Kitabu cha Pili cha Mambo ya Nyakati 29:1-36

  • Hezekia, mfalme wa Yuda (1, 2)

  • Mabadiliko yaliyofanywa na Hezekia (3-11)

  • Hekalu latakaswa (12-19)

  • Utumishi wa hekaluni waanzishwa tena (20-36)

29  Hezekia+ alikuwa na umri wa miaka 25 alipoanza kutawala, naye alitawala kwa miaka 29 huko Yerusalemu. Mama yake aliitwa Abiya binti ya Zekaria.+  Aliendelea kutenda yaliyokuwa sawa machoni pa Yehova,+ kama alivyofanya Daudi babu yake.+  Katika mwaka wa kwanza wa utawala wake, mwezi wa kwanza, aliifungua milango ya nyumba ya Yehova na kuirekebisha.+  Kisha akawaleta makuhani na Walawi na kuwakusanya kwenye kiwanja kilichokuwa upande wa mashariki.  Akawaambia: “Nisikilizeni, enyi Walawi. Sasa jitakaseni+ na mwitakase nyumba ya Yehova Mungu wa mababu zenu, ondoeni kitu kichafu mahali patakatifu.+  Kwa maana baba zetu wamekosa uaminifu nao wametenda maovu machoni pa Yehova Mungu wetu.+ Walimwacha na kugeuza nyuso zao mbali na hema la ibada la Yehova na kumgeuzia mgongo.+  Pia, walifunga milango ya ukumbi+ na kuzima taa.+ Waliacha kufukiza uvumba+ na pia kumtolea Mungu wa Israeli dhabihu za kuteketezwa+ mahali patakatifu.  Kwa hiyo, ghadhabu ya Yehova ikaja dhidi ya watu wa Yuda na Yerusalemu,+ hivi kwamba akawafanya kuwa kitu cha kutisha na cha kushangaza na kitu cha kupigiwa mluzi,* kama mnavyoona kwa macho yenu wenyewe.+  Kwa hiyo mababu zetu waliuawa kwa upanga,+ na wana wetu, mabinti wetu, na wake zetu wakapelekwa utekwani kwa sababu ya mambo hayo.+ 10  Sasa ninatamani moyoni mwangu kufanya agano pamoja na Yehova Mungu wa Israeli,+ ili hasira yake inayowaka ituondokee. 11  Wanangu, huu si wakati wa kupuuza mambo,* kwa maana Yehova amewachagua ninyi msimame mbele zake, muwe wahudumu wake,+ na kufukiza moshi wa dhabihu zake.”+ 12  Ndipo Walawi wakasimama: Mahathi mwana wa Amasai na Yoeli mwana wa Azaria wa Wakohathi;+ kutoka kwa Wamerari,+ Kishi mwana wa Abdi na Azaria mwana wa Yehaleleli; kutoka kwa Wagershoni,+ Yoa mwana wa Zima na Edeni mwana wa Yoa; 13  kutoka kwa wana wa Elisafani, Shimri na Yeueli; kutoka kwa wana wa Asafu,+ Zekaria na Matania; 14  kutoka kwa wana wa Hemani,+ Yehieli na Shimei; kutoka kwa wana wa Yeduthuni,+ Shemaya na Uzieli. 15  Kisha wakawakusanya pamoja ndugu zao na kujitakasa, nao wakaja kama mfalme alivyoamuru kulingana na maneno ya Yehova, ili kuitakasa nyumba ya Yehova.+ 16  Ndipo makuhani wakaingia ndani ya nyumba ya Yehova ili kuitakasa, nao wakaondoa uchafu wote uliokuwa katika hekalu la Yehova na kuupeleka kwenye ua+ wa nyumba ya Yehova. Halafu Walawi wakauchukua na kuupeleka nje katika Bonde la Kidroni.+ 17  Kwa hiyo walianza kazi hiyo ya kutakasa katika siku ya kwanza ya mwezi wa kwanza, na katika siku ya nane ya mwezi huo wakafika katika ukumbi wa Yehova.+ Waliitakasa nyumba ya Yehova kwa siku nane, na katika siku ya 16 ya mwezi wa kwanza wakamaliza kazi hiyo. 18  Baada ya hayo wakaenda kwa Mfalme Hezekia na kumwambia: “Tumeitakasa nyumba yote ya Yehova, madhabahu ya dhabihu za kuteketezwa+ na vyombo vyake vyote,+ na meza ya mikate ya tabaka*+ na vyombo vyake vyote. 19  Na vyombo vyote ambavyo Mfalme Ahazi aliviondoa wakati wa utawala wake alipokosa kutenda kwa uaminifu,+ tumevitayarisha na kuvitakasa,+ navyo viko mbele ya madhabahu ya Yehova.” 20  Basi Mfalme Hezekia akaamka mapema na kuwakusanya pamoja wakuu wa jiji, nao wakapanda kwenda katika nyumba ya Yehova. 21  Wakaleta ng’ombe dume saba, kondoo dume saba, wanakondoo dume saba, na mbuzi dume saba watolewe kuwa dhabihu ya dhambi kwa ajili ya ufalme, kwa ajili ya mahali patakatifu, na kwa ajili ya watu wa Yuda.+ Basi akawaambia makuhani, wazao wa Haruni, wawatoe dhabihu kwenye madhabahu ya Yehova. 22  Kisha wakawachinja ng’ombe hao,+ na makuhani wakachukua damu yao na kuinyunyiza kwenye madhabahu;+ halafu wakawachinja wale kondoo dume na kunyunyiza damu yao kwenye madhabahu, kisha wakawachinja wanakondoo dume hao na kunyunyiza damu yao kwenye madhabahu. 23  Kisha wakawaleta wale mbuzi dume wa dhabihu ya dhambi mbele ya mfalme na kutaniko na kuweka mikono yao juu yao. 24  Makuhani wakawachinja na kutoa dhabihu ya dhambi kwenye madhabahu wakitumia damu yao, ili kufunika dhambi za Waisraeli wote, kwa sababu mfalme alisema kwamba dhabihu ya kuteketezwa na dhabihu ya dhambi ilipaswa kutolewa kwa ajili ya Waisraeli wote. 25  Wakati huo, aliwaweka Walawi katika nyumba ya Yehova wakiwa na matoazi, vinanda, na vinubi,+ kulingana na amri ya Daudi+ na ya Gadi+ mwonaji wa mfalme na ya nabii Nathani,+ kwa maana amri hiyo ilitoka kwa Yehova kupitia manabii wake. 26  Basi Walawi walikuwa wakisimama wakiwa na ala za Daudi, na makuhani wakiwa na tarumbeta.+ 27  Kisha Hezekia akaagiza dhabihu ya kuteketezwa itolewe kwenye madhabahu.+ Dhabihu ya kuteketezwa ilipoanza kutolewa, wimbo wa Yehova ulianza na pia milio ya tarumbeta, kwa kufuata mwongozo wa ala za Mfalme Daudi wa Israeli. 28  Na kutaniko lote likainama chini wimbo huo ulipokuwa ukiimbwa na tarumbeta kupigwa—yote hayo yaliendelea mpaka walipomaliza kutoa dhabihu ya kuteketezwa. 29  Na mara tu walipomaliza kutoa dhabihu hiyo, mfalme na wote waliokuwa pamoja naye wakainama chini na kusujudu. 30  Sasa Mfalme Hezekia na wakuu wakawaambia Walawi wamsifu Yehova kwa maneno ya Daudi+ na ya mwonaji Asafu.+ Kwa hiyo wakamsifu kwa shangwe nyingi, nao wakainama chini na kusujudu. 31  Kisha Hezekia akasema: “Sasa kwa kuwa mmetengwa kando* kwa ajili ya Yehova, njooni mlete dhabihu mbalimbali na dhabihu za shukrani katika nyumba ya Yehova.” Basi kutaniko likaanza kuleta dhabihu mbalimbali na dhabihu za shukrani, na kila mtu aliyekuwa na moyo wa kutoa kwa hiari alileta dhabihu za kuteketezwa.+ 32  Idadi ya dhabihu za kuteketezwa zilizoletwa na kutaniko ilikuwa ng’ombe 70, kondoo dume 100, wanakondoo dume 200—wote hao wakiwa dhabihu ya kuteketezwa kwa Yehova+ 33  na dhabihu takatifu zilikuwa ng’ombe 600 na kondoo 3,000. 34  Lakini hakukuwa na makuhani wa kutosha kuwachuna ngozi wanyama wote wa dhabihu za kuteketezwa, kwa hiyo ndugu zao Walawi waliwasaidia+ mpaka kazi hiyo ilipoisha na mpaka makuhani walipoweza kujitakasa,+ kwa kuwa Walawi walikuwa na bidii zaidi ya* kujitakasa kuliko makuhani. 35  Pia, kulikuwa na dhabihu nyingi za kuteketezwa,+ na vilevile vipande vya mafuta vya dhabihu za ushirika+ na matoleo ya vinywaji kwa ajili ya dhabihu za kuteketezwa.+ Hivyo utumishi wa nyumba ya Yehova ukaanzishwa tena.* 36  Kwa hiyo Hezekia na watu wote wakashangilia jambo ambalo Mungu wa kweli alikuwa amewafanyia watu,+ kwa sababu jambo hilo lilitendeka haraka sana.*

Maelezo ya Chini

Au “kudhihakiwa.”
Au “kupumzika.”
Yaani, mikate ya wonyesho.
Tnn., “Sasa mmeujaza mkono wenu.”
Tnn., “walikuwa na moyo mnyoofu katika.”
Au “ukatayarishwa.”
Au “ghafla.”