Kitabu cha Pili cha Mambo ya Nyakati 26:1-23

  • Uzia, mfalme wa Yuda (1-5)

  • Kampeni za kivita za Uzia (6-15)

  • Uzia mwenye kiburi apigwa na ukoma (16-21)

  • Kifo cha Uzia (22, 23)

26  Kisha watu wote wa Yuda wakamchukua Uzia,+ aliyekuwa na umri wa miaka 16, wakamweka kuwa mfalme baada ya Amazia baba yake.+  Alijenga upya jiji la Elothi+ na kulirudisha kwa Yuda baada ya mfalme* kuzikwa pamoja na mababu zake.+  Uzia+ alikuwa na umri wa miaka 16 alipoanza kutawala, naye alitawala kwa miaka 52 huko Yerusalemu. Mama yake aliitwa Yekolia wa Yerusalemu.+  Aliendelea kutenda yaliyokuwa sawa machoni pa Yehova, kama Amazia baba yake alivyotenda.+  Naye aliendelea kumtafuta Mungu katika siku za Zekaria, aliyemfundisha kumwogopa Mungu wa kweli. Wakati alipokuwa akimtafuta Yehova, Mungu wa kweli alimfanikisha.+  Alienda kupigana na Wafilisti+ na kuupenya ukuta wa Gathi,+ ukuta wa Yabne,+ na ukuta wa Ashdodi.+ Kisha akajenga majiji katika eneo la Ashdodi na miongoni mwa Wafilisti.  Mungu wa kweli aliendelea kumsaidia kuwashinda Wafilisti, Waarabu+ waliokuwa wakiishi Gurbaali, na Wameunimu.  Waamoni+ wakaanza kumpa Uzia ushuru. Hatimaye umaarufu wake ukaenea mpaka Misri, kwa maana alipata nguvu nyingi sana.  Isitoshe, Uzia alijenga minara+ Yerusalemu karibu na Lango la Pembeni,+ Lango la Bondeni,+ na Nguzo ya Kutegemeza Ukuta, naye akaiimarisha. 10  Pia, alijenga minara+ nyikani na kuchimba* matangi mengi ya maji (kwa maana alikuwa na mifugo mingi sana); alifanya hivyo pia katika Shefela na katika nchi tambarare ya juu. Alikuwa na wakulima na watunzaji wa mizabibu milimani na kule Karmeli, kwa maana alipenda kilimo. 11  Zaidi ya hayo, Uzia akawa na jeshi lililojihami kwa ajili ya vita. Wanajeshi hao walienda vitani, wakiwa wamepangwa katika vikundi. Walihesabiwa na kuandikishwa+ na mwandishi Yeieli+ na ofisa aliyeitwa Maaseya, chini ya amri ya Hanania, mmoja wa wakuu wa mfalme. 12  Idadi kamili ya viongozi wa koo* waliowaongoza mashujaa hao hodari ilikuwa 2,600. 13  Wanajeshi waliokuwa chini ya amri yao walikuwa 307,500, wanaume waliokuwa tayari kwa ajili ya vita, jeshi lenye nguvu la kumsaidia mfalme kupigana na maadui.+ 14  Uzia alilihami jeshi lote kwa ngao, mikuki,+ kofia, makoti ya vita,+ pinde, na mawe ya kombeo.+ 15  Pia, alitengeneza mitambo ya vita huko Yerusalemu iliyobuniwa na wahandisi; iliwekwa kwenye minara+ na kwenye pembe za kuta, nayo ilikuwa na uwezo wa kurusha mishale na mawe makubwa. Basi umaarufu wake ukaenea kwa mapana na marefu, kwa maana alisaidiwa sana akawa na nguvu. 16  Hata hivyo, mara tu alipokuwa na nguvu, moyo wake ukawa na kiburi ambacho kilisababisha aangamie, naye alikosa kutenda kwa uaminifu kumwelekea Yehova Mungu wake kwa kuwa aliingia katika hekalu la Yehova ili kufukiza uvumba kwenye madhabahu ya uvumba.+ 17  Mara moja kuhani Azaria na makuhani wengine 80 wa Yehova wenye ujasiri wakamfuata humo. 18  Wakamkabili Mfalme Uzia na kumwambia: “Si vyema kwako, Uzia, kumfukizia Yehova uvumba!+ Ni makuhani tu wanaopaswa kufukiza uvumba, kwa maana wao ni wazao wa Haruni,+ waliotakaswa. Toka mahali patakatifu, kwa maana hujatenda kwa uaminifu, na kwa sababu hiyo hutapokea utukufu wowote kutoka kwa Yehova Mungu.” 19  Lakini Uzia, aliyekuwa ameshika chetezo mkononi, akawaka hasira;+ na hasira yake ilipokuwa imewaka dhidi ya makuhani, ukoma+ ukatokea kwenye paji lake la uso mbele ya makuhani katika nyumba ya Yehova karibu na madhabahu ya uvumba. 20  Azaria mkuu wa makuhani na makuhani wote walipogeuka na kumtazama, waliona kwamba alikuwa amepigwa na ukoma kwenye paji la uso! Kwa hiyo wakamtoa humo haraka, naye mwenyewe akatoka nje haraka, kwa sababu Yehova alikuwa amemletea pigo. 21  Mfalme Uzia aliendelea kuwa na ukoma mpaka siku aliyokufa, naye aliendelea kukaa katika nyumba iliyotengwa akiwa mtu mwenye ukoma,+ kwa sababu alizuiwa kuingia katika nyumba ya Yehova. Yothamu mwanawe ndiye aliyesimamia nyumba ya* mfalme, akiwahukumu watu nchini.+ 22  Na mambo mengine katika historia ya Uzia, kuanzia mwanzo mpaka mwisho, yaliandikwa na nabii Isaya+ mwana wa Amozi. 23  Kisha Uzia akafa na kuzikwa pamoja na mababu zake, lakini alizikwa katika kiwanja cha kuzikia kilichokuwa mali ya wafalme, kwa maana walisema: “Ni mtu mwenye ukoma.” Na Yothamu mwanawe+ akawa mfalme baada yake.

Maelezo ya Chini

Yaani, Amazia baba yake.
Inaelekea alichimba kwenye miamba.
Yaani, ukoo wa upande wa baba.
Au “jumba la.”