Kitabu cha Pili cha Mambo ya Nyakati 8:1-18

  • Miradi mingine ya ujenzi ya Sulemani (1-11)

  • Ibada ya hekaluni yapangwa (12-16)

  • Meli za Sulemani (17, 18)

8  Katika muda wa miaka 20 ambayo Sulemani alijenga nyumba ya Yehova na nyumba yake* mwenyewe,+  Sulemani alijenga upya majiji ambayo Hiramu+ alikuwa amempa, akawapa Waisraeli* waishi humo.  Isitoshe, Sulemani alienda Hamath-soba na kuliteka jiji hilo.  Kisha akajenga tena jiji la Tadmori kule nyikani na majiji yote yenye maghala+ aliyokuwa amejenga Hamathi.+  Alijenga pia Beth-horoni ya Juu+ na Beth-horoni ya Chini,+ majiji yenye ngome yaliyokuwa na kuta, malango, na makomeo,  na Baalathi+ na pia majiji yote ya Sulemani yenye maghala, majiji yote ya magari ya vita,+ majiji ya wapanda farasi, na chochote ambacho Sulemani alitamani kujenga huko Yerusalemu, Lebanoni, na katika nchi yote iliyokuwa chini ya mamlaka yake.  Na watu wote waliobaki, yaani, Wahiti, Waamori, Waperizi, Wahivi, na Wayebusi+ ambao hawakuwa sehemu ya Waisraeli,+  wazao wao waliobaki nchini—wale ambao Waisraeli hawakuwaangamiza+—Sulemani aliwaandikisha ili wafanye kazi ya kulazimishwa mpaka leo hii.+  Lakini Sulemani hakumfanya Mwisraeli yeyote kuwa mtumwa wake,+ kwa sababu walikuwa mashujaa wake, wakuu wa makamanda wake wasaidizi, na wakuu wa waendeshaji wa magari yake ya vita na wapanda farasi wake.+ 10  Kulikuwa na wakuu 250 wa wasaidizi wa Mfalme Sulemani, waliokuwa wasimamizi wa watu.+ 11  Pia, Sulemani alimtoa binti ya Farao+ kutoka katika Jiji la Daudi na kumpeleka katika nyumba aliyokuwa amemjengea,+ kwa maana alisema: “Ingawa ni mke wangu, hapaswi kukaa katika nyumba ya Mfalme Daudi wa Israeli, kwa sababu sehemu ambazo Sanduku la Yehova limeletwa ni takatifu.”+ 12  Kisha Sulemani akamtolea Yehova dhabihu za kuteketezwa+ kwenye madhabahu+ ya Yehova aliyokuwa amejenga mbele ya ukumbi.+ 13  Alifuata utaratibu wa kila siku kwa kutoa dhabihu kulingana na amri ya Musa iliyohusu Sabato,+ miezi mipya,+ na sherehe zilizoamriwa mara tatu kwa mwaka+—Sherehe ya Mikate Isiyo na Chachu,+ Sherehe ya Majuma,+ na Sherehe ya Vibanda.*+ 14  Pia, alipanga vikundi vya makuhani+ kwa ajili ya utumishi wao kulingana na sheria ya Daudi baba yake, na Walawi katika vituo vyao vya kazi, ili watoe sifa+ na kuhudumu mbele ya makuhani kulingana na utaratibu wa kila siku, na walinzi wa malango katika vikundi vyao kwenye malango mbalimbali,+ kwa maana hivyo ndivyo alivyoamuru Daudi, mtu wa Mungu wa kweli. 15  Nao hawakuacha amri ambayo mfalme aliwapa makuhani na Walawi kuhusiana na jambo lolote au kuhusiana na maghala. 16  Basi kazi yote ya Sulemani ilipangwa vizuri sana,* kuanzia siku ambayo msingi wa nyumba ya Yehova uliwekwa+ mpaka ilipomalizwa. Basi nyumba ya Yehova ikakamilishwa.+ 17  Huo ndio wakati ambapo Sulemani alienda Esion-geberi+ na Elothi+ kwenye ufuo wa bahari katika nchi ya Edomu.+ 18  Hiramu+ aliwatuma watumishi wake mwenyewe wampelekee meli na mabaharia wenye uzoefu. Wakaenda Ofiri+ pamoja na watumishi wa Sulemani, wakachukua huko talanta 450* za dhahabu+ na kumletea Mfalme Sulemani.+

Maelezo ya Chini

Au “jumba lake.”
Tnn., “wana wa Israeli.”
Au “Vibanda vya Muda.”
Au “ilikuwa na mpangilio mzuri; ilikamilishwa.”
Talanta moja ilikuwa na uzito wa kilogramu 34.2. Angalia Nyongeza B14.