Kitabu cha Pili cha Mambo ya Nyakati 34:1-33

  • Yosia, mfalme wa Yuda (1, 2)

  • Mabadiliko yaliyofanywa na Yosia (3-13)

  • Kitabu cha Sheria chapatikana (14-21)

  • Unabii wa Hulda kuhusu msiba (22-28)

  • Yosia awasomea watu kitabu kilichopatikana (29-33)

34  Yosia+ alikuwa na umri wa miaka minane alipoanza kutawala, naye alitawala kwa miaka 31 huko Yerusalemu.+  Alitenda yaliyokuwa sawa machoni pa Yehova na kutembea katika njia za Daudi babu yake, naye hakugeuka na kwenda kulia au kushoto.  Katika mwaka wa 8 wa utawala wake, alipokuwa angali mvulana, alianza kumtafuta Mungu wa Daudi babu yake;+ na katika mwaka wa 12, akaanza kusafisha Yuda na Yerusalemu+ kwa kuondoa mahali pa juu+ na miti mitakatifu,* sanamu za kuchongwa,+ na sanamu za chuma.*  Pia, walibomoa madhabahu za Mabaali mbele yake, naye akavikatakata vinara vya uvumba vilivyokuwa juu ya madhabahu hizo. Pia alivunja vipandevipande miti mitakatifu,* sanamu za kuchongwa, na sanamu za chuma,* akazipondaponda zikawa ungaunga na kuunyunyiza juu ya makaburi ya wale waliokuwa wakizitolea dhabihu.+  Akaiteketeza mifupa ya makuhani juu ya madhabahu zao.+ Basi akaisafisha nchi ya Yuda na Yerusalemu.  Na katika majiji ya Manase, Efraimu,+ Simeoni, na mpaka Naftali, katika magofu yaliyozunguka majiji hayo,  alibomoa madhabahu na kupondaponda miti mitakatifu* na sanamu za kuchongwa,+ zikabaki ungaunga; naye akavikatakata vinara vyote vya uvumba katika nchi yote ya Israeli,+ kisha akarudi Yerusalemu.  Katika mwaka wa 18 wa utawala wake, alipokuwa ameisafisha nchi na hekalu,* alimtuma Shafani+ mwana wa Azalia, Maaseya mkuu wa jiji, na Yoa mwana wa Yoahazi aliyefanya kazi ya kuweka kumbukumbu ili wairekebishe nyumba ya Yehova Mungu wake.+  Walienda kwa kuhani mkuu Hilkia na kumpa pesa zilizokuwa zimeletwa katika nyumba ya Mungu, ambazo Walawi waliokuwa walinzi wa malango walikuwa wamekusanya kutoka kwa watu wa kabila la Manase, Efraimu, na Waisraeli wengine wote,+ na pia kutoka kwa watu wa Yuda, Benjamini, na wakaaji wa Yerusalemu. 10  Kisha wakawapa pesa hizo wale waliowekwa kusimamia kazi katika nyumba ya Yehova. Halafu wafanyakazi waliokuwa katika nyumba ya Yehova wakazitumia kuikarabati na kuirekebisha nyumba hiyo. 11  Waliwapa mafundi na wajenzi ili wanunue mawe yaliyochongwa na mbao za kuunganisha na za kutengeneza maboriti ya kujenga nyumba ambazo wafalme wa Yuda waliacha ziharibike.+ 12  Wanaume hao walifanya kazi hiyo kwa uaminifu.+ Walawi waliowekwa wawasimamie ni Yahathi na Obadia kutoka kwa Wamerari,+ na Zekaria na Meshulamu kutoka kwa Wakohathi,+ ili watumikie wakiwa waangalizi. Na Walawi fulani, ambao wote walikuwa wanamuziki stadi,+ 13  waliwasimamia vibarua* na walikuwa waangalizi wa watu wote waliokuwa wakifanya kazi katika utumishi wa aina mbalimbali; na baadhi ya Walawi walikuwa waandishi, maofisa, na walinzi wa malango.+ 14  Walipokuwa wakitoa pesa zilizokuwa zimeletwa katika nyumba ya Yehova,+ kuhani Hilkia alipata kitabu cha Sheria ya Yehova+ kilichotolewa kupitia* Musa.+ 15  Kwa hiyo Hilkia akamwambia mwandishi Shafani: “Nimepata kitabu cha Sheria katika nyumba ya Yehova.” Basi Hilkia akampa Shafani kitabu hicho. 16  Kisha Shafani akampelekea mfalme kitabu hicho na kumwambia: “Watumishi wako wanafanya kila jambo ulilowaambia wafanye. 17  Wamekusanya* pesa zilizopatikana katika nyumba ya Yehova, nao wamewapa wanaume waliowekwa kusimamia kazi na wale wanaofanya kazi.” 18  Pia, mwandishi Shafani akamwambia mfalme: “Kuna kitabu ambacho kuhani Hilkia amenipa.”+ Kisha Shafani akaanza kukisoma mbele ya mfalme.+ 19  Mara tu mfalme aliposikia maneno ya kitabu hicho cha Sheria, akayararua mavazi yake.+ 20  Kisha mfalme akamwagiza hivi Hilkia, Ahikamu+ mwana wa Shafani, Abdoni mwana wa Mika, mwandishi Shafani, na Asaya mtumishi wa mfalme: 21  “Nendeni mkatafute ushauri wa Yehova kwa niaba yangu na kwa niaba ya watu ambao wamebaki Israeli na Yuda kuhusu maneno ya kitabu hiki ambacho kimepatikana; kwa maana ghadhabu ya Yehova itakayomwagwa dhidi yetu ni kali kwa sababu mababu zetu hawakutekeleza neno la Yehova kwa kuyashika mambo yote yaliyoandikwa katika kitabu hiki.”+ 22  Basi Hilkia, pamoja na wale waliotumwa na mfalme, wakaenda kwa nabii wa kike aliyeitwa Hulda.+ Alikuwa mke wa Shalumu mwana wa Tikva mwana wa Harhasi, mtunzaji wa chumba cha mavazi, naye alikuwa akiishi katika Wilaya ya Pili ya Yerusalemu; wakazungumza naye huko.+ 23  Akawaambia: “Yehova Mungu wa Israeli anasema hivi: ‘Mwambieni hivi mtu aliyewatuma kwangu: 24  “Yehova anasema, ‘Nitaleta msiba mahali hapa na kwa wakaaji wake,+ laana zote zilizoandikwa katika kitabu+ walichosoma mbele ya mfalme wa Yuda. 25  Kwa sababu wameniacha+ na wanaifukizia miungu mingine moshi wa dhabihu ili kunikasirisha+ kwa kazi zote za mikono yao, ghadhabu yangu itamwagika mahali hapa nayo haitazimwa.’”+ 26  Lakini mwambieni hivi mfalme wa Yuda aliyewatuma kutafuta ushauri wa Yehova: “Yehova Mungu wa Israeli anasema hivi: ‘Kuhusu maneno ambayo umesikia,+ 27  kwa sababu moyo wako ulikuwa msikivu,* nawe ukajinyenyekeza mbele za Mungu uliposikia mambo yake kuhusu mahali hapa na wakaaji wake, ukajinyenyekeza mbele zangu na kuyararua mavazi yako na kulia mbele zangu, mimi pia nimekusikia,+ asema Yehova. 28  Ndiyo sababu nitakuzika pamoja na mababu zako,* nawe utalazwa kwa amani katika kaburi lako, na macho yako hayataona msiba wote nitakaoleta mahali hapa na kwa wakaaji wake.’”’”+ Kisha wakampelekea mfalme jibu hilo. 29  Basi mfalme akatuma ujumbe na kuwakusanya wazee wote wa Yuda na Yerusalemu.+ 30  Baada ya hayo mfalme akapanda kwenda katika nyumba ya Yehova pamoja na wanaume wote wa Yuda, wakaaji wa Yerusalemu, makuhani, Walawi—watu wote, wadogo kwa wakubwa. Akasoma, watu wote wakisikia, maneno yote ya kitabu cha agano kilichokuwa kimepatikana katika nyumba ya Yehova.+ 31  Mfalme akasimama mahali pake na kufanya agano*+ mbele za Yehova, kwamba atamfuata Yehova na kushika amri zake, vikumbusho vyake, na masharti yake kwa moyo wake wote na kwa nafsi* yake yote+ kwa kutekeleza maneno ya agano hilo yaliyoandikwa katika kitabu hicho.+ 32  Zaidi ya hayo, aliwahimiza watu wote waliokuwa Yerusalemu na Benjamini wakubali agano hilo. Na wakaaji wa Yerusalemu wakatenda kulingana na agano la Mungu, Mungu wa mababu zao.+ 33  Kisha Yosia akaondoa vitu vyote vyenye kuchukiza* katika nchi zote za Waisraeli,+ naye akawafanya watu wote wa Israeli wamtumikie Yehova Mungu wao. Katika maisha yake yote* hawakuacha kumfuata Yehova Mungu wa mababu zao.

Maelezo ya Chini

Angalia Kamusi.
Au “sanamu za kuyeyushwa.”
Angalia Kamusi.
Au “sanamu za kuyeyushwa.”
Angalia Kamusi.
Tnn., “nyumba.”
Au “waliobeba mizigo.”
Tnn., “kwa mkono wa.”
Tnn., “Wamemimina.”
Tnn., “laini.”
Tnn., “nitakukusanya kwa mababu zako.” Huu ni msemo wa kishairi unaorejelea kifo.
Au “kufanya upya lile agano.”
Angalia Kamusi.
Au “akaondoa miungu yote.”
Tnn., “Siku zake zote.”