Kitabu cha Pili cha Mambo ya Nyakati 7:1-22

  • Hekalu lajaa utukufu wa Yehova (1-3)

  • Sherehe za kuzindua hekalu (4-10)

  • Yehova amtokea Sulemani (11-22)

7  Basi, mara tu Sulemani alipomaliza kusali,+ moto ulishuka kutoka mbinguni+ ukateketeza ile dhabihu ya kuteketezwa na dhabihu nyinginezo, na utukufu wa Yehova ukajaa katika nyumba hiyo.+  Makuhani hawakuweza kuingia ndani ya nyumba ya Yehova kwa sababu utukufu wa Yehova ulikuwa umejaa katika nyumba ya Yehova.+  Waisraeli wote walikuwa wakitazama moto uliposhuka na utukufu wa Yehova ulipokuwa juu ya nyumba hiyo, nao wakainama kifudifudi kwenye sakafu ya mawe, wakasujudu na kumshukuru Yehova, “kwa maana yeye ni mwema; upendo wake mshikamanifu unadumu milele.”  Sasa mfalme na watu wote wakazitoa dhabihu mbele za Yehova.+  Mfalme Sulemani alitoa ng’ombe 22,000 na kondoo 120,000 kuwa dhabihu. Basi mfalme na watu wote wakaizindua nyumba ya Mungu wa kweli.+  Makuhani walikuwa wamesimama katika vituo vyao vya kazi, na Walawi pia waliokuwa na ala za muziki zilizopigwa kuambatana na nyimbo ambazo Yehova aliimbiwa.+ (Mfalme Daudi alikuwa ametengeneza ala hizo ili kumshukuru Yehova—“kwa maana upendo wake mshikamanifu unadumu milele”—wakati Daudi alipokuwa akitoa sifa pamoja nao.*) Na makuhani walikuwa wakipiga tarumbeta kwa sauti kubwa+ mbele yao, huku Waisraeli wote wakiwa wamesimama.  Kisha Sulemani akatakasa sehemu ya katikati ya ua uliokuwa mbele ya nyumba ya Yehova, kwa maana alipaswa kutolea mahali hapo dhabihu za kuteketezwa+ na vipande vya mafuta vya dhabihu za ushirika, kwa sababu madhabahu ya shaba+ ambayo Sulemani alikuwa amejenga haingeweza kutoshea dhabihu za kuteketezwa, matoleo ya nafaka,+ na vipande vya mafuta.+  Wakati huo Sulemani alifanya sherehe hiyo kwa siku saba+ pamoja na Waisraeli wote, kutaniko kubwa sana kuanzia Lebo-hamathi* kushuka mpaka kwenye Korongo* la Misri.+  Lakini siku ya nane* walifanya kusanyiko takatifu,+ kwa sababu walikuwa wameizindua madhabahu kwa siku saba na kufanya sherehe hiyo kwa siku saba. 10  Kisha siku ya 23 ya mwezi wa saba, aliwaruhusu watu waende nyumbani kwao wakishangilia+ na kufurahi moyoni kwa sababu ya wema ambao Yehova alikuwa amemtendea Daudi na Sulemani na watu wake Waisraeli.+ 11  Kwa hiyo Sulemani akaikamilisha nyumba ya Yehova na nyumba ya* mfalme;+ na kila kitu ambacho Sulemani alitamani moyoni mwake kufanya kuhusiana na nyumba ya Yehova na nyumba yake mwenyewe, alifanikiwa kukitimiza.+ 12  Kisha Yehova akamtokea Sulemani+ usiku na kumwambia: “Nimesikia sala yako, nami nimechagua mahali hapa kwa ajili yangu ili pawe nyumba ya dhabihu.+ 13  Nikifunga mbingu ili mvua isinyeshe, nami nikiamuru panzi waile nchi, nami nikileta ugonjwa hatari miongoni mwa watu wangu, 14  na watu wangu ambao wameitwa kwa jina langu+ wakijinyenyekeza+ na kusali na kuutafuta uso wangu na kuacha njia zao ovu,+ ndipo nitakaposikia kutoka mbinguni na kuwasamehe dhambi yao na kuiponya nchi yao.+ 15  Sasa macho yangu yatatazama na masikio yangu yatasikiliza kwa makini sala zinazotolewa mahali hapa.+ 16  Na sasa nimeichagua nyumba hii na kuitakasa ili jina langu likae humu milele,+ na macho yangu na moyo wangu utakuwa humu sikuzote.+ 17  “Nawe, ukitembea mbele zangu kama Daudi baba yako alivyotembea, kwa kutenda mambo yote niliyokuamuru, nawe ukitii masharti yangu na sheria* zangu,+ 18  ndipo nitakapoimarisha kiti cha ufalme wako,+ kama nilivyofanya agano pamoja na Daudi baba yako,+ niliposema, ‘Hutakosa kamwe mwanamume wa uzao wako atakayetawala Israeli.’+ 19  Lakini ikiwa utageuka na kuacha maagizo yangu na amri zangu ambazo nimeweka mbele yako, nawe uende na kuabudu miungu mingine na kuiinamia,+ 20  nitawang’oa Waisraeli kutoka katika nchi ambayo nimewapa,+ na nyumba hii ambayo nimeitakasa kwa ajili ya jina langu nitaitupilia mbali kutoka mbele za macho yangu, nami nitaifanya iwe kitu cha kudharauliwa* na kitu cha kudhihakiwa miongoni mwa mataifa yote.+ 21  Na nyumba hii itakuwa marundo ya magofu. Kila mtu atakayepita karibu nayo ataitazama kwa mshangao+ na kuuliza, ‘Kwa nini Yehova aliitendea hivi nchi hii na nyumba hii?’+ 22  Kisha watasema, ‘Ni kwa sababu walimwacha Yehova+ Mungu wa mababu zao, aliyewatoa nchini Misri,+ nao wakashikamana na miungu mingine, wakaiinamia na kuiabudu.+ Ndiyo sababu aliwaletea msiba huo wote.’”+

Maelezo ya Chini

Huenda ni Walawi.
Au “njia ya kuingia Hamathi.”
Angalia Kamusi.
Siku ya kwanza baada ya sherehe hiyo, au siku ya 15.
Au “jumba la.”
Tnn., “hukumu.”
Tnn., “methali.”