Kitabu cha Pili cha Samweli 17:1-29

  • Hushai avuruga ushauri wa Ahithofeli (1-14)

  • Daudi aonywa; amtoroka Absalomu (15-29)

    • Barzilai na wengine wamletea vyakula (27-29)

17  Kisha Ahithofeli akamwambia Absalomu: “Tafadhali, niruhusu nichague wanaume 12,000 niende kumfuatia Daudi usiku wa leo.  Nitamkuta akiwa amechoka na akiwa dhaifu,*+ kisha nitamtia woga; na watu wote walio pamoja naye watakimbia, nami nitamuua mfalme peke yake.+  Halafu nitawarudisha watu wote kwako. Kurudi kwa watu wote kunategemea kitakachompata mtu unayemtafuta. Kisha watu wote watakuwa na amani.”  Pendekezo hilo lilikuwa zuri kabisa machoni pa Absalomu na wazee wote wa Israeli.  Hata hivyo, Absalomu akasema: “Tafadhali, mwiteni pia Hushai+ Mwarki, tusikie jambo atakalosema.”  Basi Hushai akaja kwa Absalomu. Kisha Absalomu akamwambia: “Huu ndio ushauri uliotolewa na Ahithofeli. Je, tufuate ushauri wake? Kama sivyo, tuambie jambo la kufanya.”  Ndipo Hushai akamwambia Absalomu: “Wakati huu, ushauri uliotolewa na Ahithofeli si mzuri!”+  Hushai akaendelea kusema: “Unajua vizuri kwamba baba yako na wanaume wake ni mashujaa,+ na wana hasira* kama dubu aliyepoteza watoto wake porini.+ Isitoshe, baba yako ni mpiganaji hodari,+ naye hatakaa usiku kucha na watu.  Sasa hivi amejificha ndani ya mojawapo ya mapango* au mahali pengine;+ ikiwa atakuwa wa kwanza kutushambulia, wale watakaosikia habari hiyo watasema, ‘Watu wanaomfuata Absalomu wameshindwa!’ 10  Hata mwanamume jasiri aliye na moyo kama wa simba+ hakika atanyong’onyea kwa woga, kwa maana Waisraeli wote wanajua kwamba baba yako ni mwanamume shujaa+ na kwamba wanaume walio pamoja naye ni jasiri. 11  Natoa ushauri huu: Waisraeli wote na wakusanyike kwako, kuanzia Dani mpaka Beer-sheba,+ wengi kama chembe za mchanga kwenye ufuo wa bahari,+ nawe uwaongoze vitani. 12  Tutamshambulia mahali popote atakapopatikana, nasi tutamwangukia kama umande unavyoanguka ardhini; na hakuna hata mmoja wao atakayeokoka, wala yeye wala mwanamume yeyote aliye pamoja naye. 13  Ikiwa atakimbilia jiji fulani, Waisraeli wote watachukua kamba na kwenda katika jiji hilo na kuliburuta mpaka bondeni, na hakuna hata jiwe dogo litakalobaki.” 14  Ndipo Absalomu na wanaume wote wa Israeli wakasema: “Ushauri wa Hushai Mwarki ni bora+ kuliko ushauri wa Ahithofeli!” Kwa maana Yehova alikuwa ameazimia* kuvuruga ushauri mzuri wa Ahithofeli,+ ili Yehova amletee msiba Absalomu.+ 15  Baadaye Hushai akamwambia Sadoki na Abiathari+ waliokuwa makuhani: “Hivi ndivyo Ahithofeli alivyomshauri Absalomu na wazee wa Israeli, na hivi ndivyo nilivyowashauri. 16  Sasa tumeni ujumbe haraka kwa Daudi na kumwonya hivi: ‘Usikae kwenye vivuko vilivyo nyikani usiku wa leo, lakini hakikisha umevuka, usipofanya hivyo, wewe mfalme na watu wote walio pamoja nawe mtaangamizwa.’”*+ 17  Yonathani+ na Ahimaazi+ walikuwa wakikaa En-rogeli;+ basi kijakazi fulani akaenda na kuwaambia, nao wakaenda kumwambia Mfalme Daudi kwa maana hawakutaka kujihatarisha kwa kuonekana wakiingia jijini. 18  Hata hivyo, kijana fulani akawaona na kumwambia Absalomu. Basi wote wawili wakaondoka haraka na kwenda mpaka kwenye nyumba ya mtu fulani huko Bahurimu+ aliyekuwa na kisima katika ua wa nyumba yake. Wakaingia kisimani, 19  kisha mke wa mwanamume huyo akakifunika kisima hicho na kuweka chengachenga za nafaka juu yake; hakuna aliyejua jambo hilo. 20  Watumishi wa Absalomu wakaja kwa mwanamke huyo nyumbani kwake na kumuuliza: “Ahimaazi na Yonathani wako wapi?” Mwanamke huyo akawajibu: “Walipita hapa wakaenda kwenye maji.”+ Kisha wanaume hao wakawatafuta lakini hawakuwapata, basi wakarudi Yerusalemu. 21  Baada ya wanaume hao kwenda zao, walitoka kisimani na kwenda kumjulisha Mfalme Daudi. Wakamwambia: “Ondoka, uvuke haraka maji haya, kwa maana Ahithofeli ametoa ushauri dhidi yako.”+ 22  Mara moja Daudi na watu wote waliokuwa pamoja naye wakaondoka na kuvuka Yordani. Wakati wa mapambazuko, hapakuwa na mtu hata mmoja ambaye hakuwa amevuka Yordani. 23  Ahithofeli alipoona kwamba ushauri wake haukufuatwa, aliweka matandiko juu ya punda wake na kwenda nyumbani kwake katika mji wao.+ Baada ya kuwapa maagizo watu wa nyumbani mwake,+ akajitia kitanzi.*+ Basi akafa na kuzikwa katika makaburi ya mababu zake. 24  Wakati huo, Daudi akaenda Mahanaimu,+ naye Absalomu akavuka Yordani pamoja na wanaume wote wa Israeli. 25  Absalomu alimweka Amasa+ kuwa msimamizi wa jeshi badala ya Yoabu;+ Amasa alikuwa mwana wa mwanamume Mwisraeli aliyeitwa Ithra, aliyelala na Abigaili,+ binti ya Nahashi, dada ya Seruya, mama ya Yoabu. 26  Waisraeli na Absalomu wakapiga kambi katika nchi ya Gileadi.+ 27  Mara tu Daudi alipofika Mahanaimu, Shobi mwana wa Nahashi kutoka katika jiji la Raba+ la Waamoni, Makiri+ mwana wa Amieli kutoka Lo-debari, na Barzilai+ Mgileadi kutoka Rogelimu 28  wakaleta vitanda, mabeseni, vyungu, ngano, shayiri, unga, nafaka iliyokaangwa, maharagwe mapana, dengu, nafaka iliyokauka, 29  asali, siagi, kondoo, na jibini. Walimletea vitu hivyo vyote Daudi na watu waliokuwa pamoja naye ili wale,+ kwa maana walisema: “Watu wana njaa, wamechoka, na wana kiu nyikani.”+

Maelezo ya Chini

Au “amedhoofika mikono yote miwili.”
Au “na wana uchungu nafsini.”
Au “mashimo; mabonde.”
Au “amekusudia.”
Tnn., “mtamezwa.”
Au “akajinyonga.”