Kitabu cha Pili cha Samweli 2:1-32

  • Daudi, mfalme wa Yuda (1-7)

  • Ish-boshethi, mfalme wa Israeli (8-11)

  • Vita kati ya nyumba ya Daudi na nyumba ya Sauli (12-32)

2  Baadaye Daudi akamuuliza hivi Yehova:+ “Je, nipande kwenda katika mojawapo ya majiji ya Yuda?” Yehova akamwambia: “Panda uende.” Kisha Daudi akamuuliza: “Niende wapi?” Akajibu: “Hebroni.”+  Basi Daudi akapanda kwenda huko na wake zake wawili, Ahinoamu+ wa Yezreeli na Abigaili+ mjane wa Nabali Mkarmeli.  Daudi akawachukua pia wanaume waliokuwa pamoja naye,+ kila mmoja na familia yake, nao wakakaa katika majiji yanayozunguka Hebroni.  Kisha wanaume wa Yuda wakaja, na huko wakamtia mafuta Daudi awe mfalme juu ya nyumba ya Yuda.+ Wakamwambia Daudi: “Watu wa Yabesh-gileadi ndio waliomzika Sauli.”  Basi Daudi akawatuma wajumbe kwa watu wa Yabesh-gileadi na kuwaambia: “Yehova na awabariki, kwa sababu mlimtendea bwana wenu, Sauli, kwa upendo mshikamanifu kwa kumzika.+  Yehova na awatendee kwa upendo mshikamanifu na uaminifu. Mimi pia nitawatendea fadhili kwa sababu mmefanya jambo hili.+  Sasa mikono yenu na iwe na nguvu, nanyi muwe jasiri kwa sababu bwana wenu Sauli amekufa, na nyumba ya Yuda imenitia mafuta niwe mfalme juu yao.”  Lakini Abneri+ mwana wa Neri mkuu wa jeshi la Sauli, alikuwa amemchukua Ish-boshethi,+ mwana wa Sauli, akamvusha mpaka Mahanaimu+  na kumfanya kuwa mfalme wa Gileadi,+ wa Waashuri, Yezreeli,+ Efraimu,+ Benjamini, na juu ya Waisraeli wote. 10  Ish-boshethi, mwana wa Sauli, alikuwa na umri wa miaka 40 alipokuwa mfalme wa Israeli, naye alitawala kwa miaka miwili. Hata hivyo, nyumba ya Yuda ilimuunga mkono Daudi.+ 11  Muda ambao Daudi alikuwa mfalme huko Hebroni juu ya nyumba ya Yuda ulikuwa miaka saba na miezi sita.+ 12  Baada ya muda Abneri mwana wa Neri na watumishi wa Ish-boshethi, mwana wa Sauli, wakatoka Mahanaimu+ na kwenda Gibeoni.+ 13  Yoabu+ mwana wa Seruya+ na watumishi wa Daudi wakaondoka pia na kukutana nao kwenye kidimbwi cha Gibeoni; kikundi kimoja kiliketi upande mmoja wa kidimbwi hicho na kikundi cha pili upande wa pili. 14  Hatimaye Abneri akamwambia hivi Yoabu: “Acha vijana wasimame na kupambana* mbele yetu.” Ndipo Yoabu akasema: “Acha wasimame.” 15  Basi wakasimama, wakahesabiwa na kuvuka, 12 wa Benjamini na Ish-boshethi mwana wa Sauli, na 12 kutoka kati ya watumishi wa Daudi. 16  Kila mmoja alimkamata mwenzake kichwani na kumchoma kwa upanga ubavuni, na wote wakaanguka pamoja. Basi mahali hapo huko Gibeoni pakaitwa Helkath-hasurimu. 17  Vita vikawa vikali sana siku hiyo, mwishowe Abneri na wanaume wa Israeli wakashindwa na watumishi wa Daudi. 18  Basi wana watatu wa Seruya+ walikuwa mahali hapo—Yoabu,+ Abishai,+ na Asaheli;+ naye Asaheli alikuwa na mbio sana* kama swala katika nchi tambarare. 19  Asaheli akamkimbiza Abneri, naye hakugeuka kulia wala kushoto alipokuwa akimkimbiza. 20  Abneri alipotazama nyuma, aliuliza: “Ni wewe Asaheli?” akajibu: “Naam, ni mimi.” 21  Ndipo Abneri akamwambia: “Nenda kulia au kushoto umkamate kijana mmoja na kuchukua vitu vyake.” Lakini Asaheli hakutaka kuacha kumkimbiza. 22  Basi Abneri akamwambia tena Asaheli: “Acha kunikimbiza. Kwa nini nikuue? Nitawezaje kumtazama usoni ndugu yako Yoabu?” 23  Lakini hakuacha kumkimbiza, basi Abneri akamchoma tumboni kwa ncha ya nyuma ya mkuki,+ na mkuki huo ukatokea mgongoni mwake; akaanguka na kufa papo hapo. Kila mtu aliyefika mahali ambapo Asaheli alianguka na kufa alisimama hapo kwa muda. 24  Kisha Yoabu na Abishai wakaenda kumfuatia Abneri. Jua lilipokuwa likitua, wakafika kwenye kilima cha Ama, kilicho ng’ambo ya Gia kwenye njia inayoelekea katika nyika ya Gibeoni. 25  Wabenjamini wakakusanyika huko na kumfuata Abneri, wakawa kundi moja, nao wakajiimarisha juu ya kilima fulani. 26  Kisha Abneri akamwita Yoabu na kumuuliza: “Je, upanga utaendelea kuangamiza* bila kukoma? Je, hujui kwamba mwisho utakuwa mchungu tu? Basi, utangoja kwa muda gani ndipo uwaambie watu waache kuwafuatia ndugu zao?” 27  Yoabu akamwambia: “Kwa hakika kama Mungu wa kweli anavyoishi, usingesema, watu hawa wangeendelea kuwafuatia ndugu zao mpaka asubuhi.” 28  Sasa Yoabu akapiga pembe, wanaume wake wakaacha kuwafuatia Waisraeli, na vita vikakoma. 29  Kisha Abneri na watu wake wakapiga mwendo kupitia Araba+ usiku huo wote, wakavuka Yordani na kupiga mwendo kupitia katika bonde lote* na mwishowe wakafika Mahanaimu.+ 30  Baada ya Yoabu kuacha kumfuatia Abneri, akawakusanya watu wote pamoja. Watumishi 19 wa Daudi walikosekana kutia ndani Asaheli. 31  Lakini watumishi wa Daudi walikuwa wamewashinda Wabenjamini na wanaume wa Abneri, na wanaume 360 kati yao walikuwa wameuawa. 32  Wakamchukua Asaheli+ na kumzika katika kaburi la baba yake huko Bethlehemu.+ Kisha Yoabu na wanaume wake wakapiga mwendo usiku kucha, wakafika Hebroni+ wakati wa mapambazuko.

Maelezo ya Chini

Au “kushindana.”
Tnn., “alikuwa na miguu myepesi.”
Tnn., “kunyafua.”
Au labda, “kupitia eneo lote la Bithroni.”