande kwenda kushambulia Ramothi-gileadi.+  Kisha Mfalme Ahabu wa Israeli akamuuliza Mfalme Yehoshafati wa Yuda: “Je, utaenda pamoja nami Ramothi-gileadi?” Akamjibu: “Mimi ni kama wewe, na watu wangu ni kama watu wako, nao watakuunga mkono vitani.”  Lakini Yehoshafati akamwambia mfalme wa Israeli: “Tafadhali, kwanza tafuta neno la Yehova.”+  Kwa hiyo mfalme wa Israeli akawakusanya pamoja manabii, wanaume 400, akawauliza: “Je, twende kupigana vita dhidi ya Ramothi-gileadi, au nisiende?” Wakasema: “Panda uende, na Mungu wa kweli atalitia jiji hilo mikononi mwako mfalme.”  Kisha Yehoshafati akasema: “Je, hakuna nabii wa Yehova mahali hapa?+ Acheni tumuulize yeye pia.”+  Ndipo mfalme wa Israeli akamwambia Yehoshafati: “Bado kuna mtu mmoja+ ambaye tunaweza kumwomba ushauri kutoka kwa Yehova; lakini ninamchukia, kwa maana hatabiri kamwe mambo mema kunihusu, anatabiri mabaya sikuzote.+ Anaitwa Mikaya mwana wa Imla.” Hata hivyo, Yehoshafati akasema: “Mfalme, usiseme jambo kama hilo.”  Basi mfalme wa Israeli akamwita ofisa fulani wa makao ya mfalme na kumwambia: “Mlete haraka Mikaya mwana wa Imla.”+  Sasa mfalme wa Israeli na Yehoshafati mfalme wa Yuda walikuwa wameketi kila mmoja wao kwenye kiti chake cha ufalme, akiwa amevaa mavazi ya kifalme, katika uwanja wa kupuria nafaka kwenye lango la kuingia Samaria, na manabii wote walikuwa wakitabiri mbele yao. 10  Kisha Sedekia mwana wa Kenaana akajitengenezea pembe za chuma na kusema: “Yehova anasema hivi: ‘Kwa pembe hizi utawapiga* Wasiria mpaka utakapowaangamiza.’” 11  Wale manabii wengine wote walikuwa wakitabiri vivyo hivyo, wakisema: “Panda mpaka Ramothi-gileadi, nawe utafanikiwa;+ Yehova atalitia jiji hilo mikononi mwako mfalme.” 12  Basi mjumbe aliyeenda kumwita Mikaya akamwambia: “Tazama! Manabii wote kwa pamoja wanasema mema kumhusu mfalme. Tafadhali, acha neno lako liwe kama maneno yao,+ useme mema.”+ 13  Lakini Mikaya akasema: “Kwa hakika kama Yehova anavyoishi, jambo lolote ambalo Mungu wangu atasema ndilo nitakalosema.”+ 14  Kisha akaingia kwa mfalme, naye mfalme akamuuliza: “Mikaya, je, twende kupigana vita dhidi ya Ramothi-gileadi, au nisiende?” Mara moja akajibu: “Panda uende nawe utafanikiwa; watatiwa mikononi mwako.” 15  Ndipo mfalme akamuuliza: “Nitakuapisha mara ngapi kwamba hupaswi kuniambia jambo lingine lolote isipokuwa ukweli katika jina la Yehova?” 16  Basi Mikaya akasema: “Ninawaona Waisraeli wote wakiwa wametawanyika milimani, kama kondoo wasio na mchungaji.+ Yehova akasema: ‘Hawa hawana bwana. Acha kila mmoja wao arudi kwa amani nyumbani kwake.’” 17  Kisha mfalme wa Israeli akamwambia Yehoshafati: “Je, sikukwambia, ‘Hatatabiri mambo mema kunihusu, ila mabaya’?”+ 18  Ndipo Mikaya akasema: “Basi, sikia neno la Yehova: Nilimwona Yehova akiwa ameketi kwenye kiti chake cha ufalme+ na jeshi lote la mbinguni+ likiwa limesimama upande wake wa kulia na upande wake wa kushoto.+ 19  Halafu Yehova akauliza, ‘Ni nani atakayemdanganya Mfalme Ahabu wa Israeli, ili apande kwenda na kufia huko Ramothi-gileadi?’ Na malaika mmoja akasema jambo moja na mwingine akasema jambo lingine. 20  Kisha roho*+ fulani akaja na kusimama mbele za Yehova na kusema, ‘Mimi nitamdanganya.’ Yehova akamuuliza, ‘Utatumia njia gani?’ 21  Akajibu, ‘Nitaenda na kuwa roho ya udanganyifu katika vinywa vya manabii wake wote.’ Kwa hiyo akasema, ‘Utamdanganya, na zaidi ya hilo, utafanikiwa. Nenda ukafanye hivyo.’ 22  Na sasa Yehova ametia roho ya udanganyifu katika vinywa vya hawa manabii wako,+ lakini Yehova ametangaza kwamba utapata msiba.” 23  Sasa Sedekia+ mwana wa Kenaana akamkaribia Mikaya+ na kumpiga kwenye shavu+ na kumuuliza: “Roho ya Yehova iliniacha jinsi gani na kuja kuzungumza nawe?”+ 24  Mikaya akamjibu: “Tazama! Utajua ni jinsi gani utakapoingia katika chumba cha ndani zaidi kujificha.” 25  Ndipo mfalme wa Israeli akasema: “Mchukue Mikaya umpeleke kwa Amoni mkuu wa jiji na kwa Yoashi mwana wa mfalme. 26  Waambie, ‘Mfalme anasema hivi: “Mfungeni mtu huyu gerezani+ na kumlisha kiasi kidogo cha mkate na maji mpaka nitakaporudi kwa amani.”’” 27  Lakini Mikaya akasema: “Ukirudi kwa amani, basi Yehova hajazungumza nami.”+ Kisha akasema: “Zingatieni maneno yangu, enyi watu wote.” 28  Basi mfalme wa Israeli na Yehoshafati mfalme wa Yuda wakapanda kwenda Ramothi-gileadi.+ 29  Ndipo mfalme wa Israeli akamwambia Yehoshafati: “Nitabadili sura yangu na kuingia vitani, lakini wewe vaa mavazi yako ya kifalme.” Kwa hiyo mfalme wa Israeli akabadili sura yake, nao wakaingia vitani. 30  Sasa mfalme wa Siria alikuwa amewaagiza hivi makamanda wake wa magari ya vita: “Msipigane na yeyote, mdogo au mkubwa, isipokuwa mfalme wa Israeli.” 31  Na mara tu makamanda hao wa magari ya vita walipomwona Yehoshafati, wakaambiana: “Ni mfalme wa Israeli.” Basi wakamgeukia ili kupigana naye; na Yehoshafati akaanza kulilia msaada,+ na Yehova akamsaidia, na mara moja Mungu akawaelekeza upande mwingine ili wamwache. 32  Makamanda hao wa magari ya vita walipoona kwamba hakuwa mfalme wa Israeli, mara moja wakaacha kumfuatia. 33  Lakini mtu fulani alivuta upinde wake bila kukusudia* na kumpiga mfalme wa Israeli katikati ya sehemu ambazo koti lake la vita linaungana. Basi mfalme akamwambia mtu aliyeendesha gari lake: “Geuka uniondoe vitani,* kwa sababu nimejeruhiwa vibaya.”+ 34  Vita vikapamba moto siku hiyo yote, nao wakalazimika kumsimamisha mfalme ndani ya gari, akiwaelekea Wasiria mpaka jioni; akafa jua lilipokuwa likitua.+

Maelezo ya Chini

Au “akamshawishi.”
Au “utawasukuma.”
Au “malaika.”
Au “bila nia mbaya.”
Tnn., “kambini.”