Kitabu cha Pili cha Mambo ya Nyakati 31:1-21

  • Hezekia aung’oa uasi imani (1)

  • Makuhani na Walawi wategemezwa ifaavyo (2-21)

31  Mara tu walipomaliza kufanya mambo hayo yote, Waisraeli wote waliokuwepo wakaenda katika majiji ya Yuda, nao wakazivunjavunja nguzo takatifu,+ wakaikatakata miti mitakatifu,*+ na kubomoa mahali pa juu+ na madhabahu+ katika nchi yote ya Yuda na Benjamini, na pia kule Efraimu na Manase,+ mpaka walipoviharibu kabisa vitu hivyo, kisha Waisraeli wote wakarudi katika majiji yao, kila mmoja kwenye miliki yake.  Kisha Hezekia akawaweka makuhani katika vikundi vyao+ na Walawi katika vikundi vyao,+ kila kuhani na Mlawi katika utumishi wake,+ kwa ajili ya dhabihu za kuteketezwa na dhabihu za ushirika, ili wahudumu na kushukuru na kusifu katika malango ya nyua* za Yehova.+  Baadhi ya mali za mfalme mwenyewe zilitolewa kwa ajili ya dhabihu za kuteketezwa,+ kutia ndani dhabihu zilizotolewa asubuhi na jioni,+ na pia dhabihu za kuteketezwa kwa ajili ya Sabato,+ miezi mipya,+ na sherehe mbalimbali,+ kulingana na mambo yaliyoandikwa katika Sheria ya Yehova.  Isitoshe, aliwaamuru watu walioishi Yerusalemu watoe fungu ambalo makuhani na Walawi walistahili kupokea,+ ili waishike kabisa* sheria ya Yehova.  Mara tu agizo hilo lilipotolewa, Waisraeli walitoa kwa wingi mazao ya kwanza ya nafaka, divai mpya, mafuta,+ na asali, na mazao yote ya shambani;+ walileta kwa wingi sehemu ya kumi ya kila kitu.+  Na watu wa Israeli na wa Yuda waliokuwa wakiishi katika majiji ya Yuda walileta pia sehemu ya kumi ya ng’ombe na kondoo na sehemu ya kumi ya vitu vitakatifu+ vilivyotakaswa kwa ajili ya Yehova Mungu wao. Walivileta na kuvipanga katika marundo mengi.  Katika mwezi wa tatu,+ walianza kuvipanga katika marundo vitu walivyotoa michango; na katika mwezi wa saba+ wakamaliza.  Hezekia na wakuu walipokuja na kuona marundo hayo, walimsifu Yehova na kuwabariki watu wake Waisraeli.  Hezekia akawauliza makuhani na Walawi kuhusu marundo hayo, 10  ndipo Azaria mkuu wa makuhani wa nyumba ya Sadoki akamwambia: “Tangu watu walipoanza kuleta michango ndani ya nyumba ya Yehova,+ wamekuwa wakila na kushiba na bado kiasi kikubwa kimebaki, kwa maana Yehova amewabariki watu wake, na kiasi hiki kikubwa sana kimebaki.”+ 11  Ndipo Hezekia akawaambia watayarishe vyumba vya kuhifadhia vitu hivyo*+ katika nyumba ya Yehova, basi wakavitayarisha. 12  Waliendelea kuleta kwa uaminifu michango, sehemu za kumi,+ na vitu vitakatifu; na Mlawi aliyeitwa Konania aliwekwa kuwa msimamizi wa vitu hivyo vyote, na Shimei ndugu yake alikuwa wa pili. 13  Yehieli, Azazia, Nahathi, Asaheli, Yerimothi, Yozabadi, Elieli, Ismakia, Mahathi, na Benaya walikuwa maofisa waliomsaidia Konania na Shimei ndugu yake, kama Mfalme Hezekia alivyoagiza, na Azaria alikuwa msimamizi wa nyumba ya Mungu wa kweli. 14  Na Kore mwana wa Imna, Mlawi aliyekuwa mlinzi wa malango upande wa mashariki,+ alisimamia matoleo ya hiari+ ya Mungu wa kweli, naye aligawa mchango uliotolewa kwa Yehova+ na pia vitu vitakatifu kabisa.+ 15  Na Edeni, Miniamini, Yeshua, Shemaya, Amaria, na Shekania walikuwa chini ya usimamizi wake katika majiji ya makuhani,+ katika wadhifa wao wa kuaminiwa, ili wawagawie ndugu zao kwa usawa katika vikundi,+ wakubwa kwa wadogo. 16  Hilo halikutia ndani mchango waliogawiwa wanaume wenye umri wa miaka mitatu na zaidi walioandikishwa kwenye orodha ya koo, ambao walikuja kila siku kutumikia katika nyumba ya Yehova na kutimiza majukumu ya vikundi vyao. 17  Makuhani waliandikishwa katika orodha ya koo kulingana na ukoo wao,*+ kama walivyoandikishwa Walawi waliokuwa na umri wa miaka 20 na zaidi,+ kulingana na majukumu ya vikundi vyao.+ 18  Walioandikishwa katika orodha ya koo walitia ndani watoto wao wote, wake zao, wana wao, na mabinti wao, kutaniko lote—kwa maana walidumisha utakaso wao kwa ajili ya mambo matakatifu kwa sababu ya wadhifa wao wa kuaminiwa— 19  na pia wazao wa Haruni, makuhani walioishi katika mashamba yenye malisho ambayo yalizunguka majiji yao.+ Katika majiji yote, wanaume walikuwa wamechaguliwa na kutajwa majina ili wampe mafungu kila mwanamume kuhani na kila mtu aliyeandikishwa katika orodha ya koo za Walawi. 20  Hezekia alifanya hayo katika nchi yote ya Yuda, naye aliendelea kutenda mema na yaliyo sawa na ya uaminifu mbele za Yehova Mungu wake. 21  Na kila kazi aliyofanya ili kumtafuta Mungu wake, iwe ni kuhusiana na utumishi wa nyumba ya Mungu wa kweli+ au kuhusiana na Sheria na amri, aliifanya kwa moyo wote, naye alifanikiwa.

Maelezo ya Chini

Angalia Kamusi.
Tnn., “kambi.”
Au “wajitoe kikamili kwa.”
Au “vyumba vya kulia chakula.”
Yaani, ukoo wa upande wa baba.