Kitabu cha Pili cha Samweli 1:1-27

  • Daudi apata habari za kifo cha Sauli (1-16)

  • Daudi aimba wimbo wa kumwombolezea Sauli na Yonathani (17-27)

1  Baada ya kifo cha Sauli, Daudi aliporudi baada ya kuwashinda* Waamaleki, alikaa Siklagi+ kwa siku mbili.  Siku ya tatu, mtu fulani alikuja kutoka katika kambi ya Sauli akiwa amevaa nguo zilizoraruka, na akiwa na mavumbi kichwani. Alipomkaribia Daudi, alijiangusha chini na kumwinamia.  Daudi akamuuliza: “Umetoka wapi?” Akajibu: “Nimetoroka katika kambi ya Israeli.”  Daudi akamuuliza: “Ni nini kilichotokea? Tafadhali niambie.” Akamwambia: “Watu wamekimbia kutoka vitani na wengi wameanguka na kufa. Hata Sauli na Yonathani mwanawe wamekufa.”+  Kisha Daudi akamuuliza hivi kijana huyo aliyemletea habari: “Unajuaje kwamba Sauli na Yonathani mwanawe wamekufa?”  Kijana huyo akajibu: “Nilifika kwenye Mlima Gilboa+ bila kutazamia, nikamwona Sauli akiwa ameegemea mkuki wake, na magari ya vita na wapanda farasi walikuwa wamemfikia.+  Alipogeuka na kuniona, aliniita, nami nikasema, ‘Naam!’  Akaniuliza, ‘Wewe ni nani?’ nikajibu, ‘Mimi ni Mwamaleki.’+  Kisha akasema, ‘Tafadhali, nikaribie uniue, kwa maana nina maumivu makali sana, lakini bado niko hai.’ 10  Basi nikamkaribia na kumuua,+ kwa maana nilijua kwamba hangeendelea kuishi baada ya kuanguka chini akiwa amejeruhiwa. Kisha nikachukua taji lililokuwa kichwani mwake na kikuku kilichokuwa mkononi mwake, nami nimevileta hapa kwako bwana wangu.” 11  Ndipo Daudi akashika mavazi yake na kuyararua, na watu wote waliokuwa pamoja naye wakafanya vivyo hivyo. 12  Nao wakaomboleza na kulia na kufunga+ mpaka jioni kwa ajili ya Sauli, kwa ajili ya Yonathani mwanawe, kwa ajili ya watu wa Yehova, kwa ajili ya nyumba ya Israeli,+ kwa sababu walikuwa wameuawa kwa upanga. 13  Daudi akamuuliza hivi kijana aliyemletea habari: “Unatoka wapi?” Akajibu: “Mimi ni mwana wa mkaaji mgeni, Mwamaleki.” 14  Kisha Daudi akamuuliza: “Kwa nini hukuogopa kuinua mkono wako kumuua mtiwa-mafuta wa Yehova?”+ 15  Ndipo Daudi akamwita kijana mmoja na kumwambia: “Njoo umuue.” Basi akampiga na kumuua.+ 16  Daudi akamwambia: “Damu yako na iwe juu ya kichwa chako mwenyewe, kwa sababu kinywa chako mwenyewe kilitoa ushahidi dhidi yako, uliposema, ‘Mimi mwenyewe nilimuua mtiwa-mafuta wa Yehova.’”+ 17  Kisha Daudi akaimba wimbo huu wa maombolezo kwa ajili ya Sauli na Yonathani mwanawe+ 18  na kusema kwamba watu wa Yuda wafundishwe wimbo wa maombolezo unaoitwa “Upinde,” ulioandikwa katika kitabu cha Yashari:+ 19  “Ee Israeli, uzuri umeuawa kwenye vilima vyako.+ Jinsi walivyoanguka wanaume wenye nguvu! 20  Msiseme jambo hilo kule Gathi;+Msilitangaze katika barabara za Ashkeloni,Mabinti wa Wafilisti wasije wakashangilia,Mabinti wa watu wasiotahiriwa wasije wakafurahi. 21  Enyi milima ya Gilboa,+Msipate umande wowote wala mvua yoyote,Wala mashamba yanayozaa michango mitakatifu,+Kwa sababu ngao ya wenye nguvu ilichafuliwa huko,Sasa ngao ya Sauli haijatiwa mafuta. 22  Kutoka kwenye damu ya waliouawa, kutoka kwenye mafuta ya wenye nguvu,Upinde wa Yonathani haukurudi nyuma,+Na upanga wa Sauli haukurudi bila mafanikio.+ 23  Sauli na Yonathani,+ watu waliopendwa na kuthaminiwa* walipokuwa hai,Na katika kifo hawakutenganishwa.+ Walikuwa wepesi kuliko tai,+Walikuwa wenye nguvu kuliko simba.+ 24  Enyi mabinti wa Israeli, mlilieni Sauli,Aliyewavisha nguo nyekundu na mapambo,Aliyetia mapambo ya dhahabu kwenye nguo zenu. 25  Jinsi wenye nguvu walivyoanguka vitani! Yonathani amelala akiwa ameuawa juu ya vilima vyenu!+ 26  Nimehuzunika kwa ajili yako, ndugu yangu Yonathani;Nilikupenda sana.+ Upendo wako kwangu ulikuwa mzuri sana kuliko upendo wa wanawake.+ 27  Jinsi wenye nguvu walivyoangukaNa silaha za vita kuangamia!”

Maelezo ya Chini

Au “kuwaua.”
Au “kupendeza.”