Kitabu cha Pili cha Mambo ya Nyakati 30:1-27

  • Hezekia aadhimisha Pasaka (1-27)

30  Hezekia akatuma ujumbe kwa watu wote wa Israeli+ na Yuda, na hata aliwaandikia barua watu wa Efraimu na Manase+ waje Yerusalemu katika nyumba ya Yehova kuadhimisha Pasaka ya Yehova Mungu wa Israeli.+  Hata hivyo, mfalme, wakuu wake, na kutaniko lote Yerusalemu likaamua kuadhimisha Pasaka katika mwezi wa pili,+  kwa maana hawakuweza kuiadhimisha wakati ambapo iliadhimishwa kwa ukawaida,+ kwa sababu hakukuwa na makuhani wa kutosha waliojitakasa+ na watu hawakuwa wamekusanyika Yerusalemu.  Mpango huo ulionekana kuwa mzuri machoni pa mfalme na kutaniko lote.  Basi wakaamua kutangaza kotekote Israeli, kuanzia Beer-sheba mpaka Dani,+ kwamba watu waje Yerusalemu kuadhimisha Pasaka ya Yehova Mungu wa Israeli, kwa maana wakiwa kikundi hawakuwa wameiadhimisha kulingana na yaliyoandikwa.+  Kisha wajumbe* wakaenda kotekote Israeli na Yuda wakiwa na barua hizo kutoka kwa mfalme na wakuu wake, kama mfalme alivyoamuru, akisema: “Watu wa Israeli, rudini kwa Yehova Mungu wa Abrahamu, Isaka, na Israeli, ili naye arudi kwa watu waliobaki walioponyoka kutoka mikononi mwa wafalme wa Ashuru.+  Msiwe kama mababu zenu na kama ndugu zenu waliokosa kutenda kwa uaminifu kwa Yehova Mungu wa mababu zao, hivi kwamba akawafanya kuwa kitu cha kutisha, kama mnavyoona.+  Sasa msiwe wakaidi kama mababu zenu.+ Jinyenyekezeni kwa Yehova, nanyi mje mahali pake patakatifu+ ambapo amepatakasa milele, mumtumikie Yehova Mungu wenu, ili hasira yake inayowaka iwaondokee.+  Kwa maana mkirudi kwa Yehova, ndugu zenu na wana wenu wataonyeshwa rehema na wale waliowateka,+ nao wataruhusiwa kurudi katika nchi hii;+ kwa maana Yehova Mungu wenu ni mwenye huruma* na rehema,+ naye hataugeuza uso wake mbali nanyi mkirudi kwake.”+ 10  Kwa hiyo wajumbe* hao walienda jiji hadi jiji katika nchi yote ya Efraimu na Manase,+ walifika hata Zabuloni, lakini watu walikuwa wakiwafanyia mzaha na kuwadhihaki.+ 11  Hata hivyo, watu fulani kutoka Asheri, Manase, na Zabuloni walijinyenyekeza na kuja Yerusalemu.+ 12  Mkono wa Mungu wa kweli ulikuwa pia juu ya watu wa Yuda ili kuwaunganisha* watekeleze yale ambayo mfalme na wakuu walikuwa wameamuru kulingana na neno la Yehova. 13  Umati wa watu ulikusanyika Yerusalemu katika mwezi wa pili+ kuadhimisha Sherehe ya Mikate Isiyo na Chachu;+ lilikuwa kutaniko kubwa sana. 14  Basi wakaondoa madhabahu zilizokuwa Yerusalemu,+ wakaziondoa madhabahu zote za kufukizia uvumba+ na kuzitupa katika Bonde la Kidroni. 15  Kisha wakamchinja mnyama wa Pasaka katika siku ya 14 ya mwezi wa pili. Makuhani na Walawi wakaona aibu, kwa hiyo wakajitakasa na kuleta dhabihu za kuteketezwa katika nyumba ya Yehova. 16  Nao wakasimama katika nafasi zao za kawaida, kulingana na Sheria ya Musa, mtu wa Mungu wa kweli; kisha makuhani wakanyunyiza damu+ waliyokabidhiwa na Walawi. 17  Kulikuwa na watu wengi katika kutaniko hilo ambao hawakuwa wamejitakasa, na Walawi ndio waliowachinja wanyama wa dhabihu za Pasaka kwa ajili ya wote ambao hawakuwa safi,+ ili wawatakase kwa Yehova. 18  Kwa maana idadi kubwa ya watu, hasa wale waliotoka Efraimu, Manase,+ Isakari, na Zabuloni, hawakuwa wamejitakasa, lakini bado walikula Pasaka, kinyume cha mambo yaliyoandikwa. Lakini Hezekia alisali kwa ajili yao, akisema: “Yehova, wewe uliye mwema,+ msamehe 19  kila mtu ambaye ameutayarisha moyo wake ili kukutafuta wewe Mungu wa kweli,+ Yehova, Mungu wa mababu zake, ingawa hajatakaswa kulingana na kiwango cha utakatifu.”+ 20  Basi Yehova akamsikiliza Hezekia, akawasamehe* watu hao. 21  Kwa hiyo Waisraeli waliokuwa Yerusalemu wakaadhimisha Sherehe ya Mikate Isiyo na Chachu+ kwa siku saba, wakiwa na shangwe nyingi,+ na Walawi na makuhani walikuwa wakimsifu Yehova siku baada ya siku, wakimpigia Yehova ala zao kwa sauti kubwa.+ 22  Zaidi ya hayo, Hezekia alizungumza na Walawi wote waliokuwa wakimtumikia Yehova kwa busara, akawatia moyo.* Nao wakala katika kipindi chote cha sherehe hiyo ya siku saba,+ wakitoa dhabihu za ushirika+ na kumshukuru Yehova Mungu wa mababu zao. 23  Kisha kutaniko lote likaamua kuendelea na sherehe hiyo kwa siku saba zaidi, kwa hiyo waliifanya kwa siku saba zaidi huku wakishangilia.+ 24  Na Mfalme Hezekia wa Yuda alitoa mchango wa ng’ombe dume 1,000 na kondoo 7,000 kwa ajili ya kutaniko, na wakuu walitoa mchango wa ng’ombe dume 1,000 na kondoo 10,000 kwa ajili ya kutaniko;+ na makuhani wengi walikuwa wakijitakasa.+ 25  Na kutaniko lote la Yuda, makuhani, Walawi, kutaniko lote lililotoka Israeli,+ na wakaaji wageni+ waliotoka katika nchi ya Israeli na wale walioishi Yuda wakaendelea kushangilia. 26  Na kulikuwa na shangwe nyingi Yerusalemu, kwa maana tangu siku za Sulemani mwana wa Daudi mfalme wa Israeli, jambo kama hilo halikuwa limeonekana Yerusalemu.+ 27  Hatimaye makuhani Walawi wakasimama na kuwabariki watu;+ na Mungu akasikia sauti yao, na sala yao ikafika katika makao yake matakatifu, mbinguni.

Maelezo ya Chini

Tnn., “wakimbiaji.”
Au “neema.”
Tnn., “wakimbiaji.”
Tnn., “kuwapa moyo mmoja.”
Tnn., “akawaponya.”
Tnn., “akazungumza na moyo wao.”