Kitabu cha Pili cha Samweli 16:1-23

  • Siba amchongea Mefiboshethi (1-4)

  • Shimei amtukana Daudi (5-14)

  • Absalomu ampokea Hushai (15-19)

  • Ushauri wa Ahithofeli (20-23)

16  Daudi alipokuwa amepita mbele kidogo ya kile kilele,+ Siba+ mtumishi wa Mefiboshethi+ alikuwa hapo ili kumpokea; alikuwa na punda wawili wenye matandiko, na walikuwa wamebeba mikate 200, keki 100 za zabibu kavu, keki 100 za matunda ya kiangazi,* na mtungi mkubwa wa divai.+  Mfalme akamuuliza Siba: “Kwa nini umeleta vitu hivi?” Siba akamjibu: “Punda ni kwa ajili ya nyumba ya mfalme ili wapande juu yao, mikate na matunda ya kiangazi ni kwa ajili ya vijana, na divai ni kwa ajili ya wale watakaochoka nyikani.”+  Mfalme akamuuliza: “Na mwana wa bwana wako yuko wapi?”+ Siba akamwambia mfalme: “Yuko Yerusalemu, kwa maana alisema, ‘Leo nyumba ya Israeli itanirudishia utawala wa kifalme wa baba yangu.’”+  Ndipo mfalme akamwambia Siba: “Tazama! Mali yote ya Mefiboshethi ni yako.”+ Siba akasema: “Nainama mbele yako. Acha nipate kibali machoni pako, bwana wangu mfalme.”+  Mfalme Daudi alipofika Bahurimu, mtu fulani kutoka katika ukoo wa nyumba ya Sauli anayeitwa Shimei,+ mwana wa Gera, akaja kumtukana Daudi huku akimkaribia.+  Alikuwa akimtupia Daudi mawe, na watumishi wote wa Mfalme Daudi, pamoja na watu wote na wanaume mashujaa waliokuwa upande wake wa kulia na wa kushoto.  Shimei alimtukana akisema: “Ondoka, ondoka, wewe mtu mwenye hatia ya damu! Wewe mtu asiyefaa kitu!  Yehova amekulipiza kwa sababu ya hatia yote uliyopata kwa kumwaga damu ya watu wa nyumba ya Sauli, ambaye umechukua mahali pake na kutawala ukiwa mfalme, lakini Yehova anautia ufalme mikononi mwa Absalomu mwana wako. Sasa msiba umekupata kwa sababu wewe ni mtu mwenye hatia ya damu!”+  Ndipo Abishai mwana wa Seruya+ akamwambia mfalme: “Kwa nini huyu mbwa mfu+ akutukane bwana wangu mfalme?+ Tafadhali niruhusu nivuke, nikamkate kichwa.”+ 10  Lakini mfalme akasema: “Nina nini nanyi, enyi wana wa Seruya?+ Mwacheni anitukane,+ kwa sababu Yehova amemwambia,+ ‘Mtukane Daudi!’ Basi ni nani anayepaswa kumuuliza, ‘Kwa nini unafanya hivi?’” 11  Kisha Daudi akamwambia Abishai na watumishi wake wote: “Ikiwa mwanangu mwenyewe, niliyemzaa anatafuta uhai wangu,*+ je, Mbenjamini hatafanya zaidi?+ Mwacheni anitukane, kwa maana Yehova alimwambia afanye hivyo! 12  Huenda Yehova ataona mateso yangu,+ na Yehova atanilipa kwa wema badala ya matusi niliyotukanwa leo hii.”+ 13  Kwa hiyo Daudi na wanaume wake wakaendelea kuteremka barabarani huku Shimei akitembea kando ya mlima sambamba na Daudi, naye alikuwa akimtukana kwa sauti,+ akitupa mawe na kurusha mavumbi mengi. 14  Hatimaye mfalme na watu wote waliokuwa pamoja naye wakafika wakiwa wamechoka mahali walikokuwa wakienda, nao wakapumzika.* 15  Wakati huo, Absalomu na wanaume wote wa Israeli wakafika Yerusalemu, na Ahithofeli+ alikuwa pamoja naye. 16  Hushai+ Mwarki,+ rafiki ya* Daudi, alipoingia kwa Absalomu, alimwambia hivi Absalomu: “Mfalme na aishi muda mrefu!+ Mfalme na aishi muda mrefu!” 17  Ndipo Absalomu akamuuliza Hushai: “Je, huu ndio upendo mshikamanifu unaomtendea rafiki yako? Kwa nini hukwenda na rafiki yako?” 18  Basi Hushai akamwambia Absalomu: “Siwezi kufanya hivyo, ninamuunga mkono yule aliyechaguliwa na Yehova, na watu hawa, na wanaume wote wa Israeli. Nitakaa pamoja naye. 19  Na kwa mara nyingine nasema, Ninapaswa kumtumikia nani? Je, sipaswi kumtumikia mwana wake? Kama nilivyomtumikia baba yako, ndivyo nitakavyokutumikia.”+ 20  Ndipo Absalomu akamwambia Ahithofeli: “Nipe ushauri.+ Tufanye nini?” 21  Basi Ahithofeli akamwambia Absalomu: “Fanya ngono na masuria wa baba yako,+ aliowaacha waitunze nyumba.*+ Kisha Waisraeli wote watasikia kwamba umekuwa uvundo kwa baba yako, na wale wanaokuunga mkono watapata nguvu.” 22  Kwa hiyo wakampigia hema Absalomu juu ya paa,+ naye Absalomu akafanya ngono na masuria wa baba yake+ Waisraeli wote wakitazama.+ 23  Siku hizo, ushauri uliotolewa na Ahithofeli+ ulionwa kama neno la* Mungu wa kweli. Hivyo ndivyo ushauri wote wa Ahithofeli ulivyothaminiwa, na Daudi na pia Absalomu.

Maelezo ya Chini

Hasa tini na labda pia tende.
Au “nafsi yangu.”
Tnn., “wakajiburudisha.”
Au “msiri wa.”
Au “walitunze jumba la mfalme.”
Au “ulionwa kama ushauri uliotafutwa kutoka kwa.”