Kitabu cha Pili cha Mambo ya Nyakati 3:1-17

  • Sulemani aanza kujenga hekalu (1-7)

  • Patakatifu Zaidi (8-14)

  • Nguzo mbili za shaba (15-17)

3  Kisha Sulemani akaanza kujenga nyumba ya Yehova+ huko Yerusalemu juu ya Mlima Moria,+ mahali ambapo Yehova alikuwa amemtokea Daudi baba yake,+ mahali ambapo Daudi alikuwa ametayarisha kwenye uwanja wa kupuria wa Ornani Myebusi.+  Alianza kujenga siku ya pili ya mwezi wa pili, katika mwaka wa nne wa utawala wake.  Na msingi ambao Sulemani aliweka kwa ajili ya ujenzi wa nyumba ya Mungu wa kweli ulikuwa na urefu wa mikono 60 na upana wa mikono 20,+ kulingana na kipimo cha awali.*  Ukumbi wa mbele ulikuwa na urefu wa mikono 20, nao ulilingana na upana wa nyumba,* na kimo chake kilikuwa 120;* naye akafunika upande wa ndani kwa dhahabu safi.+  Alifunika nyumba kuu kwa mbao za miberoshi, kisha akaifunika kwa dhahabu bora,+ halafu akaipamba kwa michongo ya mitende+ na minyororo.+  Pia, aliifunika nyumba hiyo kwa mawe maridadi yenye thamani;+ na dhahabu+ aliyotumia ilikuwa dhahabu kutoka Parvaimu.  Aliifunika nyumba, maboriti, vizingiti, kuta zake, na milango yake kwa dhahabu;+ naye akachonga makerubi kwenye kuta zake.+  Kisha akajenga chumba cha Patakatifu Zaidi;*+ urefu wake ulilingana na upana wa nyumba, mikono 20, na upana wake ulikuwa mikono 20. Akaifunika kwa talanta 600* za dhahabu bora.+  Uzito wa dhahabu iliyotumiwa kutengenezea misumari ulikuwa shekeli 50;* naye alifunika vyumba vya darini kwa dhahabu. 10  Kisha akatengeneza mifano ya makerubi wawili katika chumba cha Patakatifu Zaidi,* akawafunika kwa dhahabu.+ 11  Kwa ujumla mabawa ya makerubi hao+ yalikuwa na urefu wa mikono 20; bawa moja la kerubi wa kwanza lilikuwa na urefu wa mikono mitano nalo liligusa ukuta wa nyumba, na bawa la pili lilikuwa na urefu wa mikono mitano nalo liligusa bawa moja la kerubi wa pili. 12  Na bawa moja la kerubi wa pili lilikuwa na urefu wa mikono mitano nalo liligusa ukuta wa nyumba, na bawa la pili lilikuwa na urefu wa mikono mitano nalo liligusa bawa moja la yule kerubi wa kwanza. 13  Mabawa ya makerubi hao yalikuwa yamenyooshwa kufikia urefu wa mikono 20; nao walikuwa wamesimama kwa miguu yao, nyuso zao zikielekea ndani.* 14  Alitengeneza pia pazia+ kwa nyuzi za bluu, sufu ya zambarau, kitambaa chekundu, na kitambaa bora, na kulitarizi kwa mifano ya makerubi.+ 15  Kisha akatengeneza nguzo mbili+ mbele ya nyumba hiyo, zenye urefu wa mikono 35, na kifuniko kilichokuwa juu ya kila nguzo kilikuwa na urefu wa mikono mitano.+ 16  Pia alitengeneza minyororo iliyokuwa kama mikufu, akaiweka juu ya nguzo hizo, kisha akatengeneza makomamanga 100 na kuyaweka kwenye minyororo hiyo. 17  Akasimamisha nguzo hizo mbele ya hekalu, moja upande wa kulia* na nyingine upande wa kushoto;* akaiita nguzo ya upande wa kulia Yakini* na nguzo ya upande wa kushoto Boazi.*

Maelezo ya Chini

Kipimo cha kawaida cha mkono mmoja kililingana na sentimita 44.5 (inchi 17.5), lakini baadhi ya watu wanahisi kwamba “kipimo cha awali” kinarejelea kipimo cha mkono mrefu ambacho kililingana na sentimita 51.8 (inchi 20.4). Angalia Nyongeza B14.
Kipimo kisichojulikana.
Au “mikono 20 kufikia upana wa nyumba.”
Talanta moja ilikuwa na uzito wa kilogramu 34.2. Angalia Nyongeza B14.
Tnn., “nyumba.”
Shekeli moja ilikuwa na uzito wa gramu 11.4. Angalia Nyongeza B14.
Tnn., “nyumba.”
Yaani, zikielekea Patakatifu.
Au “kusini.”
Au “kaskazini.”
Maana yake “Naye [yaani, Yehova] Aimarishe Kabisa.”
Labda inamaanisha “Katika Nguvu.”