Kitabu cha Pili cha Mambo ya Nyakati 20:1-37

  • Mataifa jirani yawatisha watu wa Yuda (1-4)

  • Yehoshafati asali apate msaada (5-13)

  • Jibu la Yehova (14-19)

  • Watu wa Yuda waokolewa kimuujiza (20-30)

  • Mwisho wa utawala wa Yehoshafati (31-37)

20  Baadaye Wamoabu+ na Waamoni,+ pamoja na baadhi ya Waamonimu,* wakaja kupigana vita na Yehoshafati.  Basi Yehoshafati akaambiwa hivi: “Umati mkubwa umekuja kukushambulia kutoka katika eneo la bahari,* kutoka Edomu,+ wamefika Hasason-tamari, yaani, En-gedi.”+  Ndipo Yehoshafati akaogopa, akaazimia* kumtafuta Yehova.+ Basi akatangaza watu wote wa Yuda wafunge.  Kisha watu wa Yuda wakakusanyika pamoja kutafuta ushauri wa Yehova;+ walikuja kutoka katika majiji yote ya Yuda ili kutafuta ushauri wa Yehova.  Ndipo Yehoshafati akasimama katika kutaniko la Yuda na Yerusalemu ndani ya nyumba ya Yehova mbele ya ule ua mpya,  akasema: “Ee Yehova Mungu wa mababu zetu, je, wewe si Mungu mbinguni;+ je, huna mamlaka juu ya falme zote za mataifa?+ Mkononi mwako mna nguvu na uwezo, na hakuna anayeweza kushindana nawe.+  Ee Mungu wetu, je, hukuwafukuza wakaaji wa nchi hii kutoka mbele ya watu wako Waisraeli na kisha kuupa uzao wa* rafiki yako Abrahamu nchi hii iwe miliki yao ya kudumu?+  Nao wakaishi katika nchi hiyo na kukujengea humo mahali patakatifu kwa ajili ya jina lako,+ wakisema,  ‘Tukipatwa na msiba, upanga, hukumu kali, au ugonjwa hatari, au njaa, na tusimame mbele ya nyumba hii na mbele zako (kwa maana jina lako limo katika nyumba hii)+ na kukulilia utusaidie katika taabu yetu, nawe usikie na kutuokoa.’+ 10  Sasa tazama, ndio hawa wanaume wa Amoni, Moabu, na eneo lenye milima la Seiri,+ ambao hukuwaruhusu Waisraeli wawavamie walipotoka nchini Misri. Waligeuka na kwenda mbali nao na hawakuwaangamiza.+ 11  Sasa wanatulipa kwa kuja kutufukuza kutoka katika miliki yako uliyotupatia iwe urithi wetu.+ 12  Ee Mungu wetu, je, hutatekeleza hukumu dhidi yao?+ Kwa maana hatuna nguvu mbele ya umati huu mkubwa unaokuja kutushambulia; nasi hatujui tunalopaswa kufanya,+ lakini macho yetu yanakutazama wewe.”+ 13  Wakati huo, watu wote wa Yuda walikuwa wamesimama mbele za Yehova, pamoja na watoto wao wadogo, wake zao, na wana wao. 14  Ndipo katikati ya kutaniko, roho ya Yehova ikamjia Yahazieli mwana wa Zekaria mwana wa Benaya mwana wa Yeieli mwana wa Matania, Mlawi wa wana wa Asafu. 15  Akasema: “Sikilizeni kwa makini, enyi watu wote wa Yuda nanyi wakaaji wa Yerusalemu na Mfalme Yehoshafati! Yehova anawaambia hivi: ‘Msiogope wala msihofu kwa sababu ya umati huu mkubwa, kwa maana vita si vyenu bali ni vya Mungu.+ 16  Kesho shukeni kukabiliana nao. Watakuwa wakipanda kupitia njia ya Sisi, nanyi mtawakuta mwishoni mwa bonde* kabla ya nyika ya Yerueli. 17  Hamtahitaji kupigana vita hivi. Simameni mahali penu, simameni tuli,+ muuone wokovu wa Yehova kwa ajili yenu.*+ Enyi watu wa Yuda na Yerusalemu, msiogope wala msihofu.+ Kesho nendeni mkakabiliane nao, na Yehova atakuwa pamoja nanyi.’”+ 18  Mara moja Yehoshafati akainama chini kifudifudi, na watu wote wa Yuda na wakaaji wa Yerusalemu wakaanguka chini mbele za Yehova ili kumwabudu Yehova. 19  Kisha Walawi waliokuwa wazao wa Wakohathi+ na wazao wa Wakora wakasimama ili kumsifu Yehova Mungu wa Israeli kwa sauti kubwa sana.+ 20  Kesho yake, wakaamka asubuhi na mapema na kwenda katika nyika ya Tekoa.+ Walipokuwa wakienda, Yehoshafati akasimama na kusema: “Nisikilizeni, enyi watu wa Yuda nanyi wakaaji wa Yerusalemu! Iweni na imani katika Yehova Mungu wenu ili mweze kusimama imara.* Iweni na imani katika manabii wake,+ nanyi mtafanikiwa.” 21  Baada ya kushauriana na watu, aliwaweka wanaume ili wamwimbie+ Yehova na kumsifu wakiwa wamevaa mavazi matakatifu huku wakiwatangulia wanaume wenye silaha, wakisema: “Mshukuruni Yehova, kwa maana upendo wake mshikamanifu unadumu milele.”+ 22  Walipoanza kuimba kwa shangwe nyimbo za sifa, Yehova akawaweka watu wawavizie wanaume wa Amoni, Moabu, na eneo lenye milima la Seiri waliokuwa wakivamia Yuda, nao wakaangamizana wenyewe kwa wenyewe.+ 23  Na Waamoni na Wamoabu wakageuka na kuwashambulia wakaaji wa eneo lenye milima la Seiri+ ili wawaue na kuwaangamiza kabisa; na baada ya kuwamaliza wakaaji wa Seiri, wakasaidiana kuangamizana wao kwa wao.+ 24  Lakini watu wa Yuda walipofika kwenye mnara wa mlinzi wa nyikani+ na kutazama umati huo, waliona maiti zao zikiwa zimetapakaa ardhini;+ hakuna yeyote aliyeponyoka. 25  Basi Yehoshafati na watu wake wakaja kuchukua nyara kutoka kwao, wakapata vitu vingi sana, mavazi, na vitu vyenye kutamanika, ambavyo waliwavua mpaka waliposhindwa kubeba zaidi.+ Walichukua nyara hizo kwa siku tatu, kwa maana zilikuwa nyingi sana. 26  Siku ya nne walikusanyika pamoja katika Bonde la* Beraka, kwa maana walimsifu* Yehova huko. Ndiyo sababu tangu siku hiyo walipaita mahali hapo Bonde la Beraka.*+ 27  Kisha watu wote wa Yuda na Yerusalemu, wakiongozwa na Yehoshafati, wakarudi Yerusalemu wakishangilia, kwa maana Yehova alikuwa amewafanya washangilie dhidi ya maadui wao.+ 28  Basi wakaingia Yerusalemu wakiwa na vinanda, vinubi,+ na tarumbeta+ na kwenda katika nyumba ya Yehova.+ 29  Na falme zote za nchi mbalimbali ziliposikia kwamba Yehova alikuwa amepigana na maadui wa Israeli zilishikwa na hofu ya Mungu.+ 30  Kwa hiyo ufalme wa Yehoshafati haukuwa na usumbufu wowote, na Mungu wake akaendelea kumpumzisha pande zote.+ 31  Na Yehoshafati akaendelea kutawala Yuda. Alikuwa na umri wa miaka 35 alipoanza kutawala, naye alitawala kwa miaka 25 huko Yerusalemu. Mama yake aliitwa Azuba binti ya Shilhi.+ 32  Aliendelea kutembea katika njia ya Asa baba yake.+ Hakugeuka kutoka katika njia hiyo, naye alitenda yaliyokuwa sawa machoni pa Yehova.+ 33  Hata hivyo, mahali pa juu hapakuondolewa,+ na bado watu hawakuwa wameutayarisha moyo wao kwa ajili ya Mungu wa mababu zao.+ 34  Na mambo mengine katika historia ya Yehoshafati, kuanzia mwanzo mpaka mwisho, yameandikwa katika maandishi ya Yehu+ mwana wa Hanani,+ yaliyotiwa katika Kitabu cha Wafalme wa Israeli. 35  Baada ya hayo Mfalme Yehoshafati wa Yuda akaungana na Mfalme Ahazia wa Israeli, aliyetenda uovu.+ 36  Kwa hiyo akashirikiana naye katika kutengeneza meli za kwenda Tarshishi,+ walizitengenezea kule Esion-geberi.+ 37  Hata hivyo, Eliezeri mwana wa Dodavahu wa Maresha alitoa unabii dhidi ya Yehoshafati, akisema: “Kwa sababu umeungana na Ahazia, Yehova ataharibu kazi zako.”+ Basi meli hizo zikavunjika,+ kwa hiyo hazikuweza kwenda Tarshishi.

Maelezo ya Chini

Au labda, “Wameuni.”
Inaonekana ni Bahari ya Chumvi.
Tnn., “akauelekeza uso wake.”
Tnn., “mbegu ya.”
Au “korongo.”
Au “muone jinsi Yehova atakavyowaokoa.”
Au “kuvumilia.”
Au “Nchi Tambarare ya Chini ya.”
Tnn., “walimbariki.”
Maana yake “Baraka.”