Kitabu cha Pili cha Mambo ya Nyakati 5:1-14

  • Matayarisho ya kuzindua hekalu (1-14)

    • Sanduku la agano laletwa hekaluni (2-10)

5  Kwa hiyo Sulemani akakamilisha kazi yote aliyopaswa kufanya kwa ajili ya nyumba ya Yehova.+ Kisha Sulemani akaingiza ndani vitu ambavyo Daudi baba yake alikuwa amevifanya kuwa vitakatifu,+ naye akaweka fedha, dhahabu, na vitu vyote katika hazina za nyumba ya Mungu wa kweli.+  Wakati huo Sulemani aliwakusanya wazee wa Israeli, viongozi wote wa makabila, wakuu wa koo* za Israeli. Wakaja Yerusalemu ili kuliondoa sanduku la agano la Yehova katika Jiji la Daudi,+ yaani, Sayuni.+  Wanaume wote wa Israeli walikusanyika mbele ya mfalme wakati wa sherehe* inayofanywa katika mwezi wa saba.+  Basi wazee wote wa Israeli wakaja, na Walawi wakalibeba Sanduku.+  Wakalipandisha Sanduku, hema la mkutano,+ na vyombo vyote vitakatifu vilivyokuwa katika hema hilo. Makuhani na Walawi* wakavipandisha vitu hivyo.  Mfalme Sulemani na Waisraeli wote waliokusanywa ili wakutane naye walikuwa mbele ya Sanduku. Kondoo na ng’ombe wengi sana wasiohesabika au kujulikana idadi walikuwa wakitolewa dhabihu.+  Kisha makuhani wakalileta sanduku la agano la Yehova mahali pake, katika chumba cha ndani zaidi cha nyumba, yaani, Patakatifu Zaidi, chini ya mabawa ya makerubi.+  Kwa hiyo mabawa ya makerubi yalikuwa yamenyooshwa juu ya mahali ambapo Sanduku liliwekwa, hivi kwamba makerubi hao walilifunika Sanduku na fito zake.+  Fito hizo zilikuwa ndefu sana hivi kwamba ncha zake zilionekana kutoka Patakatifu mbele ya chumba cha ndani zaidi, lakini hazikuonekana kutoka upande wa nje. Nazo ziko huko mpaka leo hii. 10  Hakukuwa na kitu kingine ndani ya Sanduku hilo isipokuwa yale mabamba mawili ambayo Musa aliyaweka humo kule Horebu,+ Yehova alipofanya agano+ na Waisraeli walipokuwa wakitoka Misri.+ 11  Makuhani walipotoka mahali patakatifu (kwa maana makuhani wote waliokuwepo walikuwa wamejitakasa,+ bila kuzingatia vikundi vyao),+ 12  waimbaji wote Walawi+ walioongozwa na Asafu,+ Hemani,+ Yeduthuni,+ wana wao na ndugu zao walikuwa wamevaa mavazi ya kitambaa bora, wakiwa wamebeba matoazi, vinanda, na vinubi; walikuwa wamesimama upande wa mashariki wa madhabahu, na makuhani 120 waliokuwa wakipiga tarumbeta walikuwa pamoja nao.+ 13  Mara tu wapiga tarumbeta na waimbaji walipoanza kumsifu na kumshukuru Yehova kwa pamoja, na milio ya tarumbeta, matoazi, na ala nyingine za muziki zilipoanza kusikika walipokuwa wakimsifu Yehova, “kwa maana yeye ni mwema; upendo wake mshikamanifu unadumu milele,”+ ndipo nyumba hiyo, nyumba ya Yehova, ikajaa wingu.+ 14  Makuhani hawakuweza kusimama ili kuhudumu kwa sababu ya wingu hilo, kwa maana utukufu wa Yehova ulijaa katika nyumba ya Mungu wa kweli.+

Maelezo ya Chini

Yaani, ukoo wa upande wa baba.
Yaani, Sherehe ya Vibanda.
Au “makuhani Walawi.”