Kitabu cha Pili cha Mambo ya Nyakati 32:1-33

  • Senakeribu alitisha jiji la Yerusalemu (1-8)

  • Senakeribu ampinga Yehova (9-19)

  • Malaika aangamiza jeshi la Ashuru (20-23)

  • Ugonjwa wa Hezekia na kiburi chake (24-26)

  • Mambo aliyotimiza Hezekia na kifo chake (27-33)

32  Baada ya mambo hayo na matendo hayo ya uaminifu,+ Mfalme Senakeribu wa Ashuru alikuja na kuvamia Yuda. Alizingira majiji yenye ngome, akikusudia kuvunja na kuingia ndani na kuyateka.+  Hezekia alipoona kwamba Senakeribu amekuja akikusudia kulishambulia jiji la Yerusalemu,  alishauriana na wakuu wake na mashujaa wake na kuamua kuziba chemchemi za maji zilizokuwa nje ya jiji,+ nao wakamsaidia.  Watu wengi walikusanywa, nao wakaziba chemchemi zote na kijito kilichopita nchini, wakisema: “Kwa nini wafalme wa Ashuru waje na kupata maji mengi?”  Zaidi ya hayo, akiwa ameazimia, alijenga upya ukuta wote uliobomolewa, akajenga minara juu yake, na kujenga ukuta mwingine upande wa nje. Alirekebisha pia Kilima*+ cha Jiji la Daudi na kutengeneza silaha nyingi na ngao.  Kisha akawachagua wakuu wa majeshi wawaongoze watu, akawakusanya kwenye uwanja wa jiji uliokuwa karibu na lango la jiji, akawatia moyo* akisema:  “Iweni jasiri na imara. Msiogope wala msihofu kwa sababu ya mfalme wa Ashuru+ na umati wote ulio pamoja naye, kwa maana walio pamoja nasi ni wengi kuliko wale walio pamoja naye.+  Yeye anategemea mkono wa nyama* lakini sisi tuna Yehova Mungu wetu wa kutusaidia na kupigana vita vyetu.”+ Basi watu wakaimarishwa na maneno ya Mfalme Hezekia wa Yuda.+  Baada ya hayo, Mfalme Senakeribu wa Ashuru alipokuwa Lakishi+ pamoja na fahari yake yote ya kifalme,* aliwatuma watumishi wake Yerusalemu, kwa Mfalme Hezekia wa Yuda na kwa Wayudea wote waliokuwa Yerusalemu,+ akisema: 10  “Mfalme Senakeribu wa Ashuru anasema hivi: ‘Ni nini mnachotumainia kinachowafanya mkae Yerusalemu wakati limezingirwa?+ 11  Je, Hezekia hawapotoshi ili mfe kwa njaa kali na kiu, anaposema: “Yehova Mungu wetu atatuokoa kutoka mikononi mwa mfalme wa Ashuru”?+ 12  Je, siye Hezekia huyuhuyu aliyeondoa mahali pa juu+ pa Mungu wenu na madhabahu Zake+ kisha akawaambia watu wa Yuda na Yerusalemu: “Mnapaswa kuinama mbele ya madhabahu moja na kufukiza moshi wa dhabihu zenu”?+ 13  Je, hamjui yale ambayo mimi na mababu zangu tuliyatendea mataifa yote ya nchi mbalimbali?+ Je, miungu ya mataifa ya nchi hizo iliweza kuwaokoa kutoka mikononi mwangu?+ 14  Ni mungu gani kati ya miungu yote ya mataifa hayo ambayo mababu zangu waliiangamiza aliyeweza kuwaokoa watu wake kutoka mikononi mwangu, hivi kwamba Mungu wenu aweze kuwaokoa ninyi kutoka mikononi mwangu?+ 15  Sasa msiache Hezekia awadanganye au kuwapotosha hivyo!+ Msimwamini, kwa maana hakuna mungu yeyote wa taifa lolote au ufalme aliyeweza kuwaokoa watu wake kutoka mikononi mwangu na kutoka mikononi mwa mababu zangu. Basi, Mungu wenu atawezaje kuwaokoa ninyi kutoka mikononi mwangu?’”+ 16  Watumishi wake wakasema mambo mengi zaidi mabaya dhidi ya Yehova Mungu wa kweli na dhidi ya Hezekia mtumishi wake. 17  Aliandika pia barua+ za kumtukana Yehova Mungu wa Israeli+ na kusema mambo mabaya dhidi yake, akisema: “Kama miungu ya mataifa ya nchi mbalimbali ilivyoshindwa kuwaokoa watu wake kutoka mikononi mwangu,+ vivyo hivyo Mungu wa Hezekia hatawaokoa watu wake kutoka mikononi mwangu.” 18  Waliendelea kuwaambia watu wa Yerusalemu waliokuwa ukutani mambo hayo kwa sauti kubwa kwa lugha ya Wayahudi, ili wawaogopeshe na kuwatia hofu, na ili waliteke jiji.+ 19  Walisema mambo mabaya dhidi ya Mungu wa Yerusalemu kama walivyosema dhidi ya miungu ya mataifa yaliyo duniani, ambayo ni kazi ya mikono ya mwanadamu. 20  Lakini Mfalme Hezekia na nabii Isaya+ mwana wa Amozi waliendelea kusali kuhusu jambo hilo na kuzililia mbingu ili wapate msaada.+ 21  Ndipo Yehova akamtuma malaika, na malaika huyo akamwangamiza kabisa kila shujaa hodari,+ kiongozi, na mkuu katika kambi ya mfalme wa Ashuru, hivi kwamba akarudi katika nchi yake akiwa ameaibika. Baadaye aliingia katika nyumba ya* mungu wake, na humo baadhi ya wanawe mwenyewe wakamuua kwa upanga.+ 22  Basi Yehova akamwokoa Hezekia na wakaaji wa Yerusalemu kutoka mikononi mwa Mfalme Senakeribu wa Ashuru na kutoka mikononi mwa wengine wote na kuwapumzisha pande zote. 23  Na watu wengi wakamletea Yehova zawadi huko Yerusalemu na kumletea Mfalme Hezekia wa Yuda vitu bora,+ naye akaheshimiwa sana na mataifa yote baada ya mambo hayo. 24  Siku hizo Hezekia akawa mgonjwa karibu afe, akasali kwa Yehova,+ naye akamjibu na kumpa ishara.*+ 25  Lakini Hezekia hakuonyesha uthamini kwa wema wote aliotendewa, kwa maana moyo wake uliingiwa na kiburi, jambo lililomfanya yeye pamoja na watu wa Yuda na wa Yerusalemu wapatwe na ghadhabu. 26  Hata hivyo, Hezekia alijinyenyekeza, moyo wake ukaacha kuwa na kiburi,+ yeye pamoja na wakaaji wa Yerusalemu, na ghadhabu ya Yehova haikuja dhidi yao katika siku za Hezekia.+ 27  Hezekia akapata utajiri mwingi sana na utukufu;+ akajijengea maghala+ ya kuweka fedha, dhahabu, mawe yenye thamani, mafuta ya zeri, ngao, na vitu vyote vyenye kutamanika. 28  Alijenga pia maghala ya mazao ya nafaka na divai mpya na mafuta, na pia mabanda kwa ajili ya mifugo ya kila aina na mabanda kwa ajili ya kondoo na mbuzi. 29  Pia alijijengea majiji, akapata mifugo mingi sana, makundi ya kondoo, mbuzi, na ng’ombe, kwa maana Mungu alimpa mali nyingi sana. 30  Hezekia ndiye aliyeziba chemchemi ya juu ya maji+ ya Gihoni+ na kuyaelekeza moja kwa moja chini upande wa magharibi katika Jiji la Daudi,+ na Hezekia alifanikiwa katika kila kazi aliyofanya. 31  Hata hivyo, wasemaji wa wakuu wa Babiloni walipotumwa wamuulize kuhusu ishara+ iliyokuwa imetokea* nchini,+ Mungu wa kweli alimwacha ili kumjaribu,+ ili ajue mambo yote yaliyokuwa moyoni mwake.+ 32  Na mambo mengine katika historia ya Hezekia na matendo yake ya upendo mshikamanifu,+ yameandikwa katika maono ya nabii Isaya,+ mwana wa Amozi, katika Kitabu cha Wafalme wa Yuda na wa Israeli.+ 33  Kisha Hezekia akafa na kuzikwa pamoja na mababu zake kwenye njia inayopanda kuelekea kwenye makaburi ya wana wa Daudi;+ na watu wote wa Yuda na wakaaji wa Yerusalemu wakamheshimu alipokufa. Na Manase mwanawe akawa mfalme baada yake.

Maelezo ya Chini

Au “Milo.” Neno la Kiebrania linalomaanisha “jaza.”
Tnn., “akazungumza na moyo wao.”
Au “nguvu za mwanadamu.”
Au “uwezo wake wote wa kijeshi na fahari.”
Au “hekalu la.”
Au “kumfanyia muujiza.”
Au “muujiza uliokuwa umetokea.”