Kitabu cha Pili cha Mambo ya Nyakati 24:1-27

  • Utawala wa Yehoashi (1-3)

  • Yehoashi arekebisha hekalu (4-14)

  • Uasi imani wa Yehoashi (15-22)

  • Yehoashi auawa (23-27)

24  Yehoashi alikuwa na umri wa miaka saba alipoanza kutawala,+ naye alitawala kwa miaka 40 huko Yerusalemu. Mama yake aliitwa Sibia kutoka Beer-sheba.+  Yehoashi aliendelea kutenda yaliyokuwa sawa machoni pa Yehova sikuzote za kuhani Yehoyada.+  Yehoyada alimchagulia wake wawili, naye akazaa wana na mabinti.  Baadaye Yehoashi alitamani moyoni mwake kuirekebisha nyumba ya Yehova.+  Kwa hiyo akawakusanya makuhani na Walawi na kuwaambia: “Nendeni kwenye majiji ya Yuda mkusanye kutoka kwa Waisraeli wote pesa za kurekebisha nyumba ya Mungu+ mwaka baada ya mwaka; nanyi mnapaswa kushughulikia jambo hili haraka.” Lakini Walawi hawakulishughulikia jambo hilo haraka.+  Kwa hiyo, mfalme akamwita mkuu Yehoyada na kumuuliza:+ “Kwa nini hukuwaamuru Walawi walete kutoka Yuda na Yerusalemu kodi takatifu iliyoagizwa na Musa+ mtumishi wa Yehova, ile kodi takatifu ya kutaniko la Israeli, kwa ajili ya hema la Ushahidi?+  Kwa maana wana wa Athalia,+ yule mwanamke mwovu, walikuwa wamevunja na kuingia ndani ya nyumba ya Mungu wa kweli,+ nao walikuwa wametumia vitu vyote vitakatifu vya nyumba ya Yehova kwa ajili ya Mabaali.”  Kisha, kwa agizo la mfalme, sanduku+ lilitengenezwa na kuwekwa nje kwenye lango la nyumba ya Yehova.+  Halafu tangazo likatolewa katika nchi yote ya Yuda na Yerusalemu kwamba watu wamletee Yehova kodi takatifu+ ambayo Musa mtumishi wa Mungu wa kweli alikuwa amewaagiza Waisraeli nyikani. 10  Wakuu wote na watu wote wakashangilia,+ nao wakaendelea kuleta michango na kuitumbukiza katika sanduku hilo mpaka lilipojaa.* 11  Kila mara Walawi walipoleta sanduku hilo ili mfalme akabidhiwe, na maofisa walipoona kwamba kulikuwa na pesa nyingi ndani yake, mwandishi wa mfalme na mwakilishi wa kuhani mkuu walikuja na kuzitoa pesa sandukuni,+ kisha walilirudisha mahali pake. Hivyo ndivyo walivyofanya siku baada ya siku, nao walikusanya pesa nyingi. 12  Kisha mfalme pamoja na Yehoyada waliwapa wale waliosimamia kazi katika utumishi wa nyumba ya Yehova, na wasimamizi hao waliwaajiri watu waliokata mawe na mafundi wa kurekebisha nyumba ya Yehova,+ na pia mafundi wa chuma na shaba ili kuirekebisha nyumba ya Yehova. 13  Na wasimamizi hao wakaianzisha kazi, na kazi hiyo ya kurekebisha ikasonga mbele chini ya usimamizi wao, nao wakairudisha nyumba ya Mungu wa kweli katika hali yake inayofaa na kuiimarisha. 14  Na mara tu walipomaliza, walimletea mfalme na Yehoyada pesa zilizobaki, nao wakazitumia kutengeneza vyombo vya nyumba ya Yehova, vyombo vya huduma na vya kutolea dhabihu na vikombe na vyombo vya dhahabu na vya fedha.+ Nao walitoa kwa ukawaida dhabihu za kuteketezwa + katika nyumba ya Yehova sikuzote za Yehoyada. 15  Yehoyada alizeeka na kufa baada ya kuishi maisha marefu na yenye kuridhisha; alikuwa na umri wa miaka 130 alipokufa. 16  Basi wakamzika katika Jiji la Daudi pamoja na wafalme,+ kwa sababu alikuwa ametenda mema katika Israeli+ kwa ajili ya Mungu wa kweli na nyumba Yake. 17  Baada ya kifo cha Yehoyada, wakuu wa Yuda walikuja na kumwinamia mfalme, na mfalme akawasikiliza. 18  Waliiacha nyumba ya Yehova Mungu wa mababu zao na kuanza kuabudu miti mitakatifu* na sanamu, hivi kwamba hasira ya Mungu ikaja* dhidi ya Yuda na Yerusalemu kwa sababu ya hatia yao. 19  Aliendelea kuwatuma manabii miongoni mwao ili wawarudishe kwa Yehova, nao waliendelea kuwaonya* lakini walikataa kusikiliza.+ 20  Roho ya Mungu ikamjia* Zekaria mwana wa kuhani Yehoyada,+ naye akasimama mahali palipo juu mbele ya watu na kuwaambia: “Mungu wa kweli anasema hivi: ‘Kwa nini mnazivunja amri za Yehova? Hamtafanikiwa! Kwa sababu mmemwacha Yehova, yeye naye, atawaacha ninyi.’”+ 21  Lakini walipanga njama dhidi yake,+ wakampiga mawe katika ua wa nyumba ya Yehova, kwa agizo la mfalme.+ 22  Kwa hiyo Mfalme Yehoashi hakukumbuka upendo mshikamanifu ambao Yehoyada baba yake* alimtendea, alimuua mwanawe, ambaye alisema hivi alipokuwa akifa: “Yehova na ashughulikie jambo hili na kukulipiza kisasi.”+ 23  Mwanzoni mwa mwaka, jeshi la Siria lilikuja kumshambulia Yehoashi, likavamia Yuda na Yerusalemu.+ Kisha likawaua wakuu wote+ wa watu na kupeleka nyara zao zote kwa mfalme wa Damasko. 24  Kwa maana ingawa jeshi la Wasiria lililovamia lilikuwa na wanaume wachache, Yehova alitia mikononi mwao jeshi kubwa sana la watu wa Yuda na Yerusalemu+ kwa sababu walikuwa wamemwacha Yehova Mungu wa mababu zao; kwa hiyo wakatekeleza* hukumu dhidi ya Yehoashi. 25  Na walipoondoka katika nchi yake (kwa maana walimwacha akiwa amejeruhiwa vibaya*), watumishi wake mwenyewe walipanga njama dhidi yake kwa sababu alikuwa amemwaga damu ya wana* wa kuhani Yehoyada.+ Walimuua katika kitanda chake mwenyewe.+ Basi akafa na kuzikwa katika Jiji la Daudi,+ lakini hawakumzika katika makaburi ya wafalme.+ 26  Hawa ndio waliopanga njama+ dhidi yake: Zabadi mwana wa Shimeathi mwanamke Mwamoni na Yehozabadi mwana wa Shimrithi mwanamke Mmoabu. 27  Na kuhusu wanawe na mambo mengi yaliyotangazwa dhidi yake+ na pia kazi ya kurekebisha* nyumba ya Mungu wa kweli,+ mambo hayo yote yameandikwa katika maandishi ya* Kitabu cha Wafalme. Na Amazia mwanawe akawa mfalme baada yake.

Maelezo ya Chini

Au labda, “wote walipokuwa wametoa.”
Tnn., “kulikuwa na hasira.”
Angalia Kamusi.
Au “kutoa ushahidi dhidi yao.”
Au “ikamfunika.”
Yaani, baba ya Zekaria.
Yaani, Wasiria.
Au “akiwa na magonjwa mengi.”
Au “mwana.” Huenda wingi unaonyesha utukufu.
Tnn., “kuweka msingi wa.”
Au “ufafanuzi wa; maelezo ya.”