Kitabu cha Pili cha Mambo ya Nyakati 28:1-27

  • Ahazi, mfalme wa Yuda (1-4)

  • Ashindwa na Wasiria na Waisraeli (5-8)

  • Odedi awaonya Waisraeli (9-15)

  • Watu wa Yuda wanyenyekezwa (16-19)

  • Ahazi aabudu sanamu; kifo chake (20-27)

28  Ahazi+ alikuwa na umri wa miaka 20 alipoanza kutawala, naye alitawala kwa miaka 16 huko Yerusalemu. Hakutenda yaliyokuwa sawa machoni pa Yehova kama alivyotenda Daudi babu yake.+  Badala yake, alitembea katika njia za wafalme wa Israeli,+ na hata alitengeneza sanamu za chuma*+ za Mabaali.  Isitoshe, alifukiza moshi wa dhabihu katika Bonde la Mwana wa Hinomu* na kuwateketeza wanawe motoni,+ akifuata mazoea yenye kuchukiza ya mataifa+ ambayo Yehova alikuwa ameyafukuza kutoka mbele ya Waisraeli.  Aliendelea pia kutoa dhabihu na kufukiza moshi wa dhabihu mahali pa juu,+ kwenye vilima, na chini ya kila mti wenye majani mengi.+  Kwa hiyo Yehova Mungu wake akamtia mikononi mwa mfalme wa Siria,+ hivi kwamba wakamshinda, wakachukua mateka wengi, na kuwapeleka Damasko.+ Alitiwa pia mikononi mwa mfalme wa Israeli, ambaye aliwaua watu wake wengi.  Kwa maana Peka+ mwana wa Remalia aliwaua watu 120,000 huko Yuda katika siku moja, wote walikuwa wanaume jasiri, kwa sababu Waisraeli walikuwa wamemwacha Yehova Mungu wa mababu zao.+  Na Zikri, shujaa Mwefraimu, alimuua Maaseya mwana wa mfalme na Azrikamu aliyekuwa msimamizi wa jumba la mfalme,* na Elkana aliyekuwa wa pili baada ya mfalme.  Zaidi ya hayo, Waisraeli waliwachukua mateka ndugu zao 200,000—wanawake, wana, na mabinti; walichukua pia nyara nyingi na kuzipeleka Samaria.+  Lakini nabii wa Yehova aliyeitwa Odedi alikuwa huko. Alienda kukutana na wanajeshi waliokuwa wakija Samaria na kuwaambia: “Tazameni! Yehova Mungu wa mababu zenu aliwatia watu wa Yuda mikononi mwenu kwa sababu walimkasirisha,+ nanyi mliwaua kwa hasira kali ambayo imefika mpaka mbinguni. 10  Na sasa mnakusudia kuwafanya watu wa Yuda na Yerusalemu wawe watumishi wenu wa kiume na wa kike.+ Lakini, je, ninyi pia hamna hatia mbele za Yehova Mungu wenu? 11  Sasa nisikilizeni, warudisheni ndugu zenu mliowachukua mateka, kwa maana hasira ya Yehova inayowaka iko dhidi yenu.” 12  Ndipo baadhi ya wakuu wa Waefraimu, Azaria mwana wa Yehohanani, Berekia mwana wa Meshilemothi, Yehizkia mwana wa Shalumu, na Amasa mwana wa Hadlai, wakawakabili watu waliokuwa wakitoka vitani, 13  wakawaambia: “Msiwalete mateka humu, kwa maana hilo litatufanya tuwe na hatia mbele za Yehova. Mnalokusudia kufanya litaongeza dhambi zetu na hatia yetu, kwa maana tayari tuna hatia kubwa na kuna hasira inayowaka dhidi ya Israeli.” 14  Basi wanajeshi hao wenye silaha wakawapa wakuu na kutaniko lote mateka na nyara+ walizochukua. 15  Kisha wanaume waliokuwa wamechaguliwa na kutajwa majina wakaenda na kuwachukua mateka, nao wakachukua mavazi kutoka katika zile nyara na kuwapa wote waliokuwa uchi. Basi wakawavika mavazi na kuwapa viatu, vyakula na vinywaji, na mafuta ya kujipaka. Zaidi ya hayo, waliwasafirisha kwa punda watu waliokuwa dhaifu na kuwapeleka kwa ndugu zao kule Yeriko, jiji la mitende. Kisha wakarudi Samaria. 16  Wakati huo Mfalme Ahazi aliwaomba wafalme wa Ashuru wamsaidie.+ 17  Na kwa mara nyingine tena Waedomu walivamia nchi ya Yuda, wakaishambulia na kuchukua mateka. 18  Wafilisti+ walivamia pia majiji ya Shefela+ na Negebu nchini Yuda na kuteka Beth-shemeshi,+ Aiyaloni,+ Gederothi, Soko na miji yake, Timna+ na miji yake, na Gimzo na miji yake; nao wakaanza kuishi humo. 19  Yehova aliwanyenyekeza watu wa Yuda kwa sababu ya Mfalme Ahazi wa Israeli, kwa maana aliwaacha watu wa Yuda watende watakavyo, na hivyo wakakosa kuwa waaminifu kwa Yehova kwa kiwango kikubwa. 20  Hatimaye Mfalme Tilgath-pilneseri+ wa Ashuru akaja kukabiliana naye na kumtesa+ badala ya kumtia nguvu. 21  Kwa maana Ahazi alikuwa amechukua kila kitu kilichokuwa katika nyumba ya Yehova na nyumba ya* mfalme+ na nyumba za wakuu na kumpa mfalme wa Ashuru kuwa zawadi; lakini hilo halikumsaidia kamwe. 22  Na wakati alipokuwa akiteseka, Mfalme Ahazi alikosa hata zaidi kuwa mwaminifu kwa Yehova. 23  Akaanza kuitolea dhabihu miungu ya Damasko+ iliyokuwa imemshinda,+ akasema: “Kwa sababu miungu ya wafalme wa Siria inawasaidia, nitaitolea dhabihu ili inisaidie.”+ Lakini miungu hiyo ilimfanya yeye na Waisraeli wote wajikwae. 24  Zaidi ya hayo, Ahazi alikusanya vyombo vya nyumba ya Mungu wa kweli; akavikata vipandevipande vyombo vya nyumba ya Mungu wa kweli,+ akaifunga milango ya nyumba ya Yehova,+ na kujitengenezea madhabahu katika kila pembe ya Yerusalemu. 25  Na katika majiji yote ya Yuda, alijenga mahali pa juu pa kuifukizia moshi wa dhabihu miungu mingine,+ akamkasirisha Yehova Mungu wa mababu zake. 26  Na mambo mengine katika historia yake, shughuli zake zote kuanzia mwanzo mpaka mwisho, yameandikwa katika Kitabu cha Wafalme wa Yuda na wa Israeli.+ 27  Kisha Ahazi akafa na kuzikwa pamoja na mababu zake jijini Yerusalemu, kwa maana hawakumpeleka kwenye makaburi ya wafalme wa Israeli.+ Na Hezekia mwanawe akawa mfalme baada yake.

Maelezo ya Chini

Au “sanamu za kuyeyushwa.”
Angalia Kamusi, “Gehena.”
Tnn., “nyumba.”
Au “jumba la.”