Kitabu cha Pili cha Mambo ya Nyakati 21:1-20

  • Yehoramu, mfalme wa Yuda (1-11)

  • Barua kutoka kwa Eliya (12-15)

  • Mwisho mbaya wa Yehoramu (16-20)

21  Kisha Yehoshafati akafa na kuzikwa pamoja na mababu zake katika Jiji la Daudi; na Yehoramu mwanawe akawa mfalme baada yake.+  Ndugu zake, yaani, wana wa Yehoshafati, walikuwa Azaria, Yehieli, Zekaria, Azaria, Mikaeli, na Shefatia; hao wote walikuwa wana wa Mfalme Yehoshafati wa Israeli.  Na baba yao alikuwa amewapa zawadi nyingi za fedha na dhahabu, na vitu vyenye thamani, pamoja na majiji yenye ngome kule Yuda;+ lakini alimpa Yehoramu ufalme,+ kwa sababu yeye ndiye aliyekuwa mzaliwa wa kwanza.  Yehoramu alipochukua mamlaka ya ufalme wa baba yake, aliimarisha mamlaka yake kwa kuwaua ndugu zake wote+ kwa upanga, na pia baadhi ya wakuu wa Israeli.  Yehoramu alikuwa na umri wa miaka 32 alipoanza kutawala, naye alitawala huko Yerusalemu kwa miaka minane.+  Alitembea katika njia ya wafalme wa Israeli,+ kama walivyofanya watu wa nyumba ya Ahabu, kwa maana alikuwa amemwoa binti ya Ahabu;+ na Yehoramu akaendelea kutenda maovu machoni pa Yehova.  Lakini Yehova hakutaka kuiangamiza nyumba ya Daudi kwa sababu ya agano alilokuwa amefanya pamoja na Daudi,+ kwa maana alikuwa ameahidi kumpa taa, yeye na wanawe, sikuzote.+  Katika siku zake, Waedomu waliasi nchi ya Yuda+ na kujichagulia mfalme wao wenyewe.+  Basi Yehoramu na makamanda wake wakavuka na magari yake yote ya vita, naye akaondoka usiku na kuwashinda Waedomu waliokuwa wamemzingira yeye na makamanda wake wa magari ya vita. 10  Lakini tangu siku hiyo Waedomu wameendelea kuiasi nchi ya Yuda. Watu wa Libna+ pia walimwasi Yehoramu wakati huo, kwa sababu alikuwa amemwacha Yehova Mungu wa mababu zake.+ 11  Alikuwa amejenga pia mahali pa juu+ kwenye milima ya Yuda, akasababisha wakaaji wa Yerusalemu wafanye ukahaba wa kiroho, naye akawapotosha watu wa Yuda. 12  Baadaye alipokea barua kutoka kwa nabii Eliya+ iliyosema: “Yehova Mungu wa Daudi babu yako anasema, ‘Hujafuata* njia za Yehoshafati baba yako+ wala njia za Mfalme Asa+ wa Yuda. 13  Lakini unafuata njia ya wafalme wa Israeli+ na kusababisha watu wa Yuda na wakaaji wa Yerusalemu wafanye ukahaba wa kiroho+ kama ukahaba uliofanywa na nyumba ya Ahabu,+ na hata uliwaua ndugu zako mwenyewe,+ watu wa nyumba ya baba yako, waliokuwa bora kuliko wewe. 14  Kwa hiyo, Yehova anawaletea pigo kubwa watu wako, wana wako, wake zako, na mali zako zote. 15  Nawe utashikwa na magonjwa mengi, kutia ndani ugonjwa wa matumbo, mpaka ugonjwa huo utakaposababisha matumbo yako yatoke nje, siku baada ya siku.’” 16  Kisha Yehova akawachochea*+ Wafilisti+ na Waarabu+ walioishi karibu na Waethiopia ili wamshambulie Yehoramu. 17  Basi wakaivamia Yuda, wakaingia humo kwa nguvu na kuchukua mali zote zilizokuwa katika nyumba ya* mfalme,+ na pia wanawe na wake zake; Yehoahazi,*+ mwanawe wa mwisho, ndiye mwana pekee aliyebaki pamoja naye. 18  Na baada ya mambo hayo yote, Yehova akampiga kwa ugonjwa wa matumbo usioweza kupona.+ 19  Wakati fulani baadaye, baada ya miaka miwili kamili kupita, matumbo yake yalitoka nje kwa sababu ya ugonjwa huo, naye akafa alipokuwa akiteseka sana kwa sababu ya ugonjwa huo; na watu wake hawakuwasha moto kwa ajili yake kama ule uliowashwa kwa ajili ya mababu zake.+ 20  Alikuwa na umri wa miaka 32 alipoanza kutawala, naye alitawala kwa miaka 8 huko Yerusalemu. Hakuna mtu yeyote aliyesikitishwa na kifo chake. Basi wakamzika katika Jiji la Daudi,+ lakini si katika makaburi ya wafalme.+

Maelezo ya Chini

Tnn., “Hujatembea katika.”
Tnn., “akaichochea roho ya.”
Au “jumba la.”
Anaitwa pia Ahazia.