Kitabu cha Pili cha Mambo ya Nyakati 25:1-28

  • Amazia, mfalme wa Yuda (1-4)

  • Apigana vita na Edomu (5-13)

  • Amazia aabudu sanamu (14-16)

  • Apigana vita na Mfalme Yehoashi wa Israeli (17-24)

  • Kifo cha Amazia (25-28)

25  Amazia alikuwa na umri wa miaka 25 alipoanza kutawala, naye alitawala kwa miaka 29 huko Yerusalemu. Mama yake aliitwa Yehoadani wa Yerusalemu.+  Aliendelea kutenda yaliyokuwa sawa machoni pa Yehova, lakini si kwa moyo kamili.  Mara tu ufalme ulipoimarika kabisa mikononi mwake, aliwaua watumishi wake waliomuua mfalme, baba yake.+  Lakini hakuwaua wana wao, kwa maana alitenda kulingana na mambo yaliyoandikwa katika Sheria, katika kitabu cha Musa, ambamo Yehova aliamuru hivi: “Akina baba hawapaswi kuuawa kwa sababu ya wana wao, na wana hawapaswi kuuawa kwa sababu ya baba zao; lakini kila mtu anapaswa kuuawa kwa sababu ya dhambi yake mwenyewe.”+  Na Amazia akawakusanya pamoja watu wa Yuda na kuwaagiza wasimame kulingana na koo zao,* chini ya wakuu wa maelfu na chini ya wakuu wa mamia kwa ajili ya watu wote wa Yuda na Benjamini.+ Akawaandikisha waliokuwa na umri wa miaka 20 na zaidi,+ akapata kwamba walikuwa mashujaa 300,000 waliozoezwa* kwa ajili ya utumishi wa kijeshi, walioweza kutumia mkuki na ngao kubwa.  Isitoshe, alikodi mashujaa hodari 100,000 kutoka Israeli kwa talanta 100 za fedha.*  Lakini mtu fulani wa Mungu wa kweli akamjia na kumwambia: “Ee mfalme, usiruhusu jeshi la Israeli liende pamoja nawe, kwa maana Yehova hayuko pamoja na Waisraeli,+ hayuko pamoja na Mwefraimu yeyote.  Lakini nenda peke yako, utende, na uwe jasiri vitani. Usipofanya hivyo, Mungu wa kweli anaweza kukufanya ujikwae mbele ya adui, kwa maana Mungu ana nguvu za kusaidia+ na za kusababisha mtu ajikwae.”  Ndipo Amazia akamuuliza hivi mtu wa Mungu wa kweli: “Lakini vipi kuhusu zile talanta 100 ambazo nimewapa wanajeshi wa Israeli?” Mtu wa Mungu wa kweli akamjibu: “Yehova anaweza kukupa nyingi zaidi kuliko hizo.”+ 10  Basi Amazia akawaagiza wanajeshi waliokuwa wamekuja kwake kutoka Efraimu waende zao, warudi kwao. Hata hivyo, waliwakasirikia sana watu wa Yuda, basi wakarudi kwao wakiwa wamekasirika sana. 11  Kisha Amazia akajipa ujasiri na kuwaongoza wanajeshi wake mwenyewe kwenye Bonde la Chumvi,+ akawaua wanaume 10,000 wa Seiri.+ 12  Na wanaume wa Yuda wakawateka watu 10,000 wakiwa hai. Wakawapandisha juu ya mwamba na kuwatupa chini kutoka kwenye mwamba huo, na wote wakavunjika vipandevipande. 13  Lakini wanajeshi ambao Amazia aliwaambia warudi, wasiende pamoja naye vitani,+ walikuwa wakivamia majiji ya Yuda, kuanzia Samaria+ mpaka Beth-horoni;+ waliwaua watu 3,000 katika majiji hayo na kuchukua nyara nyingi sana. 14  Lakini Amazia aliporudi baada ya kuwaua Waedomu, alileta miungu ya watu wa Seiri na kuisimamisha ili iwe miungu yake mwenyewe,+ naye akaanza kuinama mbele ya miungu hiyo na kuifukizia moshi wa dhabihu. 15  Kwa hiyo Yehova akamkasirikia sana Amazia, akamtuma nabii ambaye alimwambia: “Kwa nini unaifuata miungu ya mataifa ambayo haikuwaokoa watu wake kutoka mikononi mwako?”+ 16  Nabii huyo alipokuwa akizungumza naye, mfalme akamwambia: “Je, tulikuweka uwe mshauri wa mfalme?+ Nyamaza!+ Kwa nini unataka kuuawa?” Ndipo nabii huyo akanyamaza, lakini akasema: “Najua kwamba Mungu ameamua kukuangamiza, kwa sababu umetenda hivyo na hujasikiliza ushauri wangu.”+ 17  Baada ya kushauriana na washauri wake, Mfalme Amazia wa Yuda alituma ujumbe kwa Yehoashi mwana wa Yehoahazi mwana wa Yehu mfalme wa Israeli akisema: “Njoo, tupambane vitani.”*+ 18  Mfalme Yehoashi wa Israeli akatuma ujumbe huu kwa Mfalme Amazia wa Yuda: “Gugu lenye miiba kule Lebanoni lilituma ujumbe huu kwa mwerezi huko Lebanoni, ‘Mpe mwanangu binti yako awe mke wake.’ Hata hivyo, mnyama wa mwituni wa Lebanoni akapita karibu na kulikanyaga-kanyaga gugu hilo lenye miiba. 19  Umesema, ‘Tazama! Nimewaangamiza Waedomu.’+ Kwa hiyo moyo wako umekuwa na kiburi, unataka utukuzwe. Lakini sasa kaa katika nyumba yako mwenyewe.* Kwa nini utafute msiba kisha uanguke, na kuwaangusha pia watu wa Yuda?” 20  Lakini Amazia hakusikiliza,+ kwa sababu Mungu wa kweli alikusudia kuwatia mikononi mwa adui,+ kwa sababu walikuwa wameifuata miungu ya Edomu.+ 21  Basi Mfalme Yehoashi wa Israeli akapanda kwenda huko, naye akapambana vitani na Mfalme Amazia wa Yuda huko Beth-shemeshi,+ jiji la Yuda. 22  Watu wa Yuda wakashindwa na Waisraeli, kwa hiyo kila mmoja akakimbilia nyumbani kwake.* 23  Mfalme Yehoashi wa Israeli akamkamata Mfalme Amazia wa Yuda, mwana wa Yehoashi mwana wa Yehoahazi,* huko Beth-shemeshi. Kisha akamleta Yerusalemu, naye akabomoa ukuta wa Yerusalemu kuanzia Lango la Efraimu+ mpaka Lango la Pembeni,+ urefu wa mikono 400.* 24  Akachukua dhahabu yote na fedha na vitu vyote vilivyokuwa katika nyumba ya Mungu wa kweli chini ya Obed-edomu na katika hazina za nyumba ya* mfalme,+ na pia akachukua mateka. Kisha akarudi Samaria. 25  Amazia+ mwana wa Yehoashi mfalme wa Yuda aliendelea kuishi kwa miaka 15 baada ya kifo cha Yehoashi+ mwana wa Yehoahazi mfalme wa Israeli.+ 26  Na mambo mengine katika historia ya Amazia, kuanzia mwanzo mpaka mwisho, je, hayajaandikwa katika Kitabu cha Wafalme wa Yuda na wa Israeli? 27  Kuanzia wakati ambapo Amazia aligeuka na kuacha kumfuata Yehova, walipanga njama+ dhidi yake huko Yerusalemu, akakimbilia Lakishi, lakini wakawatuma watu wamfuatie huko Lakishi, nao wakamuua huko. 28  Kwa hiyo wakambeba juu ya farasi na kumrudisha, wakamzika pamoja na mababu zake katika jiji la Yuda.

Maelezo ya Chini

Yaani, ukoo wa upande wa baba.
Tnn., “waliochaguliwa.”
Talanta moja ilikuwa na uzito wa kilogramu 34.2. Angalia Nyongeza B14.
Au “tukutane uso kwa uso.”
Au “jumba lako mwenyewe la kifalme.”
Tnn., “katika hema lake.”
Karibu mita 178 (futi 584). Angalia Nyongeza B14.
Anaitwa pia Ahazia.
Au “jumba la.”